Thursday 12 April 2018

Simba Yazidi Kuukaribia Ubingwa Ligi Kuu Bara


Na Mwandishi Wetu
VINARA wa Ligi Kuu soka Tanzania Bara, Simba wanazidu kuukaribia ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bada, baada ya kuifunga Mbeya City kwa mabao 3-1 katika mchezo uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.

Kwa ushindi huo, Simba imefikisha pointi 55 ikifunga mabao 55 katika michezo 23, ikifuatiwa na mahasimu wao, Yanga waliopo katika nafasi ya pili wakiwa na pointi 47 katika michezo 22 na nafasi ya tatu Azam yenye pointi 45 katika michezo 23.

Mabao ya Simba yalifungwa na Emmanuel Okwi, John Bocco na Asante Kwasi, huku lile la kufutia machozi la Mbeya City likiwekwa kimiani na Frank Ikobela.

Simba ilianza kwa kasi mchezo huo na kupata bao la uongozi dakika ya 16 lililofungwa na Okwi, likitokana na shuti la  Bocco lililopanguliwa na kipa wa City, Owen Chaima kuzagaa eneo la hatari.
Dakika 29 Bocco alipata nafasi ya wazi na kushindwa kuitumia baada ya kupiga mpira pembeni ya goli lakini dakika 32 baadaye Kwasi akaifungia Simba bao la pili kwa kichwa akipata krosi ya Shiza Kichuya.

Kabla ya wekundu hao kufunga bao la tatu dakika 35 lilifungwa na Bocco kutokana na krosi ya Shomari Kapombe, tayari City walifunga bao dakika 34 lililotokana na kona iliyochongwa na Danny Joram na kmkuta Ikobelo na kuujaza wavuni kwa kichwa.

Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika, Simba ilikuwa mbele mabao 3-1 wakiongoza kwa kufanya mashambulizi mengi lakini pia, walitumia faida ya wapinzani waliotumia muda mwingi kujilinda.

Kipindi cha pili Simba ilikuja na mbinu za kujihami na kushambulia kiasi  na wapinzani wao walikuja kwa kasi wakitafuta nafasi ya kufunga lakini walishindwa kutumia nafasi kadhaa walizopata. Dakika ya 65 Victor Hangaya nusura afunge kipa wa Simba Manula aliudaka.

Pia, Simba nusura ifunge dakika ya 53 mpira uligonga mwamba na dakika ya 57 Kichuya alipiga shuti kali golini lilipanguliwa na Chaima.

Hadi dakika 90 zinamalizika hakuna aliyeongeza bao na Simba ikiibuka na pointi tatu muhimu.

Michezo mingine iliyochezwa jana, Mtibwa imeshinda bao 1-0 dhidi ya Ndanda huku mchezo wa Ruvu Shooting dhidi ya Azam ukiahirishwa kutokana na mvua kubwa kunyesha Mlandizi.

Vikosi Simba;Aishi Manula, Nicholaus Gyan/James Kotei dk.87, Asante Kwasi/Mohamed Hussein dk. 73, Juuko Murshid, Yusufu Mlipili, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Shomari Kapombe, Emmanuel Okwi, John Bocco/Laudit Mavugo dk. 79 na Shiza Kichuya.

Mbeya City:Owen Chaima, Rajabu Isihaka, Majaliwa Shabani, Ally Lundenga, Ramadhan Malima, Haruna Shamte, Eliud Ambokile, Danny Joram/Danny Joram dk. 60, Victor Hangaya/Godfrey Milla dk. 76, Babu Ally/Hamidu Mohamed dk.43 na Frank Ikobela.

No comments:

Post a Comment