Sunday 29 April 2018

Wakenya Waendelea Kutamba Heart Marathon 2018


Na Mwandishi Wetu
BINGWA wa Ngorongoro Race, Mkenya Joseph Mbatha aliifanya kweli baada ya kushinda tena mbio za Heart Marathon zilizofanyika jijini Dar es Salaam na kutwaa Sh milioni 2 leo.

Ngorongoro Race zilifanyika mkoani Arusha Aprili 21 na Mbatha alishinda mbio hizo na kuondoka na Sh milioni 1 baada ya kutumia saa 1:04:54.12 kabla ya kushinda tena jana Heart Marathon kilometa 21 kwa kutumia saa 1:07.01.

Ushindi huo mbali na kufanya Wakenya kuendelea katika mbio za Tanzania, pia unamfanya mwanariadha huyo kuondoka na Sh milioni 3 ndani ya wiki moja tu na huenda akawepo katika Tulia Marathon itakayofanyika Mbeya Mei 6 mwaka huu.

Katika Heart Marathon, mshindi wa pili katika kilometa 21 kwa wanaume, alikuwa Gabriel Gerald wa Arusha aliyemaliza kwa kutumia saa 1:07:02 wakati Mkenya mwingine George Owaiyaki alimaliza watatu kwa kutumia saa 1:07:11 huku Joel Kimutae wa Kenya alimaliza wanne kwa saa 1:07.18.

Kwa upande wa wanawake katika mbio za kilometa 21, Faith Kipsum wa Kenya alimaliza wa kwanza kwa kutumia saa 1:15:17 wakati wa pili alikuwa mwanariadha wa Arusha, Sarah Rawiadhau aliyetumia saa  1:16.10 huku Betrice Chelop wa Kenya alimaliza wa tatu kwa kutumia saa 1:17.33 na Failuna Abdi alimaliza katika nafasi ya nne kwa kutumia saa 1:17.33.

Katika mbio za kilometa 10 kwa wanawake, mwanariadha mkongwe wa Tanzania, Mary Naali alializa wa kwanza kwa kutumia dakika 35:11.17 huku Fabiola William wa Singida alimaliza wa pili kwa kutumia dakika 36:35.39 wakati Neema Paulo wa Arusha pia alimaliza wanne kwa dakika 38:12.37.

Mbio hizo ziliingia dosari baada ya baadhi ya wanariadha kukimbia bila namba licha ya kusajiliwa na kulipa kiingilio na kuleta changamoto kwa waandaaji na wasimamizi.

Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday alisema kabla ya kutolewa kwa zawadi kuwa mbio hizo zimekumbwa na changamoto kadhaa, ambazo zinatakiwa kurekebishwa mwakani ili ziendelee kuwa kubwa.

Pia alitaka wanariadha wa Tanzania kutowaogopa Wakenya licha ya kuja na kushiriki mbio nchini na kuondoka na zawadi za washindi, ambapo aliwataka wanariadha wa Tanzania kujiandaa vizuri ili kupambana na kuwashindana Wakenya.

Waandaaji waliandaa jumla ya Sh milioni 16 kwa ajili ya zawadi za washindi, ambapo mshindi wa kwanza kwa wanaume na wanawake, kila mmoja aliondoka na kitita cha Sh milioni 2.

No comments:

Post a Comment