Monday 2 April 2018

Singida United Yaiondoa Yanga Kombe la Shirikisho


Na Mwandishi Wetu
PASAKA imekuwa chungu kwa Yanga baada ya kutupwa nje ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam dhidi ya Singida United kwa kuchapwa mikwaju ya penalti 4-2.

Mechi hiyo iliyopigwa kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida, ilimalizikakwa timu hizo kufungana bao 1-1 katika muda wa kawaida na ndipo ilipoamuliwa ipigwe mikwajua ya penalti na Yanga kulala kwa matokeo hayo.

Papy Tshishimbi na Emanuel Martin ndio waliokosa  penalti hizo kwa upande wa Yanga, huku nahodha Kelvin Yondani na Gadiel Michael wakipata mikwaju yao.

Kipa wa Yanga, Youthe Rostand alipangua mkwaju wa Malik Antil, lakini akashindwa kufanya hivyo kwa mikwaju iliyopigwa na Shafiq Batambuze, Tafadzwa Kutinyu, Kenny Ally na Elinyeswia Sumbi au Msingida.

Katika mchezo huo uliokuwa mgumu kwa timu zote mbili kutokana na kila upande kuwa na uhitaji wa kutinga hatua inayofuata, kipa upande ulitawala katika kila kipindi, Yanga ikitawala kipindi cha kwanza na Singida cha pili.

Yanga ilikuwa ya kwanza kupata bao la kuongoza katika dakika ya 23 bao lililofungwa kwa kichwa na winga Yusuph Mhilu baada ya kutumia kona safi iliyopigwa na Ibrahim Ajib.

Hali ya uwanja kujaa maji ilisababisha timu zote kucheza mpira wa pasi ndefu ambazo  hata hivyo haikuwa na faida kwa timu zote mbili ingawa kwa Singida ilionekana kuwanufaisha kwa mipira ya kona ambazo hata hivyo hazikuwa na faida kwao.

Bao la Yanga lilidumu mpaka mapumziko na Singida ilisawazisha dakika ya kwanza ya kipindi cha pili  kupitia kwa  kiungo Kenny Ally baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Kigi Makasi.

Baada ya hapo Yanga ilionekana kutulia na kutafuta bao ambalo lingeweza kuwavusha katika hatua nyingine hata hivyo pamoja na kufanya mabadiliko kadhaa hawakufanikiwa na kadri muda ulivyokuwa ukienda Singida walionekana kuimarika zaidi na kujipanga kuongeza bao.

Singida ilitaka kudhihirisha uimara wake kufuatia mashambulizi mfululizo waliyokuwa wakifanya langoni mwa Yanga,ingawa umahiri wa  Yondani na Andre Vincent uliwapa faida Yanga baada ya kutulia dakika zote 90.

Dakika ya 78 Yanga ilianza kutulia tena baada ya kufanikiwa kudhibiti mashambulizi wa wapinzani wao ambapo dakika tano baadaye Juma Abdul alitolewa na nafasi yake kuchukuliwa Hassan Kessy, hata hivyo bado ngoma ilikuwa ngumu mpaka dakika 90.

Kwa matokeo hayo Singida itacheza hatua ya nusu fainali na JKT Tanzania wakati Stand United iliyoitoa Njombe FC itaumana na Mtibwa Sugar iliyoitoa Azam, katika nusu fainali nyingine.

No comments:

Post a Comment