Friday 6 March 2015

Mashindano ya kuogelea kufanyika Dar



Na Mwandishi Wetu
MASHINDANO ya taifa ya kuogelea yatafanyika jijini Dar es Salaam kwa siku mbili kuanzia Machi 21, imeelezwa.

Katibu Mkuu wa Chama cha Kuogelea Tanzania (TSA) Noel Kiunsi alisema kuwa mashindano hayo ni mahsusi kwa ajili ya vijana wenye umri mbalimbali na yatafanyika katika bwawa la kuogelea litakalotangazwa  baadae.

Hatahiyo, Kiunsi alisema kuwa mwaka huu hawatafanyia mashindano hayo katika bwawa la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, huku akisisitiza muda ukifika wakati watangaza wapi watakapofanyia mashindano hayo.

Alisema lengo la mashindano hayo ni kupata wachezaji wa umri tofauti watakaounda timu za taifa zitakazoshiriki mashindano mbalimbali ya kimataifa mwaka huu.

Alisema kuwa wanatarajia jumla ya klabu 15 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzana zitashiriki katika mashindano hayo ambayo pia yatasaidia klabu kujua viwango vya wachezaji wao na kujua jinsi ya kuviongeza kwa wale vilivyoshuka au kuendelea kuwa juu kwa wale ambao havijashuka.

Alizitaja baadhi ya klabu ambazo zinatarajia kushiriki katika mashindano hayo kuwa ni pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dar Swim Team, Opac, klabu moja ya Arusha, Morogoro international School, Isamilo International School ya Mwanza, Marine Swim Club, Moshi International School na zingine.
Katibu Mkuu wa Chama cha Kuogelea Tanzania Noel Kiunsi akitoa zawadi kwa watoto walioshinda kuogelea.(Picha na Mtandao)
 Aidha, Kiunsi alisema kuwa mashindano ya Masters, ambayo yatashirikisha wachezaji wenye umri mkubwa yatafanyika jijini Dar es Salaam Mei mwaka huu katika tarehe zitakazotangazwa baadae.

No comments:

Post a Comment