Monday 24 June 2019

Serikali Yaweka Mikakati Viwanja vya Ndege

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Issac Kamwelwe leo akifungua Jukwaa la Pili la Kitaifa la Usafiri wa Anga linalofanyika kwa siku mbili kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imesema imeweka mipango kabambe ya kuboresha viwanja vidogo vya ndege (Airstrips), ili viweze kutumika kirahisi na ndege ndogo zinazosafirisha Watalii kutembelea mbuga mbalimbali za wanyama na vivutio vilivyopo nchini.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Issac Kamwelwe katika Jukwaa la Pili la Kitaifa la Usafiri wa Anga linaloendelea kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), ambapo tayari imeundwa kamati kutembelea viwanja hivyo, ambavyo amesema vipo zaidi ya 600 vikiwemo vya makampuni binafsi.

“Hivi viwanja ndivyo vinavyoingiza Watalii ndani ya mbuga na vivutio vingine baada ya kushuka pale KIA (Kilimanjaro International Airport) na hapa Dar es Salaam Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), sasa hivi vinatakiwa viwe katika ubora mzuri utakaofanya Watalii kujiona wapo sehemu nzuri na salama,” amesisitiza Mhandisi Kamwelwe.
Wadau mbalimbali wa masuala ya usafiri wa anga leo kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC),  wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi wa Jukwaa la Pili la Kitaifa la Usafiri wa Anga, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Issac Kamwelwe.

Hata hivyo, Mhandisi Kamwelwe amesema Idara ya Uhandisi ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), itaimarishwa zaidi ili iweze kufanya marekebisho kwenye viwanja hivi, ikiwezekana kununuliwa vifaa ili kufanya kazi kwa ufanisi.

Pia amesema tayari Serikali imeweza kusimamia vyema mradi wa ujenzi wa Jengo la Tatu la abiria la JNIA, ambao umekamilika na limeongeza uwezo wa kuhudumia abiria, ambapo itahudumia abiria milioni sita kwa mwaka badala ya milioni 2 waliokuwa wakihudumia na Terminal 2.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Vedastus Fabian (kushoto) akiwasikiliza Maafisa Naomi Mbilinyi na Gladston Mlay (kulia), kutoka Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), katika maonesho yanayokwenda sambamba na Jukwaa la Pili la Kimataifa la Usafiri wa Anga linalofanyika kwa siku mbili mfululizo kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC). 
“Ninawataka wafanyabiashara na wadau wengine wote kuchangamkia fursa za kibiashara zilizopo kwenye jengo letu hili la kisasa, ambapo sasa nimetaarifiwa wapo katika hatua za kuwapata watoa huduma ndio maana ninasema mjitokeze kwa wingi kuomba,” amesema Mhandisi Kamwelwe.
Dkt Bartholomew Rufunjo (kulia) leo akipata maelezo mbalimbali kuhusiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kutoka kwa Mhandisi Astelius John (kushoto), kwenye maonesho yanayokwenda sambamba na Jukwaa la Pili la Kitaifa la Usafiri wa Anga yanayofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC). Wengine pichani ni Afisa Masoko wa TAA, Pendo Mwakilasa akizungumza na Mtendaji Mkuu wa VIA Aviation Ltd, Suzan Mashibe.

Akizungumzia viwanja vingine amesema baada ya kukamilika kwa upanuzi na ukarabati wa viwanja vya ndege vya Songwe na Mwanza vitawekwa katika daraja la Kimataifa, kutokana na kuwa na miundombinu ya kisasa, ambapo kwa upande wa Mwanza ujenzi wa jengo la mizigo upo katika hatua ya mwisho kukamilika.

  1. Mhandisi Astelius John na Afisa Masoko, Pendo Mwakilasa wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (kushoto), leo wakiwaeleza masuala mbalimbali ya viwanja vya ndege wadau waliotembelea meza ya maonesho yanayokwenda sambamba na Jukwaa la Pili la Kitaifa la Usafiri wa Anga yanayofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC).
Kwa sasa kiwanja cha ndege cha Songwe kipo daraja 3C na yakikamilika maboresho ya miundombinu kitakuwa daraja la 4D na Mwanza ni daraja 4C.

Sunday 16 June 2019

Mbwana Samatta Atakiwa Lazio Kwa Bilioni 41.2


ROME, Italia
NAHODHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, na mshambuliaji wa Genk ya Ubelgiji Mbwana Samatta ni mmoja mwa wachezaji waliotangazwa hivi karibuni kabisa kusakwa na Lazio kwa ajili ya usajili wa kipindi hiki cha majira ya joto.

