Monday 30 April 2018

Simba Yauota Ubingwa Ligi Kuu Bara


Na Mwandishi Wetu
BAADA ya Simba kufanikiwa kuzoa pointi tatu kwenye mchezo dhidi ya mahasimu wao Yanga, kocha wa timu hiyo, Pierre Lechantre amejinadi kuwa, hakuna anachokisubiri sasa zaidi ya ubingwa.

Simba waliibuka na ushindi wa bao 1-0 na kuwafanya wazidi kujikita kileleni mwa msiamamo wa ligi wakiwa na pointi 62 wakiwaacha Yanga katika nafasi ya pili wakiwa na pointi 48, lakini bado wana mechi mbili zaidi mkononi.

Simba ambao wamebakisha mechi nne wanahitaji pointi tano tu ili watangazwe kuwa mabingwa wa msimu huu kutokana na Yanga ambao wamebakiwa na michezo sita kuwa kama wakishinda mechi zao zote watakuwa wamefikisha pointi 66.

Akizungumza na gazeti hili kocha huyo raia wa Ufaransa alisema kuwa mchezo dhidi ya Yanga ulikuwa ukimnyima raha, kwani alikuwa akiupigia hesabu kali za kutaka kuondoka na pointi tatu.

Alisema alikuwa akiamini wazi kuwa kama atafanikiwa kuwafuinga mahasimu wao hao njia ya ubingwa kwao itakuwa nyeupe kutokana na pengo la pointi lililopo.

“Muda mrefu mlikuwa mkiniuliza kuhusu hii mechi lakini tumeshinda, niliwaambia wachezaji wangu tushindi hii mechi na baada ya kupata alama hizi tatu nina uhakika mkubwa sasa sisi ni mabingwa, tupo vizuri katika mahesabu ,” alisema Lechantre.

Yanga Wamuangushia Jumba Bovu Kessy


Na Mwandishi Wetu
KOCHA msaidizi wa Yanga, Shedrack Nsajigwa ameeleza kuwa kipigo walichokipata juzi Jumapili kutoka kwa mahasimu wao Simba SC kimesababishwa na beki wao Hassan Kessy kutolewa kwa kadi nyekundu.

Kessy alimchezea rafu mbaya Asante Kwasi dakika ya 48 na kulazimika kuoneshwa kadi ya pili ya njano na kuifanya Yanga iliyokuwa kwa bao 1-0 kucheza pungufu mpaka mwisho wa mchezo.

Bao pekee lililoipa ushindi Simba kwenye mchezo huo, lilifungwa na Erasto Nyoni dakika ya 37 akimalizia kwa kichwa mpira wa faulo uliopigwa na Shiza Kichuya.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo kumalizika, Nsajigwa alisema kuwa licha ya kuwa nyuma ya bao hilo moja lakini kabla ya Kessy kutolewa walikuwa wamefanikiwa kuwadhibiti wapinzani wao na walikuwa na uwezo wa kusawazisha bao hilo na kuongeza lingine.

Alisema kuwa walifanya mabadiliko kipindi cha pili kwa kumtoa Raphael Daud na kumuingiza Juma Mahadhi ili kuongeza nguvu safu yao ya ushambuliaji lakini mipango yao hiyo ikafeli.

Aliongeza kuwa licha ya kufungwa lakini mchezo umeshapita hivyo akili zao zote kwa sasa wanazielekeza kwenye michezo yao yote iliyombele yao ikiwemo ile ya michuano ya kimataifa.

“Tulimuingiza Mahadhi ili kumsogeza Yusuph Mhilu juu kuongeza mashambulizi, lakini haikusaidia kutokana na kadi nyekundu, ilikuwa ni kadi ya pili ya njano hivyo ilikuwa lazima kadi nyekundu.

“Kabla ya kadi nyekundu tulikuwa tumebalansi lakini baada ya kutolewa ndio wakatuzidi ila kikubwa sasa tunaangalia m ichezo yetu ijayo,” alisema Nsajigwa.

Hans Pope Aungwanishwa Kesi ya Aveva


Na Mwandishi Wetu
MAHAKAMA ya  Hakimu Mkazi Kisutu, imeamuru Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Klabu ya Simba, Zacharia Hans Pope na mwenzake wakamatwe na kufikishwa mahakamani hapo ili waunganishwe katika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili, Rais wa Klabu  hiyo, Evans Aveva na makamu wake, Godfrey Nyange 'Kaburu'.

Pamoja na Hanspope mahakama hiyo imeamuru  Franklin Lauwo naye akamatwe afikishwe mahakamani hapo.

Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba alitoa amri hiyo jana mara baada ya Mwendesha Mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai kubadili hati ya mashitaka na kuongeza washitakiwa hao.

Wakili Swai alidai kuwa washitakiwa hao wawili wametafutwa na taasisi hiyo tangu mwezi wa tatu bila mafanikio.

Hivyo, aliomba hati ya kuwakamata washitakiwa hao ambao hawakuwepo mahakamani wakati hati ya mashitaka inabadilishwa na kuwaunganisha kuwa miongoni mwa washitakiwa wa utakatishaji fedha na kughushi.

Inadaiwa Machi 15, mwaka jana, jijini Dar es Salaam, washitakiwa Aveva na Nyange wote kwa pamoja walighushi fomu ya kuhamisha fedha kuonesha kwamba Klabu ya Simba inalipa deni la dola za Marekani 300,000 kwa  Aveva, kitu ambacho si kweli.

Katika shitaka la pili linalomkabili Aveva, inadaiwa Machi 15, mwaka jana maeneo ya Benki ya CRDB tawi la Azikiwe wilayani Ilala, Dar es Salaam, alitoa nyaraka hiyo ya uongo kwa benki hiyo kuonesha kuwa klabu hiyo inalipa dola za Marekani 300,000 kwa Aveva.

Pia inadaiwa  tarehe tofauti tofauti kati ya Machi 15 na Juni 29, mwaka jana, ndani ya mkoa huo, washitakiwa walikula njama kutakatisha fedha dola za Marekani 300,000 huku wakijua kwamba fedha hizo ni zao la uhalifu ambalo ni kughushi.

Machi 15 mwaka jana, katika Benki ya Barclays Mikocheni wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, Aveva alijipatia dola za Marekani 300,000 wakati akijua kuwa alipata fedha hizo kutokana na nyaraka za kughushi.

Katika mashitaka ya tano yanayomkabili Nyange, ilidaiwa Machi 15, mwaka jana katika tawi la Barclays tawi la Mikocheni, alimsaidia Aveva kupata fedha kutoka katika benki hiyo, huku akijua kwamba ni zao la uhalifu, ambalo ni kutokana na kughushi fomu ya kuhamishia fedha.

Sunday 29 April 2018

Simba Yainyoosha Yanga Uwanja wa Taifa


Na Mwandishi Wetu
VINARA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba wamezidi kuukaribia ubingwa baada ya leo kuibuka na pointi zote tatu kufuatia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Yanga katika mchezo uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.

Bao hilo pekee lililoifanya Simba kuzidi kuukaribia ubingwa ambao kwa mara ya mwisho waliutwaa katika msimu wa mwaka 2011-12, lilifungwa na Erasto Nyoni katika dakika ya 37 kwa kichwa akiunganisha mpira wa adhabu uliopigwa na Shiza Kichuya na kuparazwa na Rafael Daud na kumkuta mfungaji.

Yanga walijikuta wakicheza pungufu baada ya mchezaji wake Hassan Kessy kutolewa baada ya kupewa kadi ya pili ya njano kutokana na kumchezea vibaya Asante Kwasi katika dakika ya 48.

Pamoja na kucheza pungufu, lakini Simba walishindwa kutumia nafasi hiyo kupata bao jingine na badala yake kila dakika zilipotokomea, waliendelea kucheza kwa kujihami zaidi na kurudi nyuma.

Hatahivyo, Simba ndio walitawala zaidi mchezo huo, ambapo walipata jumla ya kona nane wakati watani zao Yanga hawakupata kona yoyote huku Yanga wakiwa nakadi mbili za njano wakati Simba moja na washindi walipiga mashuti matano yaliyolenga bao wakati Yanga mawili tu.

Kwa ushindi huo, Simba imefikisha pointi 62 na sasa kuhitaji pointi sita tu ili kujihakikishia ubingwa kwani Yanga akishinda mechi zake zote sita zilizobaki atafikisha pointi 66 tu, ambazo zitakuwa zimepitwa na Wekundu wa Msimbazi.

Baada ya kipigo hicho, Yanga wanaendelea kuwa katika nafasi ya tatu wakiwa na pointi zao 48 wakiwa pointi moja nyuma ya Azam FC, ambayo iko katika nafasi ya pili licha ya kucheza mechi 26 wakati Yanga wamecheza jumla ya mechi 24.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Nyoni ambaye alifunga bao hilo pekee alisema kuwa wao wamepania kila mechi kupata pointi tatu na alifanikiwa kufunga bao hilo baada ya mabeki wa Yanga kuwabana wafungaji wa Simba, Emmanuel Okwi, Shiza Kichuya na John Bocco.

