Thursday 26 April 2018

Simba Watangulia Kuwakabili Watani Yanga


Na Mwandishi Wetu
SIMBA SC tayari wapo mjini Dares Salaam tangu jana mchana kwa maandalizi ya mwisho ya pambano dhidi ya mahasimu wao, Yanga litakalofanyika Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Jijini Dar es Salaam.

Baada ya mazoezi yao asubuhi tu Uwanja wa Highland, Morogoro, wachezaji wa Simba na benchi lao zima la ufundi wakapanda basi lao kurejea Dar es Salaam ambako wamefikia katika hoteli ya SeaScape, eneo la Mbezi Beach, pembezoni mwa Bahari ya Hindi.

Simba ilikuwa Morogoro tangu Jumapili kwa kambi ya maandalizi ya mchezo wao ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya mahasimu wao, Yanga keshokutwa Jumapili,

Wekundu hao wa Msimbazi waliwasili Morogoro wakitokea Iringa, ambako Jumamosi walitoka sare ya kufungana bao 1-1 na wenyeji wao, Lipuli katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora.

Watani wao, Yanga nao wapo Morogoro tangu Jumatatu, siku moja tu baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na wenyeji wao, Mbeya City katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliofanyika kwenye Uwanja wa Sokoine.

Matarajio ni Yanga, ambao ndiyo mabingwa watetezi wa Ligi Kuu kuingia Dar es Salaam mapema kesho tayari kwa mchezo huo wa Jumapili.

Jumapili inatarajiwa kuwa siku kubwa mno katika soka ya Tanzania, miamba hiyo ya soka nchini ikimenyana vikali katika mbio za kuwania ubingwa.

Simba SC iliyo chini ya kocha Mfaransa, Pierre Lechantre anayesaidiwa na Mtunisia, Aymen Mohamed Hbibi, Mrundi, Masoud Juma na mzawa Muharami Mohamed ‘Shilton’, inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 59 baada ya kucheza mechi 25, wakati Yanga inafuatia kwa mbali kidogo ikiwa na pointi zake 48 baada ya kucheza mechi 23.

Yanga inazidiwa pointi 11 na Simba SC na ina viporo viwili, maana yake ili kutetea ubingwa wao, itabidi washinde Jumapili na washinde mechi zao zote zilizobaki za Ligi Kuu, huku wakiwaombea mahasimu wao hao wapoteze mechi nyingine, jambo ambalo ni gumu.

No comments:

Post a Comment