Monday 9 March 2015

Jkt Mbweni, Uhamiaji, Ruvu kukabidhiwa bendera leo


Timu ya JKT Mbweni wakiwa na Kombe lao la Mapinduzi.

Na Mwandishi Wetu
WAWAKILISHI wa Tanzania Bara katika mashindano ya netiboli ya Afrika Mashariki yatakayofanyika Zanzibar Jumamosi hii, wanakabidhiwa bendera leo Jumanne kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Timu hizo zitakazoshiriki mashindano hayo ni pamoja na mabingwa wa Bara JKT Mbweni, Uhamiaji Tanzania na JKT Ruvu inayoundwa na wachezaji chipukizi.

Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta), Annie Kibira alisema mwishoni mwa wiki kuwa, kabla ya kukabidhiwa bendera hiyo, timu hizo asubuhi zitapambana katika bonanza maalum kwa ajili ya kujipima nguvu.

Alisema timu hizo zitachuana katika bonanza hilo na baadae mchana watakabidhiwa bendera ya taifa kwa ajili ya kuliwakilisha nchi katika mashindano hayo ya Afrika Mashariki.

Alisema kuwa mgeni rasmi anatarajia kuwa mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) Dioniz Malinzi ambaye atakabidhi bendera kwa timu hizo.

Wiki iliyopita kocha wa JKT Mbweni Anna Shayo alisema kuwa lengo lao mwaka huu ni kumaliza ukame wa kutobeba kombe hilo baada ya mwaka jana kushika nafasi ya pili katika mashindano yaliyofanyika Nairobi.

No comments:

Post a Comment