Sunday 22 March 2015

Fernando Torres apiga bao Atletico ikiifunga Getafe



Fernando Torres (kulia) akichanja mbuga katika moja ya mechi za La Liga.

MADRID, Hispania
FERNANDO  Torres alifunga bao lake la kwanza katika Ligi Kuu ya Hispania ya La Liga katika kipindi cha miaka nane wakati Atletico Madrid ikiifunga Getafe bao 2-0.

Mshambuliaji huyo, aliyeshindwa kufunga katika mechi zake tisa za mwanzo tangu aliporejea katika ligi hiyo, aliungamisha wavuni mpira wa adhabu uliopigwa na Koke ndani ya dakika tatu.

Na muda mfupi kabla ya mapumziko Tiago aliwafungia wenyeji bao la pili kwa shuti la karibu na lango.
Torres alikuwa mchezaji anayeongoza kwa mabao katika timu ya Atletico katika kipindi chake cha moiaka mitano iliyopita nchini Hispania kabla hajaondoka mwaka 2007 na kuhamia Liverpool akiwa na umri wa miaka 23.

Matokeo hayo yameirejesha Atletico pointi moja nyuma ya Valencia iliyopo katika nafasi ya tatu, wakati Getafe imebaki katika nafasi ya 13 iliyokuwepo awali kabla ya mchezo huo.

Hatahivyo, mabingwa hao watetezi wa La Liga, ambao wako katika robo fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya, bado wako pointi sita nyuma ya vinara Barcelona, ambao leo watawakaribisha vigogo wenzao Real Madrid katika mchezo wa kufa mtu katika ligi hiyo.


No comments:

Post a Comment