Endapo Simba itatwaa ubingwa wa Tanzania Bara, itapata nafasi ya kuliwakilisha taifa katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa wa Afrika msimu ujao.

Kikosi Simba kilikuwa: Aishi Manula, Erasto Nyoni, Nicholas Gyan/ Paul Bukaba, Yusufu Mlipili, James Kotei, Jonasi Mkude, Asante Kwasi, Shomari Kapombe, John Bocco, Emmanuel Okwi na Shiza Kichuya.

Yanga:Youthe Rostand, Hassan Kessy, Gadiel Michael, Andrew Vincent, Kelvin Yondani, Said Makapu, Yusuph Mhilu, Papy Tshishimbi/Emmanuel Martin, Obrey Chirwa, Raphael Daud/ Juma Mahadhi  na Ibrahim Ajibu/ Pius Buswita.

                            MP     W       D        L        GF      GA      +/-    Pts    
 Simba                                      26      18       8        0       59      13       46      62     
 Azam                                        26      13       10      3        25      12       13       49     
 Yanga                                      24      13       9        2        40      14       27      48     
 Prisons                                25      9        11        5        22      18       4        38     
 Singida                                 26      9        11        6        23      24      -1       38     
 Mtibwa                                    25      8        9        8        20      19       1         33     
 Lipuli                                       26      7        11        8        19       20      -1       32     
 Ruvu                                        26      8        8        10      26      33      -7      32     
 Stand                                         26      7        8        11        19       30     -11      29     
 Mbeya City                         26      5        13       8        23      30     -7      28     
 Kagera Sugar              26      5        12       9        17       25      -8      27     
 Mwadui                          25      5        11        9        27      34      -7      26     
 Mbao                              25      5        9        11        23      33      -10     24     
 Majimaji                               26      4        11        11        26      36      -10     23     
 Ndanda                          26      4        11        11        17       28      -11      23     
 Njombe Mji                          26      4        10      12       16       33      -17     22


Asikitishwa Mahudhurio Hafifu Mei Mosi 2018


Baadhi ya wachezaji wa timu ya Uchukuzi wakiwa na vikombe vyao 13 walivyoshinda kwenye mashindano ya Kombe la Mei Mosi yaliyomalizika jana mkoani Iringa. (Picha Zote na Bahati Mollel wa TAA).

Na Bahati Mollel-TAA, Iringa
MWENYEKITI wa Tuico Taifa, Paulo Sangeze amesikitishwa na mahudhurio duni yaliyosababishwa na wanamichezo wafanyakazi kunyimwa fursa kushiriki Michezo ya Mei Mosi mwaka huu iliyofanyika mjini hapa.

Alisema kuwa anaungana na waandaaji kushangaa idadi ndogo ya ushiriki katika mashindano ya mwaka huu.
Katibu Mkuu wa Klabu ya Uchukuzi, Mbura Tenga (kulia) akipokea cheti cha ushiriki wa mashindano ya Mei Mosi yalifanyika  kwenye viwanja mbalimbali mkoani Iringa kutoka kwa mgeni rasmi Mwenyekiti wa TUICO Taifa,  Paul Sangeze.
“Mashirikisho yote ya wafanyakazi tumesikitika kwa idadi hii ndogo na tutahakikisha miaka ijayo timu zinaongezeka zaidi, na tunaipongeza timu ya netiboli ya Ofisi ya Rais Ikulu kushiriki wameonesha mfano mzuri,” amesema Bw. Sangeze.


Pia amesema michezo mahala pa kazi inasaidia kujenga miili ya wafanyakazi na kuongeza tija na bidii kazini, kwani viongozi wasiopenda michezo wanasababisha wafanyakazi kupata magonjwa nyemelezi.

Naye Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Mei Mosi, Bi. Joyce Benjamin alisema Rais John Pombe Magufuli hajawahi kukataza michezo, na inashangaza utashi wa viongozi wasiopenda michezo wanaokataza timu zao kushiriki kwenye michezo.

