Monday 9 April 2018

Kocha Azam FC Akata Tamaa ya Ubingwa Bara


Na Mwandishi Wetu
SARE ya bila kufungana dhidi ya Mbeya City imemkatisha tamaa kocha msaidizi wa Azam FC,  Idd Nasoro ‘Cheche’ na kusema nivyema wakajipanga upya kwa ajili ya msimu ujao.

Sare hiyo imeifanya Azam kubaki nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu wakiwa na pointi zao 43, katika michezo 23, huku Simba na Yanga zikichuana kwenye mbio za ubingwa wa Tanzania Bara msimu huu.

Akizungumza na gazeti hili, Cheche, alisema sare ya juzi dhidi ya Mbeya City imevuruga kabisa malengo yao ya ubingwa na kwa mtazamo wake nivyema wakajipanga upya kwa kusajili wachezaji wenye uzoefu ambao wataweza kutimiza malengo ya timu.

“Sisemi kwamba wachezaji waliopo hawana uwezo bali tunahitaji kuongeza baadhi kutoka ndani na nje ili kuimarisha zaidi kikosi chetu kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma,” alisema Cheche.

Kocha huyo alisema kitu kikubwa ambacho kinawakwamisha msimu huu ni baadhi ya wachezaji wao wakutumainiwa kuwa majeruhi huku waliobaki wakiwa hawana zoefu wa kutosha kwa ajili ya mapambano ya ndani ya uwanja.

Azam imebakiwa na michezo saba kabla ya kumaliza msimu huu na matarajio yao hivi sasa ni kuhakikisha wanamaliza kwa heshima ligi hiyo kama ilivyokuwa misimu minne nyuma.

No comments:

Post a Comment