Samatta alifunga mabao 20 katika mechi 28 alizocheza katika Ligi Kuu ya Ubegiji msimu uliopita, huku akisaidia mara tatu. Baada ya kusaini Genk akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa ada ya uhamisho na kiasi cha sh bilioni 2, Samatta sasa ana thamani ya zaidi ya sh bilioni 30 na Lazio wako tayari kumchukua kwa sh bilioni 41.2.

Mkataba wa Samatta Genk unamalizika mwakani na itakuwa kazi kubwa kumchukua mchezaji huyo kumpeleka Rome katika kipindi hiki cha majira ya joto.

Lazio ni klabu ya Italia yenye maskani yake jijini Rome nchini humo, na inajulikana sana kwa shughuli zake za soka katika eneo hilo na inashiriki katika Ligi Kuu ya Italia ya Serie A.

Lazio imewahi kutwa taji la Ligi Kuu ya Italia mara mbili (mwaka 1974 na 2000), na wamewahi kushinda taji la Coppa Italia mara saba na mara nne lile la Supercoppa Italiana, na wamewahi kuwa mabingwa wa Kombe la Ligi ya Mabingwa pamoja na lile la Super Cup katika wakati mmoja.

Klabu kadhaa zinazoshiriki Ligi Kuu ya England, ikiwemo West Ham tayari zimeonesha nia ya kutaka kumsajili mchezaji huyo wazamani wa Simba na TP Mazembe.


Saturday 15 June 2019

Amunike Atamba Kutinga Raundi ya Pili Afcon 2019


CAIRO, Misri
KOCHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mnigeria Emmanuel Amunike (pichani) amesema kuwa kikosi chake kitafanya kila kitu kuhakikisha kinacheza raundi ya pili ya mashindano ya Mataifa ya Kombe la Afrika (Afcon 2019).

Licha ya kucheza vizuri katika safu ya ulinzi, timu hiyo ya Tanzania ilipoteza mchezo wake wa kimataifa wa kirafiki kwa kufungwa 1-0 dhidi ya Misri uliofanyika Alhamisi jijini Alexandria ukiwa ni mchezo wao wa kwanza wa kujipima nguvu kabla ya kuanza kwa fainali hizo za Afcon 2019.

Fainali hizo za Mataifa ya Afrika zinafanyika nchini Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19 na kwa mara ya kwanza zikishirikisha jumla ya timu 24 badala ya 16 za awali.

Tanzania inatarajia kucheza mchezo wake wa pili wa marudiano utakaofanyika leo Jumapili dhidi ya Zimbabwe, ikiwa ni wiki moja kabla ya kuanza kutimua vumbi kwa fainali hizo za Afcon 2019.

Taifa Stars imepangwa katika kundi gumu la C pamoja na vigogo wa Afrika, Senegal na Algeria pamoja na nchi jirani ya Kenya.

Amunike alithibitisha walipata kila walichotarajia katika mchezo wao dhidi ya Misri na aliahidi kuwa watafanya kila wawezavyo kucheza raundi ya pili ya mashindano hayo.

“Tulicheza vzuri dhidi ya Misri na kuwabana, tulifanikiwa. Lengo letu ni kuimarisha kikosi chetu kadiri tuwezavyo, “alisema gwiji huyo wa Zamalek na nyota wazamani wa Barcelona.

“Bila shaka tunacheza katika kundi ngumu, lakini tutafanya kila tuwezalo kufuzu kucheza raundi ya pili ya mashindano hayo.

“Sifikiri kama Senegal itakuwa timu dhaifu bila ya kuwa na Mane, ni mchezaji mkubwa lakini wana wachezaji wengine wakubwa katika kikosi chao, ambacho kinaweza kutwaa taji la Afcon, “alikamilisha maelezo yake.

Tanzania itaanza kampeni zake kwa kucheza mchezo wake wa kwanza katika fainali za mwaka huu za Afco baada ya kutocheza kwa miaka 39 Juni 23 kwa kucheza dhidi ya Senegal kwenye Uwanja wa Juni 30.

Wakati huohuo, nahodha wa Misri Ahmed Elmohamady alisema kuwa ushindi dhidi ya Taifa Stars ni muhimu inasaidia wachezaji, benchi la ufundi na hata mashabiki kujiamini kabla ya kuanza rasmi kwa faiali hizo za Afcon 2019.

Kocha alijaribu mifumo tofauti tofauti na kubaini baadhi ya kasoro ambazo atazifanyia kazi na kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri katika mashindano hayo yanayofanyika katika ardhi yao ya nyumbani.

Elmohamady ndiye aliyefunga bao pekee wakati Misri ikishinda 1-0 dhidi ya Tanzania kwa ajili ya maandalizi ya mashindano hayo.

Misri leo inacheza mchezo wa mwisho wa kirafiki dhidi ya timu ya Guinea ya Naby Keita.