Mwakilishi wa Gazeti la Uhuru mkoani Iringa, Bi. Ester Malibiche (kulia) akipokea cheti cha ushiriki wa gazeti lake katika michuano ya Kombe la Mei Mosi iliyofanyika kwenye viwanja mbalimbali mkoani Iringa. 
“Tunaomba viongozi wa vyama vya wafanyakazi wa kila eneo la kazi kuingilia kati juu ya hili katika dhana nzima ya wafanyakazi kufanya michezo na kushiriki kwenye michezo ya mashirikisho mbalimbali kama Shimiwi, Shimuuta na kutofanya michezo kunapingana na ilani ya Chama cha Mapinduzi, inayosema wazi juu ya kuinua michezo nchini,” amesema Bi. Benjamin.

Katika mashindano hayo, klabu ya michezo ya Uchukuzi iliyopo (Sekta ya Uchukuzi) imebuka kidedea katika michezo ya michuano ya Kombe la Mei Mosi 2018 baada ya kushinda vikombe 13 vya michezo 10 iliyoshindaniwa kwenye viwanja mbalimbali mjini hapa.
Bi. Sharifa Amir wa Uchukuzi (kulia) akikabidhiwa kombe la ushindi wa kwanza wa mchezo wa draft kwa wanawake kutoka kwa mgeni rasmi Bw. Paul Sangeze ambaye ni Mwenyekiti wa TUICO Taifa. 
Timu hiyo inayoundwa na wachezaji mahiri imeweza kutwaa ubingwa wa kwanza kwa wanaume katika michezo ya mbio za baiskeli (Chaptele Muhumba), draft (Johanson Ngido), bao (Said Omar) na kuvuta kamba, huku kwa wanawake wametwaa ubingwa katika mbio za baiskeli na riadha (Scolastica Hasiri), bao (Sharifa Amir) na draft olnel) na karata wanawake na wanaume (Zamatradi Yusufu na Mosses Machunda).

Timu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) imeshika nafasi ya pili kwa kujikusanyia vikombe tisa kwa kutwa ubingwa wa soka, riadha wanaume (Lazaro Lugano) huku ushindi wa pili katika michezo ya riadha wanawake (Cartace Manampo), na baiskeli (Happy Mwanga), karata (Sheila Mwihava) na Nkwabi Kadago (mwanaume), na ushindi wa tatu netiboli, Stanley Umbe (baiskeli) na Jackline Massawe (bao).

Timu ya Chuo Kikuu cha Tiba ya Sayansi (MUHAS) wamekuwa watatu kwa kujikusanyia vikombe vitano vya bingwa wa karata wanawake (Emily Kyando), ; mshindi wa pili katika bao (Severina Mnyaga), huku mshindi wa tatu michezo ya kuvuta kamba na baiskeli wanawake (Severina Mnyaga) na dratf (Rebecca Chaula).

Timu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wameshika nafasi ya nne kwa kujikusanyia vikombe vinne vya ushindi wa pili katika riadha, baiskeli na bao  wanaume (Michael Luanga),  Nehemiua Johnas na Suleiman Chitanda, huku nafasi ya tatu ya draft ilichukuliwa na Joseph Mlimi.
Nahodha wa timu ya netiboli ya Ofisi ya Rais Ikulu, Bi. Sophia Komba (kulia) akipokea kombe la ubingwa wa mchezo wa netiboli wa michuano ya Kombe la Mei Mosi iliyomalizika jana kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa kutoka kwa mgeni rasmi Bw. Paul Sangeze ambaye ni Mwenyekiti wa TUICO Taifa.
Timu ya Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAOT) wamejikusanyia vikombe vitatu pekee na kuwa watatu. Vikombe vya ushindi wa pili draft wanawake na wanaume Rosemary Skainde na Alphonce Sika na ushindi wa tatu wa kamba wanaume; nazo timu za Ofisi ya Rais Ikulu, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Geita Gold Mine (GGM) kila mmoja wamejikusanyia vikombe viwili, nazo timu za RAS Iringa na Tumbaku ya Morogoro wote wamepata kikombe kimoja-kimoja.
Nahodha wa mabingwa wapya wa soka wa michuano ya Kombe la Mei Mosi timu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Stanley Uhagile akikabidhiwa kombe na mgeni rasmi Mwenyekiti wa TUICO Taifa, Bw. Paul Sangeze. Mabingwa wa zamani Geita Gold Mine (GGM) wameibuka washindi wa tatu. 


Wakenya Waendelea Kutamba Heart Marathon 2018


Na Mwandishi Wetu
BINGWA wa Ngorongoro Race, Mkenya Joseph Mbatha aliifanya kweli baada ya kushinda tena mbio za Heart Marathon zilizofanyika jijini Dar es Salaam na kutwaa Sh milioni 2 leo.

