Friday 27 April 2018

Uchukuzi Yazoa Vikombe Saba Mei Mosi 2018


Wanariadha Scolastica Hasiri na Colnel Kufahaidhuru (wote wananamba 5 kifuani), wakishangilia na baadhi ya wachezaji wa michezo mbalimbali wa timu yao ya Uchukuzi, baada ya kushinda ushindi wa kwanza kwa wanawake na wa tatu kwa wanaume katika michuano ya Kombe la Mei Mosi iliyofanyika leo kwenye uwanja wa Samora mkoani Iringa. (Picha Zote na Bahati Mollel wa TAA).



Na Bahati Mollel-TAA, Iringa
TIMU ya Uchukuzi leo ilijizolea vikombe saba baada ya wachezaji wake kuibuka mabingwa na washindi wa tatu katika michuano ya Kombe la Mei Mosi kwenye michezo ya riadha, karata, bao na draft iliyofanyika kwenye uwanja wa Samora na ukumbi wa Manispaa Iringa.

Nyota njema ilianza kuonekana alfajiri kwa Uchukuzi baada ya wanariadha wake Scolastica Hasiri kushinda mbio za kilometa nane kwa wanawake baada ya kutumia dakika 46:16 huku Colnel Kufahaidhuru ameshika nafasi ya tatu kwa wanaume baada ya kutumia dakika 44:01 zikiwa ni mbio za kilometa 10.
Mwajuma Kisengo (wa kwanza kushoto) akiwa na waamuzi wenzake wakati wa mchezo wa riadha wa michuano ya Kombe la Mei Mosi wa kilometa nane wanawake na 10 wanaume uliofanyika leo  kwenye uwanja wa Samora. (Picha na Bahati Mollel wa TAA).

Ushindi wa pili wa riadha kwa wanawake umechukuliwa na Cartace Manampo wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kwa kutumia dakika 46:50 na mshindi wa tatu ni Sophia Komba wa Ofisi ya Rais Ikulu amtumia dakika 51:46.

Kwa upande wa wanaume katika mchezo wa riadha bingwa ni Lazaro Lugano Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ametumia dakika 42:28, huku mshindi wa pili ni Michael Luanga wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) alitumia dakika 43:20.
Wachezaji wa timu mbalimbali zinazoshiriki kwenye michuano ya Kombe la Mei Mosi inayoendelea kwenye viwanja mbalimbali mkoani Iringa wakimshangilia Shaaban Kidang’ala (aliyevaa jezi nyeupe) wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) baada ya leo kuwa wa mwisho katika mbio za kilometa 10 wanaume kwa kutumia dakika 57:46.


Nafasi ya nne imekwenda kwa Francis Sweetbert wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) kwa muda dakika 45:18, huku wa tano ni Hakim Ambari wa Ofisi ya Rais Ikulu alitumia dakika 47:10 na wa mwisho ni Shaaban Kidang’ala wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) alitumia dakika 57:46.

Katika mchezo wa draft wanawake Neema Makassy wa Uchukuzi ameibuka bingwa baada ya kujikusanyia pointi 10, akifuatiwa na Rosemary Skainda wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) mwenye pointi sita; naye Rebecca Chaula wa MUHAS amekuwa mshindi wa tatu kwa kujikusanyia pointi nne.

Mchezaji Neema Makassy wa Uchukuzi (kulia) akichuana na Rebecca Chaule wa MUHAS katika mchezo wa draft kwa wanawake wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye ukumbi wa Manispaa Iringa. (Picha na Bahati Mollel wa TAA) .


Kwa upande wa wanaume mchezo wa draft mchezaji Johnson Ngido wa Uchukuzi ameibuka bingwa, akifuatiwa na Alphonce Sika wa Ofisi ys Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) na mshindi wa tatu ni Joseph Mlimi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Katika mchezo wa karata wanaume ubingwa umechukuliwa na mchezaji Wilhemin Bayanga wa Geita Gold Mine (GGM), huku mshindi wa pili ni Nkwabi Kagado wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na wa tatu ni Moses Machunda wa Uchukuzi. Kwa upande wa wanawake Emily Kyando wa MUHAS ameibuka mshindi, akifuatiwa na Sheila Mwihava wa Tanesco na Zamaradi Yussuf wa Uchukuzi akiwa tatu.
Anna Msulwa wa Ofisi ya Rais Ikulu (kulia) akitafakari jinsi ya kumshinda Zamaradi Yussuf wa Uchukuzi katika mchezo wa karata wanawake wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye ukumbi wa Manispaa Iringa. Zamaradi ameibuka mshindi wa tatu. (Picha na Bahati Mollel wa TAA).
Katika mchezo wa bao wanawake Sharifa Amir, wa pili ni Jacky Massawe wa Tanesco na watatu ni Severina wa MUHAS.

Michuano hiyo inaendelea leo kwa timu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuumana na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) katika mchezo wa netiboli, wakati katika kamba wanaume Uchukuzi watavuta na Tanesco; huku NCAA watacheza na NAO.

Mchezaji Alphonce Sika wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) (kulia) akiusoma mchezo wa fainali wa draft kwa wanaume dhidi ya Johnson Ngido wa Uchukuzi katika michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa Manispaa ya Iringa. Ngido ameibuka bingwa. (Picha na Bahati Mollel wa TAA).

Mchezaji Sharifa Amir (wa kwanza kulia) akichuana na Jacky Massawe wa Tanesco katika mchezo wa fainali wa bao kwa wanawake wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa Manispaa ya Iringa. Sharifa ameibuka bingwa. (Picha na Bahati Mollel wa TAA).  




No comments:

Post a Comment