Mawakala wa Tigo Pesa Wajishindia Mamilioni

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kifedha wa Tigo Pesa, Angelica Pesha (katikati) akizungumza na waandishi wa habari. Kushoto ni Wakala wa Pwani, Suleiman Hussein na kulia ni Vicky Ibrahim aliyejishindia sh milioni 2.5.


Na Mwandishi Wetu
ZAIDI ya mawakala 200 wa huduma ya Tigo Pesa, wamejishindia zawadi za fedha taslimu zaidi ya sh milioni 160 kwenye promosheni ya mwezi mmoja inayojulikana kama ‘Wakala Cash In Promotion’.

Promosheni hiyo ya nchi nzima iliyozinduliwa mwezi uliopita, ililenga kuwahimiza Mawakala wa Tigo Pesa nchini kufanya miamala kwa wingi ili kuweza kujishindia zawadi za fedha taslimu.

Akiwakabidhi zawadi washindi wa promosheni hiyo, kaimu mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kifedha wa Tigo Pesa, Angelica Pesha alisema, kampuni ya Tigo inathamini juhudi kubwa zinazofanywa na mawakala na kuongeza kuwa promosheni hiyo ililenga kuwazadia mawakala kutokana na kazi nzuri wanayoifanya.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kifedha wa Tigo Pesa, Angelica Pesha (kulia) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh milioni 3.5 Wakala wa Pwani, Suleiman Hussein wakati wa hafla ya kuwakabidhi  zawadi mawakala walioshinda. Hussein alikabidhia sh milioni 3.5  jijini Dar es Salaam.
“Kampeni hii siyo tu inaonyesha dhamira yetu ya kuwekeza kwenye biashara lakini pia adhma yetu ya kugawana tunachokipata kutokana na biashara tunayofanya pamoja na wadau wetu. Promosheni hii ni fursa nyingine ya kuwazawadia mawakala wetu fedha taslimu na bonasi  ambazo tunawaamini zitawapa moyo wa kufanya kazi kwa bidii zaidi ili kuendelea kufikisha huduma jumuifu za kifedha kwa wananchi wengi zaidi,” alisema.

Kwa mujibu wa Pesha, pamoja na washindi wengine, washindi wawili wakubwa kutoka kila Kanda walipatikana ambao ni Suleiman Hussein na Vicky Ibrahim kutoka Kanda ya Pwani, Peter Myovela na Stivin Katoto kutoka Kanda ya Kusini, Anton Masawe na Athuman Mbwana kutoka Kanda ya Kaskazini pamona na Harry Lwila na Joseph Kabeba kutoka Kanda ya Ziwa.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kifedha wa Tigo Pesa, Angelica Pesha (kulia) akimkaabidhi Wakala wa Tigo Pesa, Vicky Ibrahim  mfano wa hundi yenye thamani ya sh milioni 2.5.
“Pamoja na washindi 2000 ambao wamejinyakulia zawadi mbali mbali za fedha taslimu kutokana na juhudi zao, tumepata washindi wengine wawili wakubwa kutoka katika kila kanda ambao kwa jumla wao ni nane, ambao wameweza kujishindia sh milioni 12 zaidi kutokana na jitihada zao. 

Tunawapongeza sana Mawakala wote ambao wamefanya vizuri na kujishindia zawadi na kwa wale ambao wahakuweza kushinda waongeze bidii ili waweze kuwa washindi katika promosheni zijazo,” alisema.

Akipokea zawadi ya sh milioni 3.5, Suleiman Hussein ambaye ni Wakala kutoka Kanda ya Pwani alisema: “Napenda kuishukuru sana kampuni ya Tigo. Promosheni hii inaonesha ni kwa kiasi gani sisi mawakala ni kiungo muhimu kwenye huduma nzima ya Tigo Pesa. Kuibuka mshindi kwenye promosheni hii ni rahisi sana kwa kuwa unahitajika kufanya kazi kwa bidii tu. Nawashauri Mawakala wenzangu wafanye kazi kwa bidi, kwani Tigo Pesa inalipa,”
Washinfi wa shindano la Mawakala wa Tigo Pewa, Suleiman Hussein (kushoto) na Vicky Ibrahim wakiwa na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kifedha wa Tigo Pesa, Angelica Pesha (katikati) , baada ya kukabidhiwa mfani wa hundi katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam. Hussein alipata sh milioni 3.5.
Vicky Ibrahim, Wakala aliyejishindia sh milioni 2.5 alisema amefurahi kuwa mshindi wa zawadi hiyo na kuwataka wanawake kuwa mawakala wa Tigo Pesa na wale ambao tayari ni mawakala kuwekeza zaidi na kufanya kazi kwa bidii kwa kuwa Tigo Pesa inalipa.
“Tigo Pesa imetuwezesha sisi wanawake kujiajiri na kuboresha maisha yetu. Nawashauri wanawake wenzangu kujiajiri au kujiongezea vipato vyao kupitia Tigo Pesa. Kwa kuwa Mawakala pia wanaweza kujishindia zawadi kupitia promoshei hii kama ambavyo mimi nilivyojishi,” alisema.