Ngorongoro Race zilifanyika mkoani Arusha Aprili 21 na Mbatha alishinda mbio hizo na kuondoka na Sh milioni 1 baada ya kutumia saa 1:04:54.12 kabla ya kushinda tena jana Heart Marathon kilometa 21 kwa kutumia saa 1:07.01.

Ushindi huo mbali na kufanya Wakenya kuendelea katika mbio za Tanzania, pia unamfanya mwanariadha huyo kuondoka na Sh milioni 3 ndani ya wiki moja tu na huenda akawepo katika Tulia Marathon itakayofanyika Mbeya Mei 6 mwaka huu.

Katika Heart Marathon, mshindi wa pili katika kilometa 21 kwa wanaume, alikuwa Gabriel Gerald wa Arusha aliyemaliza kwa kutumia saa 1:07:02 wakati Mkenya mwingine George Owaiyaki alimaliza watatu kwa kutumia saa 1:07:11 huku Joel Kimutae wa Kenya alimaliza wanne kwa saa 1:07.18.

Kwa upande wa wanawake katika mbio za kilometa 21, Faith Kipsum wa Kenya alimaliza wa kwanza kwa kutumia saa 1:15:17 wakati wa pili alikuwa mwanariadha wa Arusha, Sarah Rawiadhau aliyetumia saa  1:16.10 huku Betrice Chelop wa Kenya alimaliza wa tatu kwa kutumia saa 1:17.33 na Failuna Abdi alimaliza katika nafasi ya nne kwa kutumia saa 1:17.33.

Katika mbio za kilometa 10 kwa wanawake, mwanariadha mkongwe wa Tanzania, Mary Naali alializa wa kwanza kwa kutumia dakika 35:11.17 huku Fabiola William wa Singida alimaliza wa pili kwa kutumia dakika 36:35.39 wakati Neema Paulo wa Arusha pia alimaliza wanne kwa dakika 38:12.37.

Mbio hizo ziliingia dosari baada ya baadhi ya wanariadha kukimbia bila namba licha ya kusajiliwa na kulipa kiingilio na kuleta changamoto kwa waandaaji na wasimamizi.

Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday alisema kabla ya kutolewa kwa zawadi kuwa mbio hizo zimekumbwa na changamoto kadhaa, ambazo zinatakiwa kurekebishwa mwakani ili ziendelee kuwa kubwa.

Pia alitaka wanariadha wa Tanzania kutowaogopa Wakenya licha ya kuja na kushiriki mbio nchini na kuondoka na zawadi za washindi, ambapo aliwataka wanariadha wa Tanzania kujiandaa vizuri ili kupambana na kuwashindana Wakenya.

Waandaaji waliandaa jumla ya Sh milioni 16 kwa ajili ya zawadi za washindi, ambapo mshindi wa kwanza kwa wanaume na wanawake, kila mmoja aliondoka na kitita cha Sh milioni 2.

Liverpool Kumuongezea Mshahara Mo Salah


LONDON, England
KLABU ya Liverpoo inajiandaa kuongezea mshahara Mo Salah ili kumuwezesha kuendelea kuwepo Anfield, imeelezwa.

Kocha wa Liverpool, yuko tayari kuanza mazungumzo ya kumpatia mchezaji huyo kiasi cha pauni 185,000 (sawa na Sh milioni 582) kwa wiki ili kumaliza maswali kuhusu hatma ya mfungaji huyo wa mabao 43 msimu huu.

Makali ya mabao ya Salah umeishtua Real Madrid na kutaka kumnunua mchezaji huyo wa kimataifa wa Misri, ambaye hashikiki kwa mabao katika Ligi Kuu ya England.
 
Kwa sasa Salah analipwa kiasi cha pauni 90,000 kwa wiki, ambazo ni sawa na zaidi ya Sh milioni  283 ikiwa na maana kuwa Salah mwenye umri wa miaka 25, hayumo katika orodha ya wachezaji wanaolipwa mishahara mikubwa Liverpool licha ya kuelekea kuipeleka timu hiyo katika fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Kocha wa Liverpool anataka kukwepa majina makubwa mengine kuondoka katika klabu hiyo kama ilivyokuwa kwa Luis Suarez na Philippe Coutinho ambao walihamia Barcelona.

Liverpool wanaweza kupata mara nne zaidi ya kiasi cha pauni milioni 34.3 walicholipa Roma katika kipindi kilichopita cha majira ya joto wakati Liverpool ilipokuwa ikimnunua mchezaji huyo.

Lakini Liverpool wanataka kumbakisha mchezaji huyo wa kimataifa wa Misri na kuongeza miaka minne aliyoibakisha katika mkataba wake.

Mkataba mpya wa Salah unatarajia kufanyika kabla ya kuanza kwa Kombe la Dunia wakati thamani yake inaweza kuongezeka zaidi.


Ikulu Mabingwa Natiboli, GGM Watatu Katika Soka


Kocha mchezaji Judith Ilunda (mwenye mpira) wa Uchukuzi akizuiwa na mlinzi Lilian Selidion wa Ikulu katika mchezo wa netiboli wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu cha Katoliki Iringa (RUCU). Ikulu walishinda magoli 32-20. (Picha Zote na Bahati Mollel wa TAA).


 Na Bahati Mollel-TAA, Iringa
WAKATI timu ya Ikulu ikitetea ubingwa wake wa netiboli kwa kuifunga Uchukuzi katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Katoliki (RUCU), nayo timu ya Geita Gold Mine (GGM) imeambulia nafasi ya tatu katika mchezo wa soka wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa.

Ikulu ambao wanawatumia wachezaji warefu na wepesi wakiongozwa na kocha wao mzoefu Mary Protas waliwafunga Uchukuzi kwa taabu iliyoongozwa na kocha wake mchezaji Judith Ilunda kwa magoli 31-20. Washindi wakimtegemea mfungaji wake Fatuma Machenga aliyefunga magoli 31 walikwenda mapumziko wakiwa mbele kwa magoli 17-9.

 Mshambuliaji Issack Hassan (17) wa Uchukuzi akijitahidi kujinasua kutoka miguuni mwa mlinzi Enock Magole wa Geita Gold Mine (GGM) katika mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye Uwanja wa Samora mjini  Iringa. GGM walishinda kwa penalti 6-5. 


Magoli ya Uchukuzi yalifungwa na mchezaji mkongwe Matalena Mhagama magoli 13 na Bahati Herman magoli saba. Uchukuzi imetwaa kombe la ushindi wa pili kwa matokeo hayo.

Katika mchezo soka wa kutafuta mshindi wa tatu timu ya GGM iliyovuliwa ubingwa na Tumbaku, sasa imeambulia nafasi ya tatu kwa kuwashinda Uchukuzi kwa mbinde baada ya kupigiana penati 6-5, baada ya kumaliza dakika 90 za kawaida bila kufungana.

Mchezaji Bahati Herman (mwenye mpira) wa Uchukuzi akijiandaa kumrushia mpira Mary Kajigili (wa kwanza kushoto) katika mchezo wa netiboli wa dhidi ya Ikulu wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye uwanja wa Chuo Kikuu cha Katoliki Iringa (RUCU). Ikulu walishinda kwa magoli 32-20. 

Timu hizo zilipigiana penati tisa kila mmoja, lakini GGM walikosa tatu na Uchukuzi walikosa nne, ambapo waliofunga penalti za GGM ni Mohamed Salum, Oswald Binamungu, Yusufu Paul, Amos Mrutu, Enock Magole na kipa  Emmanuel Sangra, huku waliokosa kwa kupaisha na nyingine kudakwa na kipa ni pamoja na Ferdinand Makaranga, Jonathan Mhagama na Yassin Abdallah.


Kocha Mkuu wa timu ya Uchukuzi, Mputa Zenno alisema wameshindwa kufanya vyema kwenye michuano hiyo kutokana na kuwa na majeruhi wengi.

“Tumekuwa na majeruhi wengi kutokana na wachezaji wetu wengi wamekuwa wakifanya mazoezi baada ya kusikia mashindano fulani, jambo ambalo linasababisha kutokua fiti kwa muda mrefu, hivyo natoa wito waendelee na mazoezi hata kama mashindano yameisha,” alisema Mputa.

Mfungaji Regina Runyoro (GS mwenye mpira) wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) akitafuta mbinu ya kumtoka mlinzi Imelda Hango (GK) wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) katika mchezo wa Kombe la Mei Mosi.

Naye Kocha Mkuu wa GGM, Mikidadi Mbaruku alisema mchezo wa mshindi wa tatu ulikuwa mzuri na mashindano kwa ujumla hayakuwa mazuri kutokana na kushirikisha timu chache, ambazo hazikutoa ushindani mkubwa.


