Wednesday 11 March 2015

Mary Waya aipa Uhamiaji ubingwa Afrika Mashariki



Mary Waya (kulia), akizungumza na mwamuzi Jaquline Sikozi Uhamiaji walipocheza na JKT Mbweni na kushinda 35-22.

Na Mwandishi Wetu
TIMU ya netiboli ya Uhamiaji Tanzania imetamba kufanya vizuri katika mashindano ya Afrika Mashariki yanayoanza Jumamosi kwenye uwanja wa Gymkhana mjini Zanzibar.

Kocha Mkuu wa timu hiyo Mmalawi Mary Waya alisema kuwa timu yao imejiandaa vizuri na ni matumaini yake kuwa,watafanya vizuri sana katika mashindano hayo ya Afrika Mashariki huko Zanzibar.

Waya aliwahi kuwa kocha wa netiboli wa timu ya Filbert Bayi na aliiwezesha timu hiyo miaka miwili mfululizo kuwa mabingwa wa Tanzania Bara katika mashindano yaliyofanyika Mbeya. Pia alikuwa kocha wa Taifa Queens kwa miaka kadhaa.

Nahodha wa Uhamiaji Tanzania, Zakia Kondo (kushoto), akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema kuwa wachezaji wake wamepokea vizuri mafunzo aliyoyatoa, hivyo wanachosubiria ni mashindano tu ili waweze kutoa vichapo kwa kila watakayekutana naye.

Alisema kuwa kwa timu za Tanzania hakuna anayoigopa kwani zote anazijua michezo yao na alikuwa akizitoa jasho alipokuwa na timu ya Filbert Bayi.

Waya pia hivi karibuni alikuwa na timu ya taifa ya Malawi ambayo aliifikisha katika fainali za Michezo ya Jumuiya ya Madola iliyofanyika Glasgow, Scotland huku Tanzania ikishindwa kufuzu kwa michezo hiyo.

Mbali na Uhamiaji Tanzania, timu zingine za Tanzania Bara zitakazoshiriki mashindano hayo ni pamoja na JKT Mbweni na JKT Ruvu inayoundwa na wachezaji chipukizi.

Pia  Uhamiaji ina wachezaji watatu wa kigeni kutoka nchini Malawi, ambao wamekuja kuiongezea nguvu timu hiyo ili iweze kufanya vizuri zaidi na kuweza kupambana na timu za Kenya na Uganda ambazo zimekuwa zikitamba katika mashindano hayo kila mwaka.

Katika kudhihisha kuwa Uhamiaji imepania kufanya vizuri na makali ya Waya yameanza kufanya kazi pale timu hiyo jana ilipowafunga mabingwa wa Tanzania Bara JKT Mbweni kwa bao 35-22 katika mchezo wa kujipima nguvu uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment