Wednesday 11 April 2018

Yanga Yapunguzwa Kasi Mbio za Ubingwa Ligi Kuu


Beki wa Yanga, Hassan Kessy (kushoto) akijaribu kuwatoka wachezaji wa Singida United, Kiggi  Makasi (kulia) na Mudathir Yahya wakati wa mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jana na kumalizika kwa sare ya 1-1.

Na Mwandishi Wetu
MABINGWA wa Ligi Kuu Tanzania Bara Yanga jana walipunguzwa kasi katika mbio za kutetea taji hilo baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na Singida United, katika mchezo wa ligi hiyo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Kwa matokeo hayo, Yanga imefikisha pointi 47 na kuifanya sasa kupitwa na watani zao Simba kwa pointi tano.

Kwa matokeo hayo ni dhahiri kuwa Yanga imeendelea kuwa mnyonge wa Singida kwa kushindwa kuifunga kwa mara ya tatu. Mchezo wa raundi ya kwanza kwenye Uwanja wa Namfua walitoka suluhu, wakati katika Kombe la Shirikisho (FA), walifungana 1-1 kabla ya Yanga kutolewa kwa penalti 4-2.

Sare hiyo inazidi kuisafishia Simba nafasi ya kuwania taji la ligi ikiendelea kubaki kileleni kwa pointi 52 na Yanga ikiendelea kuwa katika nafasi ya pili kwa pointi 47 zikitofautiana pointi tano, huku Singida United ikifikisha pointi 37.

Singida ndio ilikuwa ya kwanza kupata bao la uongozi dakika ya kwanza lililofungwa na Salita Kambale baada ya kupata krosi nzuri ya Kigi Makasi .

Katika mchezo huo, dakika 45 beki Abdallah Shaibu ‘Ninja’ aliisawazishia Yanga kwa kichwa mpira wa kona uliopigwa na Ibrahim Ajibu.

Kipindi cha kwanza kilimalizika Yanga 1-1. Kipindi cha pili Yanga walikuja kwa kushambulia zaidi lakini tayari Singida United walionekana kama wanaitaka sare baada ya kuonekana kuzuia zaidi.

Awali, kipindi cha kwanza Singida ilifanya mabadiliko kwa kuwatoa kipa Mustapha Barthez na kuingia Peter Manyika dakika ya 38. Pia, dakika ya 42 Shafiq Batambuze alitolewa na kuingia Salum Chuku na dakika ya 68 alitoka Nizah Khalifan na kuingia Yusufu Kagoma.

Yanga ilitengeneza nafasi nyingi za kufunga na kushindwa kuzitumia kupitia kwa Yusufu Mhilu, Ajibu na Chirwa kwa vipindi tofauti.

Pia, ilifanya mabadiliko kipindi cha pili kwa kuwatoa Pius Buswita na kuwaingiza Juma Mahadhi dakika ya 73, Ajibu na kuingia Geofrey Mwashiuya dakika 78 lakini haikusaidia chochote kwani hadi mpira unaisha matokeo yaliendelea kubaki sare ya bao 1-1.

Vikosi vilikuwa: Yanga; Youthe Rostand, Hassan Kessy, Haji Mwinyi, Abdallah Shaibu, Kelvin Yondani, Papy Kabamba, Yusufu Mhilu, Pius Buswita, Obrey Chirwa, Raphael Daud na Ibrahim Ajibu.

Singida United; Ally Mustapha, Miraji Adam, Shafik Batambuze, Malik Antir, Kennedy Juma, Mudathir Yahya, Deus Kaseke,Kenny Ally, Kambale Salita, Nizah Khalifan na Kigi Makasi.

No comments:

Post a Comment