Kwa upande wa Uchukuzi waliopata ni pamoja na David Kunambi, Ramadhani Madebe, Karim Sabu, Seleman Kaitaba na Abubakar Hamis, huku waliokosa kwa kupaisha juu na kipa kudaka ni Erick Mpunga, Issack Ibrahim, Ally Poloto na Said Chembela.
Daktari Hawa Senkoro (mwenye miwani) wa Uchukuzi akimchua misuli mchezaji wake Mahamood Hamis aliyebanwa na misuli wakati wa mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu dhidi ya mabingwa wa zamani timu ya Geita Gold Mine (GGM) ya michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa. GGM wametwaa nafasi ya tatu kwa ushindi wa penati 6-5.
Kiungo Salim Kibwana (wa pili kushoto) wa Geita Gold Mine (GGM) akijaribu kuondoa mpira katikati ya Ramadhani Madebe (kushoto) na Abubakar Hamis (wa pili kulia) wa Uchukuzi katika mchezo wa mshindi wa tatu wa Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo  kwenye uwanja wa Samora. GGM walishinda penati 6-5.
Katika mchezo wa kuvuta kamba kwa wanaume, timu ya Uchukuzi ilitwaa ubingwa baada ya kuwavuta Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kwa mivuto 2-0 katika mchezo uliofanyika kwenye viwanja vya Chuo Kikuu cha Katoliki (RUCU). Nayo Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) walivutana na Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) na kushinda mivuto 2-0
.

Saturday 28 April 2018

Kuziona Simba, Yanga Zikiumana ni Buku Saba Tu


Na Mwandishi Wetu
KESHO jiji la Dar es Salaam na viunga vyake litazizima kufuatia mpambano wa watani wa jadi Simba na Yanga utakochezwa Uwanja wa Taifa, huku kingilio cha juu zaidi katika mchezo huo ni Sh 30,000 wakati cha chini ni 7,000, imeelezwa.

Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara aliwambia waandishi wa habari jana kuwa tiketi za mchezo huo zinapatikana Celcom pamoja na mawakala kituo cha mafuta cha Total kilichopo Uhuru pamoja na Uwanja wa taifa.

Alitaja viingilio katika mchezo huo kuwa ni Sh 30,000 kwa VIP A, wakati VIP B ni Sh 20,000 huku mzunguko ikiwa ni Sh 7,000.

Akizungumzia mchezo huo Manara alisema: "Mchezo utakuwa mgumu, Yanga ni wakubwa wenzetu, tunawaheshimu, "alisema.

"Mashabiki wanataka ubingwa, matokeo ya mechi yetu na Yanga ndio yatakayotoa mustakabali wa ubingwa wetu, alisema  na kuongeza:

"Wachezaji wanajua nini tunataka, siwezi kusema lazima tushinde, mpira una matokeo matatu, kufunga, kufungwa na kutoka sare, mechi ndio itatoa mwelekeo wa ubingwa,"alisisitiza.

Simba na Yanga watashuka katika mechi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara, katika mchezo wa marudiano utakaopingwa  kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ambapo katika mchezo wa kwanza timu hizo zilifungana 1-1.

Simba itashuka dimbani huku ikiwa inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi Simba inaongoza msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 58 baada ya kucheza michezo 24 huku Yanga ikiwa inaifukuza kwa nyuma kwa pointi 47 akiwa na amecheza mechi 23.

Friday 27 April 2018

Bill Cosby Atupwa Jela Miaka 10


NEW YORK, Marekani
MCHEKESHAJI mahiri wa Marekani Bill Cosby (pichani) amehukumiwa kwenda jela zaidi ya miaka 10 baad aya kupatikana na hatia ya kumdhalilisha kijinsia mwanamke mmoja, Andrea Constand zaidi ya muongo mmoja uliopita.

Msanii huyoi wa vichekesho alikutwa na hatia katika makosa matatu, ambapo sasa mashabiki wake, ambao walifurahia vichekesho `live’ kwa zaidi ya miongo minne, na sasa wataona skrini za sinema.

Cosby alikuwa pia akituhumiwa na zaidi ya wanawake wengine 50 kwa kuwanyanyasa kijinsia, lakini hawakumpeleka mahakamani na kuonekana hana hatia katika madai hayo.

Muigizaji huyo, mwenye umri wa miaka 80 sasa, alikuwa akituhumiwa kumnyanyasa kinjinsia mchezaji wazamani wa mpira wa kikapy Andrea Constand mwaka 2004.

Cosby,ambaye ni muigizaji wa kwanza mkubwa wa Kiafrika katika TV, ataendelea kuwa nje hadi pale hukumu yake itakavyothibitishwa.

Hatahivyo, wakili wake alisema kuwa atakata rufaa kupinga hukumu hiyo dhidi ya mteja wake.

