Sunday 25 December 2016

Arsenal yaikaribisha West Brom katika mechi zitakazopigwa Boxing Day kesho Jumatatu



LONDON, England
ARSENAL kesho itashuka dimbani kucheza na West Brom katika moja ya mechi zitakazopigwa Boxing Day katika kinyang’anyiro cha Ligi Kuu ya England.

Hatahivyo, timu hiyo huenda ikawakosa baadhi ya wachezaji wake akiwemo kiungo Aaron Ramsey ingawa alirejea katika mazoezi baada ya kuwa nje ya uwanja kwa takribani wiki tatu kutokana na maumivu ya nyama za paja lakini timu hiyo haiku tayari kujitoa muanga kumchezesha katika mchezo huo.

Alex Oxlade-Chamberlain naye yuko nje ya uwanja kwa tatizo kama hilo lakini atarejea katika kipindi cha mwaka mpya.

Mshambuliaji Danny Welbeck, aliyekuwa nje ya uwanja kwa kipindi cha miezi saba kutokana na maumivu ya goti, amerejea katika mazoezi kamili ingawa hatachezeshwa katika mchezo huo wa Boxing Day.

Kwa upande wa wapinzani hao wa Arsenal, wenyewe wana wasiwasi wa kumkosa James Morrison baada ya kukosa mazoezi kutokana na kusumbuliwa na mafua.

Lakini beki Jonny Evans anaweza kuwemo katika mchezo huo baada ya kukosa mechi mbili kutokana na maumivu.

BAADA YA VIPIGO MFULULIZO

Baada ya vipigo mfululizo, Arsenal leo inataka kujirekebisha na kutoa zawadi ya Krismas kwa wapenzi wake kwa kuibuka na ushindi katika mchezo huo wa leo utakaofanyika kwenye Uwanja wa Emirates.

Arsenal ilipokea vipigo mfululizo kutoka kwa Everton na Manchester City, hivyo wanahitaji kurudisha imani kwa wapenzi wao kwa kuibuka na ushindi.

"Kwa kiwango cha sasa inawezekana kuwa West Brom inaweza kumaliza katika nafasi ya juu kuliko katika msimu wowote tangu mwaka 1981.

MAKOCHA WANAUZUNGUMZIAJE MCHEZO
Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger: "Hatuko katika hatari ya kwadharau wapinzani wetu hao. [kocha Tony Pulis] amefanya kazi nzuri sana.

"Wameimarika vya kutosha. Wamekuwa na mchanganyiko mzuri kati ya uwezo wao na usuala la ufundi.

"Naamini wanaendeleza uimara wao na kuimarisha nia yao ya  mchezo hasa kwa upande wa kiufundi.”

Kocha Mkuu wa West Brom, Tony Pulis: "Wakati wote ni jaribio gumu sana pale tunapokutana na Arsenal. Unatakiwa kuwa katika kiwango chako bora na itakuwa ni siku ya mapumziko.

"Tunataka mambo yetu yaende kama tunavyotaka. Wakati fulani wanafanya hivyo.”

UTABIRI WA MCHEZO HUO
Arsnal inatarajia kurejea katika njia ya ushindi ingawa inaweza kukumbana na ugumu dhidi ya West Brom, ambayo haijatoa upinzani wa mara kwa mara msimu huu.

The Baggies ilifungwa na Manchester United wikiendi iliyopita lakini waliifanya Chelsea kuwa na wakati mgumu wakati walipofungwa tamford Bridge mapema mwezi huu na watakuwa wakiangalia kurejesha tena kiwango chao, na kupata matokeo mazuri.

REKODI ZA TIMU HIZO
 West Brom imeifunga Arsenal mara tatu tu katika mechi 20 timu hizo zilipokutana katika Ligi Kuu ya England.

 Arsenal imepoteza mchezo mara moja tu kati ya mechi 11 zilizopita dhidi ya West Brom, lakini hizo ni msimu uliopita wakati Arsenal ilipokuwa mgeni kwenye Uwanja wa Hawthorns, wakati walipokuwa mbdele kwa bao 1-0 lakini walipoteza kwa 2-1.

 Kwa mara ya mwisho timu hizo zilikutana katika oxing Day ilikuwa mwaka  2002 – ilikuwa Baggies iliyokuwa mbele kwa bao 1-0 kabla ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 2-1.

 Arsenal haijawahi kushindwa kufunga walipocheza dhidi ya West Brom katika mechi 20 za Ligi Kuu timu hizo zilipokutana.

ARSENAL
Baada ya mechi 14 bila ya kufungwa, Arsenal imepoteza mechi zake mbili zilizopita, ambapo the Gunners ilianza kwa kuongoza kwa 1-0 kabla ya kupoteza mechi hizo kwa mabao 2-1.

 The Gunners haijawahi kupoteza mechi tatu mfululizo za Ligi Kuu tangu Januari 2012, ambayo pia ni mara ya mwisho ndio mara yao ya mwisho kupoteza mechi tatu za ligi katika mwezi mmoja.

WEST BROM
 West Brom wenyewe wamepoteza mechi tatu zilizopita za Ligi Kuu.

 Lakini pia waliweza kushinda mechi mbili mwezi huu na hawajawahi kushinda mechi tatu katika mwezi mmoja tangu Novemba mwaka 2012, Waliposhinda mara nne.

Unapoangalia rekodi hizo bila shaka Arsenal ina nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi katika mchezo huo na kutoa zawadi nono ya Boxing Day kwa mashabiki wake.

Friday 23 December 2016

Yanga yasimamishwa na African Lyon yashindwa kurejea kileleni, Simba wenyewe kesho dhidi ya JKT Ruvu



Na Mwandishi Wetu
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga leo wameshindwa kurejea kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo baada ya kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na timu iliyopanda daraja ya African Lyon katika kipute kilichopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Kabla ya mchezo huo wa leo, Yanga ilikuwa na pointi 36 huku watani zao Simba wakiwa pointi 38, mbili zaidi ya wenzao hao na kama Vijana hao wa Jangwani wangeshinda mchezo huo wa leo, basi wangekalia kiti cha uongozi japo kwa muda kabla ya Simba kesho Jumamosi kukutana na JKT Ruvu kwenye Uwanja huohuo wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Endapo Simba itashinda kesho, basi itafikisha jumla ya pointi 41 wakati Yanga wakiwa na pointi zao 37, hivyo watakuwa wamepitwa kwa pointi nne na kuzidi kujiweka katika wakati mgumu wa kutetea taji lao hilo.

Athari za Mgomo?
Wengi wanajiuliza kama kweli matokeo hayo ya sare dhidi ya timu iliyopanda daraja ni athari za mgomo wa wachezaji wa timu hiyo hivi karibuni wakidai fedha zao za mishahara?

Wachezaji wa timu hiyo ndio wanajua siri ya matokeo ya mchezo huo kama ni matokeo halalai au ni moja ya njia za kuushinikiza uongozi wa timu hiyo kuwalipa fedha zao katika kipindi hiki cha Sikukuu za Krismas na Mwaka Mpya.

 
Yana ilishindwa kupata mabao baada ya kocha wao mpya, Mzambia George Lwandamina kuljaza viungo watano, Haruna Niyonzima, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Said Juma na Deus Kaseke akitumia mshambuliaji mmoja tu, Amissi Tambwe.

Yanga walilisakama lango la Lyon kuanzia dakika ya tatu baada ya Tambwe kupiga kichwa vizuri akimalizia krosi ya Msuva, lakini mpira ukaenda juu kidogo na dakika ya 33 Niyonzima akapiga juu ya kuikosesha timu yake bao la wazi.

 Lyon ndio waliokuwa wa kwanza kupata bao la kuongoza lililofungwa na Ludovic Venance aliyefunga katika dakika ya 67 akiunganisha pasi ya Abdallah Mguhi ‘Messi’.
 
Venance aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Mbao FC ya Mwanza, alifunga bao hilo baada kuingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Awadh Juma.

Hata hivyo, bao hilo halikudumu sana, kwani Yanga walifanikiwa kusawazisha dakika ya 74 kupitia kwa mkali wake mabao, Amissi Tambwe akimalizia krosi nzuri ya beki wa kulia Juma Abdul.

Wakati huohuo, ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa Simba kucheza na JKT Ruvu, huku Mbeya City ikiwa mwenyeji wa Toto Africans ya Mwanza, Stand United itacheza na Kagera Sugar, Ndanda FC itakwaana na Mtibwa Sugar, Majimaji dhidi ya Azam FC, Mwadui watakwaana na Mbao  FC wakati Ruvu Shooting wenyewe watacheza Jumatatu dhidi ya Mwadui.

DSTV yawakabidhi Ving'amuzi vya bure na vifurushi vya mwezi mzima washindi 24 wa Kapu la Sikukuu



Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Multichoice Tanzania kupitia king’amuzi chake cha DStv leo imekabidhi ving’amuzi 24 vya kisasa  pamoja na vifurushi vya mwezi mzima kwa washindi wa shindano la ‘Kapu la Sikukuu’ lililoendeshwa kwa ushirikiano na Kituo cha Radio cha EFM.

Washindi hao sasa wataweza kusheherekea kwa mbwembwe Siku Kuu ya Krismas na Mwaka Mpya huku wakiangalia chaneli zaidi ya 70 kupitia king’amuzi hicho cha DStv ikiwemo michezo mbalimbali pamoja na Ligi Kuu ya Hispania ya La Liga, Ligi Kuu ya England,

Pia katika kifurushi hicho walichopata kama zawadi kina chaneli ya Maisha Magic Bongo yenye sinema na tamthilia za Kitanzania ikiwemo ile maarufu kama ya Huba, ambapo wakongwe wa filamu nchini kama akina Muhogo Mchungu, Rihami Ali, Mboto, na Hashim Kambi wanaonekana katika tamthilia hiyo iliyopata umaarufu mkubwa.

Katika hafla hiyo msanii maarufu, Mboto na Irene Paul ndio waliokabidhi zawadi kwa washindi katika hafla hiyo iliyofanyika leo nje ya Kituo cha Radio cha EFM Kawe jijini Dar es Salaam.

Akizungumza kabla ya kukabidhi zawadi hizo kwa washindi Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema aliwapongeza EFM kwa jitihada zao na kuhakikisha wanapata wasikilizaji wengi.

Aidha, Mjema aliwasifu Dstv kwa kutoa zawadi hizo kwa washindi kwani ni kitu muhimu ambacho pia kitawasaidia kuongeza wateja kwa kuwashindanisha na washindi kuwapa zawadi katika bahati nasibu iliyoendeshwa na Kituo cha EFM.

Naye Meneja Masoko wa Multchoice-Tanzania, Alpha Mria alisema kuwa kampuni yao imeamua kuwatunuku washindi hao ving’amuzi na vifurushi vya mwezi mzima vya DStv ili kuwawezesha wao na familia zao kusherehekea vizuri Krismas na Mwaka Mpya majumbani kwao huku wakiangalia DStv.

Mria alisema kuwa Multichoice haijawatunuku washindi pekee yao, bali na Watanzania wengine ambao wanatumia king’amuzi chao kwani hivi karibuni walipunguza bei ya vifurushi zao kwa wastani wa asilimia 16, huku kile kifurushi maarufu zaidi cha DStv Bomba chenye chaneli zaidi ya 70 kikipunguzwa bei hadi kufikia sh. 19,975 tu kwa mwezi.

Baadhi ya washindi waliokabidhiwa zawadi leo ni pamoja na Kelvin Mhenzi, Asha Said, Dasatan Kaligo, Said Ponela, Grace Kimani, Leila Ramadhani, Ashura Bakary, Tamirway Kamote, Baraka Mbogoni, Ratipha Bakari, Gilbert Genese, Luicia John, Ezra Raphael, Nathan William, Caroline Peter, Seleman Dovya, Alice Sangwani, Mbwana Kuwangaya, Peter Doto, Fadhil Doto, Fadhil Yusuph, Hadija Hamisi na Mlani Mohamed.


 
 

Thursday 22 December 2016

Hatimaye Crystal Palace yamtupia virago kocha wao Alan Pardew baada ya kushindwa kuibeba timu



LONDON, England
KLABU ya Crystal Palace imemtupia virago kocha wao,  Alan Pardew huku klabu hiyo ikikamata nafasi ya 17 katika msimamo wa Ligi Kuu ya England.

Pardew aliteuliwa kuifundisha timu hiyo miaka mitatau na nusu iliyopita kuanzia Januari 2015 lakini kocha huyo mwenye umri wa miaka alijikuta akitupiwa virago baada ya timu yake kushinda mchezo mmoja tu kati ya 11.

Palace imeambulia pointi 26 tu kati ya mechi 36 zilizopita za Ligi Kuu ya England na iko pointi moja tu juu ya Ukanda wa Kushuka Daraja.

Kocha wazamani wa timu ya taifa ya England Sam Allardyce ndiye anayepewa nafasi kubwa ya kuchukua mikoba ya kocha huyo.

"Kibinafsi nilikuwa na hisia nzuri kuhusu klabu hii ya soka na nina huzuni kubwa muda wangu pale umemalizika, “alisema Pardew, ambaye aliichezea zaidi ya mechi 100 Palace wakati akiwa mchezaji kati ya mwaka 1987 na 1991 na kuiongoza timu hiyo kucheza fainali ya Kombe la FA msimu uliopita, alisema katika taarifa hiyo.

Mwenyekiti wa klabu hiyo Steve Parish aliongeza: "Wakati wa kipindi chake cha kuifundisha timu hiyo, Alan alifanya kazi kwa bidii na alijitahidi kuiimarisha timu hiyo kwa miaka kadhaa.

Hatahivyo, Palace bado haijathibitisha nani atavaa viatu vya kocha huyo katika mchezo wao wa Ligi Kuu ya Enland utakaofanyika Boxing Day.

Pardew aliondoka Newcastle na kutua  Selhurst Park baada ya Neil Warnock kutimuliwa na Palace baada ya timu hiyo ikiwa katika ukanda wa kushuka daraja.

Uteuzi wake ulikuwa maarufu kwa mashabiki wakati Palace ilifanikiwa kukwepoa kushuka daraja kwa kumaliza katika nafasi ya 10, ikiwa ni nafasi yao bora kabisa kuwa kuipata katika kipindi chao cha kucheza Ligu Kuu ya Englnad.

Ina maana alikuwa kocha wa kwanza kabisa katika Ligi Kuu ya England kumaliza katika nusu ya nafasi ya juu baada ya kuwa katika katika ukanda wa kushuka daraja wakati wa Krismas.