Wednesday 12 June 2019

Kwandika Awataka TAA Kufanya Kazi Kwa Ufanisi


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
NAIBU Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa  amewakumbusha  na kuwashauri Wafanyakazi  wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kuhusu ufanisi wa kazi na hatua zinazopaswa kuchukuliwa  ili Mamlaka hiyo  iweze kuongeza ufanisi wa kazi zaidi.

Akizungumza katika uzinduzi wa Mkutano Mkuu wa 23 wa  Baraza la Wafanyakazi leo Jijini  Dodoma Kwandikwa alisema  Baraza lina nafasi kubwa  ya kuishauri Mamlaka juu ya maslahi bora kwa Wafanyakazi.

“Naomba  mjadili changamoto mnazokutana nazo mahala pa kazi na katika utekelezaji wa mipango ili kuhakikisha mnatoa huduma bora kwa wananchi, pia mjadili kuhusu makisio ya mapato na matumizi ya Mamlaka”alisema.

Pia alitaka  Baraza hilo lisaidie katika kuleta maelewano kazini kwani Rasilimali  watu ni muhimu katika kusimamia Rasilimali zingine na mipango katika Taasisi.

“Lazima tufanye kazi kwa umoja ili tuweze kupiga hatua, kwahiyo uwepo wenu ni muhimu  katika kujadiliana namna ya kuendeleza Taasisi kwa kushirikiana”alisema.
 
Pia Kwandikwa alisema Baraza liweke mazingira ya kuongeza tija kwa Watumishi wanaotimiza majukumu yao ambapo lengo ni kutambua mchango wao na kuuthamini.

“Watumishi pia watimize majukumu yao kwa weledi kwa kuzingatia sheria kanuni na taratibu za Utumishi wa umma”alisema.

Katika hatua nyingine Kwandikwa amewataka wafanyakazi wa Mamlaka  wafanye  maandalizi juu ya ufunguzi wa Jengo la tatu la abiria.

“Endeleeni kufanya uchunguzi juu ya vihatarishi vinavyoweza kujitokeza baada ya kuanza matumizi ya jengo hilo,na  mshirikishane na kudhibiti mapema vihatarishi hivyo”alisema.

Pia aliwataka Watumishi sekta ya Anga kufanya kazi kwa weledi ili kuboresha huduma za usafiri wa Anga ili kuongeza ushindani wa Kitaifa na Kimataifa.

Pia alisisitiza kuwa ni  muhimu  Watumishi wa Mamlaka kujitambua kuwa  wanamchango katika kukuza pato la Taifa kutokana na huduma wanazotoa ambazo  zina  mchango Mkubwa katika ujenzi wa Taifa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi aliainisha baadhi ya changamoto zinazoitatiza Taasisi kuwa ni maslahi duni kwa Wafanyakazi, uchache wa Wafanyakazi pamoja na nyenzo za ufanyaji kazi kama magari ya Zimamoto.

Ambapo Kwandikwa alisema “Serikali itafanyia kazi changamoto hizo ili kuhakikisha inaboresha sekta ya Usafiri wa Anga huku akitoa wa wito kufanya kazi kwa bidii na  weledi mkubwa huku akisisitiza Maazimio ya Baraza hilo yale ambayo yamekuwa changamoto yawe fursa ili yaweze kufanyiwa kazi.

Mkutano huo wa 23 wa Baraza kuu la Wafanyakazi unafanyika kwa kwa siku mbili katika ukumbi wa Takwimu Jijini hapa.

Friday 7 June 2019

Michezo Yote 52 ya Afcon 2019 Mubashara DStv



1.        Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya MultiChoice Tanzania Balozi Ami Mpungwe {Kulia} sambamba na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Jacqueline Woiso , akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo maalum ya Afcon 2019 ijulikanayo kama “DStv Tupogo”.


Na Mwandishi Wetu
HUKU zikiwa zimebaki siku chache kabla ya kuanza kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, Misri, Kampuni ya MultiChoice Tanzania (DStv) imetangaza rasmi kampeni maalumu kwa Watanzania itakayowawezesha kushuhudia michezo yote 52 ya mashindano ya Kombe hilo mubashara kupitia chaneli za Supersport zilizo katika mfumo wa HD.

Akizungumza katika hafla ya kuzindua kampeni hiyo ya DStv ijulikanayo kama ‘DStv Tupogo’ hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice Tanzania Jacqueline Woiso amesema wana furaha kubwa kupata fursa hiyo.

“Tuna furaha kubwa kwa nchi yetu kupata fursa ya kushiriki katika michuano hii ya kimataifa baada ya takribani miaka 39 toka iliposhiriki kwa mara ya mwisho mnamo mwaka 1980. Na kama ilivyo ada, ni jukumu letu na la kila Mtanzania kuhakikisha kuwa tunawatia moyo vijana wetu na kuifanya nchi yetu ifanye vizuri katika michuano hii ya kimataifa.
 
1.        Baadhi ya wachambuzi wa Kiswahili wa Supersport  wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa utambulisho wa mchambuzi mpya mwadada Salama Jabir.


Kwa kuzingatia hilo DStv imehakikisha kuwa mechi zote 52 za michauano hii ya kimataifa ya Afcon 2019 itarushwa mubashara DStv kupitia chaneli za Supersport na kwa lugha adhimu ya Kiswahili  na katika mfumo wa HD. 

Zaidi ya hayo, DStv imehakikisha kuwa mechi hizo zinaonekana katika vifurushi vyote kuanzia kile cha  DStv Bomba cha Sh. 19,000 tu. “Tumehakikisha kuwa mechi hizi zinakuwepo hadi kwenye kifurushi cha chini kabisa ili kuwawezesha watanzania wengi kushuhudia mtanange huo na kuwa sehemu ya historia ya nchi yetu kwani tunashiriki baada ya zaidi ya miaka 30”, alisema Jacqueline.

Sambamba na uzinduzi huo pia ulifanyika utambulisho wa wachambuzi wa Kiswahili wa Supersport, ambapo kwa mara ya kwanza mwanadada Salama Jabir ataungana na timu hiyo katika kuongeza ladha na vionjo na hivyo kuongeza burudani na msisimko wa watazamaji. Wenginde ni wachambuzi mahairi akiwemo Aboubakar Liongo, Ibrahim Maestro, Edo Kumwembe, Maulid Kitenge pamoja na Oscar Oscar.

1.        Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo Dk Yussuf Singo akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni maalum ya Afcon 2019 ya “DStv Tupogo”.

 Akielezea zaidi jinsi Watanzania watakavyopata uhundo huo,  Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Ronald Baraka Shelukindo amesema, “Wateja wa DStv pia wateweza kupokea matangazo ya moja kwa moja kwa kupitia application ya “DStv Now” kupitia katika vifaa mbalimbali ikiwamo  simu ya mkononi, lap top au tablet na televisheni ya kawaida”. Amesema kwa kutumia DStv Now, mteja anaweza kuunganisha vifaa hadi vine kwa wakati mmoja bila grarama yoyote ya ziada katika kifurushi chake.

 Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo Dk Yussuf Singo amesema kuwa kitendo cha DStv kuonesha mubashara michuano hiyo ni cha kupongezwa kwani ni sifa kubwa kwa nchi yetu. Pia amesema mchango mkubwa unaotolewa na MultiChoice Tanzania katika sekta ya michezo umechangia sana katika kukuza michezo na kuliletea taifa sifa kubwa.

1.        Baadhi ya wachezaji wa zamani timu ya Taifa walioshiriki katika mashindano ya Afcon 1980, wakiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi na Maendeleo ya Michezo wizara  Dk Omar Singo sambamba na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Multihoice Tanzania,  Balozi Ami Mpungwe na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Jacqueline Woiso.

 “Serikali inathamini sana michango ya aina mbalimbali inayotolewa na wadau kama DStv katika kukuza michezo hapa nchini. Tunaamini kuwa kwa ushirikiano huu mafanikia haya ambayo tumeanza kuyapata yataendelea na tutafikia azma yetu ya kuwa taifa kubwa kimichezo duniani,” alisema Dk Singo.

Akiongea katika uzinduzi wa kampeni hiyo ya Tupogo Hussein Ngulungu moja kati ya wachezaji nguli waliowahi kushiriki katika michuano ya Afcon 1980, alisema kuwa, “Kwa mara ya kwanza baada ya takribani miongo minne, Tanzania imepata tena heshima kubwa ya kushiriki katika mashindano haya makubwa hivyo ni wajibu wetu sisi watanzania kuonyesha uzalendo na kuwatia moyo vijana wetu ili kuhakikisha wanafanya vyema katika michuano hii ili kuipatia sifa nchi yetu“ alisema Hussein.

Mbali na michuano ya Kombe la Afcon 2019 itakayoanza hivi karibuni, wateja wa DStv pia wataendelea kufurahia maudhui mbalimbali zikiwemo sinema na tamthilia mbalimbali kutoka nje na hapa nyumbani kama vile msimu mpya wa vichekesho vya Kitimtim, tamthilia ya HUBA, Rebeca kipindi maarufu cha Shilawadu Xtra na bila kusahau cha Maisha Yangu kinachoelezea maisha na mapito ya watu mashuhuri kutoka hapa nyumbani Tanzania vyote vikiwa vinapatikana kupitia chaneli ya Maisha Magic Bongo iliyopo katika kifurushi cha Bomba.

Thursday 6 June 2019

Ronaldo Aipeleka Ureno Fainali Ligi Mataifa ya Ulaya 2019


LISBON, Ureno
KOCHA wa timu ya taifa ya Ureno, Fernando Santos amemuelezea Cristiano Ronaldo (pichani) ni  "mchezaji wa ajabu" baada ya kuifungia timu yake mabao matatu au hat-trick na kuiwezesha kutinga fainali ya mashindano ya Ligi ya Mataifa ya Ulaya dhidi ya Uswisi.

Ureno iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 huku mabao yake yote yakifungwa na Ronaldo na sasa inasubiri kucheza fainali keshokutwa Jumapili ama na England au Uholanzi, ambazo zilitarajia kucheza jana katika nusu fainali ya pili.

Ronaldo alifunga mabao hayo katika mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Estadio do Dragao.

Ronaldo, mwenye umri wa miaka 34, aliifungia Ureno bao la kuongoza kwa mkwajui wa mpira wa adhabu katika kipindi cha kwanza, ambao ulijaa wavuni kupitia kona ya chini ya lango upande wa kulia na kumpita kipa wa Uswisi, Yann Sommer.

Hatahivyo, Uswisi walisawazisha katika kipindi cha pili kwa penalti ya utata kupitia kwa Ricardo Rodriguez baada ya mwamuzi kudai kuwa mchezaji mmoja wa Ureno aliunawa mpira wakati sio kweli licha ya kuwasiliana na mwamuzi msaidizi wa VAR.

Licha ya kuwasiliana na mwamuzi msaidizi wa VAR, lakini mwamuzi Brych alitoa penalti hiyo na kuiwezesha Uswisi kupata bao la kusawazisha.

Wenyeji waliendelea kufanya kweli licha ya mchezo huo kuonekana kama ungeongezwa muda kwani matokeo yaliendelea kuwa sare ya 1-1.

Hatahivyo, Ronaldo alidhihirisha makali yake baada ya kuujaza wavuni mpira wa kona iliyochongwa na Bernardo Silva, kabla hajafunga bao jingine sekunde 102 baadae.

Watu wengi wakiwemo makocha waliowahi kuifundisha Ureno na timu zingine ambao baadhi yao sasa ni wachambuzi wa soka, wamemuelezea Ronaldo kama mchezaji wa àjabu’ kutokana na uwezo wake licha ya umri wake kusogea.

Kocha wazamani wa Ronald wakati akiwa Sporting Lisbon, Santos anasema kuwa mchezaji huyo ana kipaji kikubwa katika soka.

"Nilikuwa kocha wake mwaka 2003 na niliona wapi anakoelekea. Nilijua kuwa ni mtu wa ajabu…”

Ureno sasa Jumapili itacheza fainali ya Ligi ya Mataifa ya Ulaya dhidi ya Uholanzi,  ambao jana usiku waliifunga England kwa mabao 3-1 katika mchezo uliochezwa hadi muda wa ziada baada ya timu hizo kutoka sare ya 1-1 katika dakika 90 za kawaida.

Kabla ya mchezo huo, Ronaldo alicheza mechi mbili tu katika timu ya Ureno kati ya nane za kimataifa, na hakutoa mchango wowote katika mechi zote za kufuzu kwa ajili ya kufuzu kwa nusu fainali.

Mbwana Samatta Anunuliwa kwa Bilioni 35 England

Mbwana Samatta (wa pili kushoto) akiwa na wachezaji wenzake wa Genk ya Ubelgiji katika moja ya mechi za Ligi  Kuu ya nchi hiyo.

LONDON, England
BRIGHTON inaongoza mbio za klabu za Ligi Kuu kutaka kunsajili mshambuliaji wa mabingwa wa soka wa Ubelgiji Genk na nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mbwana Samatta.

Timu iliyopanda daraja ya Aston Villa, Leicester, Watford pamoja na  Burnley, zote zinataka kumsajili mchezaji huyo kwa kiasi cha pauni milioni 12 (sawa na sh bilioni 35).

Na Samatta, mwenye umri wa miaka 26, anajua kuwa anataka kwenda kucheza soka katika Ligi Kuu ya England baada ya kufanya vizuri katika Ligi Kuu ya Ubelgiji msimu huu.

Mchezaji huyo alifunga mabao 23 na kuisaidia klabu yake ya Genk kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Ubelgiji pamoja na kutwaa tizo ya kiatu cha Ebeny, ambayo hutolewa kwa mchezaji bora wa Ubegiji kutoka Afrika.

Tuzo hiyo huko nyuma imewahi kuchukuliwa na Romelu Lukaku, Vincent Kompany na Michy Batshuayi.

Samatta ataiongoza Taifa Stars katika mashindano ya Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, yatakayofanyika Misri mwezi huu, ikiwa ni mara ta kwanza kwa Tanzania kushiriki tangu ilipocheza kwa mara ya mwisho mwaka 1980.

Lakini baada ya kumalizika kwa mashindano hayo, Samatta anatarajia kuondoka Genk, ambayo alijiunga nayo Januari mwaka 2016 akitokea klabu ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo ya TP Mazembe, na kwenda Ligi Kuu ya England.

Brighton imekuwa ikimfuatilia Samatta kwa muda na kocha wazamani Chris Hughton ambaye ni shabiki mkubwa, wakati Graham Potter naye pia amekuwa akimkubali mshambuliaji huyo.

Kocha mpya wa Brighton Graham Potter anataka kuimarisha kikosi chake kipya kwa ajili ya Ligi Kuu.

Samatta endapo atajiunga na Brighton atakuwemo katika ziara ya timu hiyo kabla ya kuanza kwa ligi ambayo itafanyika Austria kuanzia Julai 7 na itacheza mechi kadhaa za kirafiki.

Taifa Stars Yaenda Misri na Matumaini Kedekede


Naibu Waziri, Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Juliana Shonza akikabidhi Bendera ya Taifa kwa Nahodha wa Timu ya Taifa Stars, Mbwana Samatta jijini Dar es Salaam leo Alhamisi. Kulia ni Mkurugenzi wa Michezo, Dk Yussuf Singo. Timu hiyo inatarajia kuondoka kesho Ijumaa kwenda Misri kwa ajili ya michuano ya michuano ya mataifa Africa (Afcon).

Na Mwandishi Wetu
TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars,  inatarajiwa kuondoka leo kuelekea nchini Misri ikiwa na kikosi cha wachezaji 32 kwa ajili ya maandalizi ya fainali za Afrika, huku ikibeba matumaini ya kufanya vizuri.

Kabla ya kuanza kwa fainali hizo Juni 21, mwaka huu nchini humo, timu hiyo itaweka kambi ya wiki mbili na kucheza mechi mbili za kirafiki za kujipima nguvu dhidi ya Misri na Zimbabwe au Nigeria.

Akizungumza jana wakati anakabidhiwa bendera na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Juliana Shonza,  Nahodha wa kikosi hicho Mbwana Samatta alisema wanaenda kupambana ili kuleta sifa kwa Tanzania.

“Kwa niaba ya wachezaji tunashukuru kwa kuwa nasi hapa na kututakia heri, nafikiri haya ni mashindano makubwa kila mmoja anafahamu, tunaenda kupambana kuleta kitu kitakachoipa sifa serikali hii ya Rais John Magufuli, na tunawaomba muendelee kuwa nasi bega kwa bega kipindi chote cha mashindano,”alisema.

Kocha Mkuu Emmanuel Amunike alisema wanaenda Misri wakiwa na malengo ya kufanya vizuri na kwamba anaamini kujituma kwa wachezaji wake kunaweza kubadilisha historia nyingine, kwani kwenye mpira lolote linaweza kutokea.

“Tangu tumeanza safari hii Agosti mwaka jana hadi hapa tulipofika kumetokana na juhudi za wachezaji, leo tunaenda Misri tukiwa na ahadi na malengo ya kufanya vizuri, lolote linawezekana kama ambavyo baada ya miaka 39 imetokea,”alisema.

Alisema watu wa Tanzania wanastahili kuona mafanikio zaidi kwasababu kuna wachezaji wengi wenye vipaji.

Kocha huyo alimshukuru Waziri Shonza kwa kuwatembelea akisema kuwa wamefurahi ujio wake kwa kuwa umewapa hamasa kama timu.

Awali, Shonza aliwatakia kila la heri wachezaji hao na kusema kuwa ana matumaini watafanya vizuri na kurudi na ushindi.

Alisema macho ya Watanzania yapo kwao hivyo, waende wakapambane, waonyeshe nidhamu na kushikamana ili kuandika historia nyingine nzuri.

“Twende Misri tukashinde na serikali ya awamu ya tano iko pamoja nanyi, tunaomba msituangushe bali mkawe wazalendo mkapigane kufa au kupona kupata matokeo mazuri,”alisema.

Tuesday 4 June 2019

Arsenal, United Zawania Kumsajili Mchezaji wa PSG


LONDON, England
ARSENAL na Manchester United zinawania kumsajili mchezaji wa Paris Saint-Germain (PSG), Thomas Meunier (pichani) msimu huu, vyanzo vimeiambia ESPN FC.