Hii ilikuwa mara ya pili kwa muigizaji huyo kusimama mahakamani kwa shtaka kama hilo, lakini hakupatikana na hatia Juni mwaka 2017.

Cosby anajulikana sana kwa maonesho katika TV katika miaka ya 1980 iliyojulikana kama Cosby Show.

Mwanasheria wa Cosby, Tom Mesereau alisisitiza kuwa “mpambano bado unaendelea”, akiongeza kuwa anaamini Cosby hana hatia na ana mpango wa kukata rufaa.

GGM Wavuliwa Ubingwa, Wakata Rufaa Mei Mosi

Beki wa Uchukuzi Erick Mpunga (jezi ya bluu) akitoa hatari langoni mwake huku mshambuliaji Kurwa Makaranga wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) akijaribu kutibua katika mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa. Tanesco wametinga fainali kwa magoli 2-1.(Picha na Bahati Mollel wa TAA).
Na Bahati Mollel-TAA, Iringa
TIMU inayoundwa na wachezaji chipukizi ya Tumbaku ya Morogoro leo iliwavua ubingwa wa michuano ya Kombe la Mei Mosi timu ya Geita Gold Mine (GGM) na kutinga hatua ya fainali baada ya kuwafunga magoli 4-1 katika mchezo wa kwanza wa nusu fainali uliofanyika kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa.

Tumbaku ambayo haijapoteza mchezo tangu ilipoanza hatua ya makundi ikiwa kundi ‘A’ na GGM ikiwa kundi ‘B’ ilianza kupata bao lake la kwanza kupitia kwa mshambuliaji wake Kelvin Makamba aliyepiga shuti kali nje ya 18 katika dakika ya pili.

GGM walisawazisha katika dakika ya 44 kwa kichwa kilichopigwa na Oswald Binamungu baada ya kupata pasi ya Ferdinand Makaranga.

Tumbaku waliongeza bao la pili katika dakika ya 51 kupitia kwa mshambuliaji wake Issa Simbaliane aliyepiga mpira wa faulu uliokwenda moja kwa moja golini, huku bao la tatu lilipachikwa kimiani katika dakika ya 62 baada ya Emmanuel Mwakibinga kuunganisha kwa kichwa kona iliyochongwa na Idd Likasi.

Kiungo Idrisa Magongo alifunga kitabu cha magoli katika dakika ya 79 kwa kufunga bao la nne.
Kiungo wa Uchukuzi Suleiman Kaitaba (kushoto) akimpiga chenga Joseph Mzee wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) katika mchezo wa nusu fainali wa Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa. Tanesco waliibuka washindi kwa magoli 2-1. (Picha na Bahati Mollel wa TAA).
Hatahivyo, Katibu mkuu wa timu ya GGM, Wilhemin Bayanga pamoja na kukiri mchezo ulikuwa mkali na mzuri lakini wameikatia rufaa timu nzima ya Tumbaku kwa madai wamechezesha mamluki.

Katika mchezo mwingine wa nusu fainali timu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) imeingia fainali baada ya kuifunga timu ngumu ya Uchukuzi kwa magoli 2-1. Uchukuzi ndio walikuwa wa kwanza kupachika bao katika dakika ya 67 kupitia kwa Omary Kitambo.

Tanesco walisawazisha kwa njia ya penalti iliyotolewa na mwamuzi Winfred Fyataga, katika dakika ya 70 na Seleman Ismail baada ya kipa Willy Barton kumchezea madhambi  Gossage Mtumwa. Bao la ushindi la Tanesco lilifungwa na Fortunatus Mgimba katika dakika ya 76 baada ya kipa Barton kuusukumiza mpira wa kona uliochongwa na mfungaji.

Kocha Mkuu wa Tanesco, Fidelis Almas amekiri leo atakuwa na kibarua kipevu kutokana na Tambuku kutokana na wachezaji wake kuwa chipukizi zaidi.

“Ninajua mechi itakuwa kali lakini tumejiandaa kukabiliana na Tumbaku kwani tunawajua kutokana na kuwaona mara kadhaa wakiwa wanacheza na tulikuwa kundi moja,” alisema Almas.

Wakati huo huo, timu ya Uchukuzi imeongeza kikombe baada ya kushinda Mzee Omari Said kuibuka bingwa katika mchezo wa bao uliofanyika kwenye ukumbi wa Manispaa Iringa. Ushindi wa pili ulichukuliwa na Suleiman Chitanda wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Shaaba Kidang’ala wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) aliibuka wa tatu.