PSG imeweka wazi mauzo ya mchezaji huyo ambayo itahitaji karibu pauni milioni 30 kwa mchezaji aliyebakiza miezi 12 kwenye mkataba wake.

Vyanzo vilisema, miamba hiyo ya Ligi Kuu tayari imeonyesha nia yao kwa mchezaji huyo.

Kocha wa Arsenal Unai Emery,  aliyemsajili Meunier PSG, yuko nyuma ya the Gunners kumuwania nyota huyo.

Vyanzo viliongeza, United na Arsenal zinajiandaa kupambana kwenye ligi ya Europa msimu ujao badala ya Ligi ya Mabingwa.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 aliliambia Le Parisien kuna klabu kubwa tano zimeonyesha muhitaji tangu Januari.

"PSG haijanambia kama inataka kuniuza,” alisema  Meunier. "Wanajua kwamba wananihitaji.”

"Kama klabu itaniambia 'sikiliza tunataka kukuuza, tunahitaji fedha’ basi sitacheza hapa msimu ujao.”

Wateja Tigo Kujishindia Tiketi Kuishangilia Stars Misri

Mkuu wa Bidhaa na Huduma wa Kampuni ya Simu za Mkononi ya Tigo, David Umoh (kulia) na Meneja wa Huduma za Ziada wa kampuni hiyo, Ikunda Ngowi wakati wa uzinduzi wa Promosheni ya SOKA LA AFRIKA  kwa ajili ya kujishindia tiketi za kwenda Misri kuishangilia Taifa Stars katika mashindano ya Mataifa ya Afrika, Afcon 2019. Hafla hiyo imefanyika Jijini Dar es Salaam leo.

Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Simu za Mkononi ya Tigo itapeleka mashabiki 10 wa soka kuishangilia timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, katika mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, nchini Misri, imeelezwa.

Taifa Stars, itashiriki kwa mara ya kwanza fainali hizo baada ya kushiriki mara ya mwisho miaka 39 iliyopita, wakati mashindano hayo yalipofanyikia Lagos, Nigeria mwaka 1980 na tangu wakati huo imekuwa ikiishia katika hatua ya kufuzu.

Tigo wameanzisha promosheni ya Soka la Afrika ili kupata kupata watu 10, ambao mbali na kujishindia nafasi hizo za kwenda kuishangilia Taifa Stars ikicheza Afcon 2019, pia watapata nafasi ya kuwa mamilionea.
Akizungumza na waandishi wa habari katika uzinduzi wa Soka la Afrika jijini Dar es Salaam leo, Mkuu wa Bidhaa na Huduma wa kampuni hiyo, David Umoh alisema kuwa wateja wa Tigo wanayo nafasi ya kujishindia safari ya kwenda Misri kushuhudia Kombe la Mataifa ya Afrika pamoja na zawadi za fedha taslimu.

Kampuni hiyo imetenga zaidi ya Sh Milioni 50 katika promosheni hiyo ya Soka Letu, ambapo pia kutakuwa na washindi 10, ambao watagharimiwa kila kitu kwenda kuishuhudia Taifa Stars katika michuano hiyo ya Afcon 2019.

“Tunaamini kwa kutumia mashindano haya, tunaweza kupata fursa nzuri kutoa habari, elimu na burudani kwa kutumia jukwaa la mawasiliano na huduma za kampuni hiyo katika kutumia huduma na bidhaa zetu, “alisema Umoh.
Meneja wa Huduma za Ziada wa Tigo, Ikunda Ngowi akizungum\za na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa Promosheni ya SOKA LA AFRIKA uliofanyika jijini Dar es Salaam jana. Kushoto ni Mkuu wa wa Bidhaa na Huduma wa kampuni hiyo, David Umoh.
Fainali za Afcon ni mashindano makubwa kabisa barani Afrika kwa timu za taifa, ambazo zinawaleta pamoja wachezaji wa Kiafrika wanaoshiriki ligi kubwa na zenye ushindani ndani na nje ya Afrika.

“Tunaamini itakuwa jambo zuri kwa wateja wetu kupata nafasi ya kwenda kushuhudia mashindano haya makubwa ikiwa ni pamoja na kushangilia timu yetu ya Taifa Stars itakayotuwakilisha. Tunawatakia kila la kheri, “aliongeza Umoh.

Alisema zaidi ya wateja 100 watashinda zawasi za fedha taslimu kila siku, wiki na kila mwezi kwa muda wa miezi mitatu katika shindano hilo, ambalo mshiriki atatakiwa kutuma neno SOKA kwenda 15670 ili kuweza kujibu maswali yanayohusu Afcon 2019.

Mashindano ya 32 ya Afcon 2019 yataanza Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19 na Tanzania imepangwa Kundi C pamoja na Kenya, Senegal na Algeria na itaanza kampeni zake kwa kucheza dhidi ya Senegal.