Saturday 27 January 2018

Yanga Yaichapa Azam Kwenye Uwanja waoi

Na Mwandishi Wetu
YANGA imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC ugenini katika mchezo wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara uliochezwa leo kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi.

Hatahivyo, ushindi huo wa Yanga umeendelea kuibakiza timu hiyo katika nafasi ya tatu nyuma ya Simba na Azam baada ya kujikusanyia pointi 28.

Washindi walishuka dimbani huku wakicheza bila ya wachezaji wake karibu saba, ambao ni majeruhi, lakini walicheza kandanda safi.

Aidha, mchezaji wa Azam FC Abubakari Salum ‘Sure Boy’ alitolewa kwa kadi nyekundu baada ya kumsukuma kwa makusudi, Hassan Kessy mbele ya mwamuzi wa kati Israel Nkongo.

Azam ndio ilikuwa ya kwanza kupata bao katika dakika ya tatu baada ya kuanza kwa mchezo huo likifungwa na Shaban Chilunda, huku Obrey Chirwa akisawazisha dakika ya 30 na la ushindi likifungwa na Gadiel Michael.

Ushindi huo umeendelea kuibakiza  Yanga katika nafasi ya tatu kwenye msimamo ikifikisha jumla ya pointi 28, nyuma ya Azam yenye pointi 30 na Simba 32.

Azam FC ilianza mpira kwa kasi na kufanikiwa kupata bao hilo la uongozi baada ya Chilunda kutengenezewa pasi na Bruce Kangawa.

Baada ya Azam kuongoza bao hilo walianza kupunguza kasi na kuwapa nafasi wapinzani wao kusawazisha kupitia kwa Chirwa aliyepata pasi ya Ibrahim Ajibu ambapo alimzunguka kipa Razaki Abalora na kufunga.

Azam baada ya kusawazishiwa walirudi tena kwenye kasi na kufanya mashambulizi mengi lakini hayakuzaa matunda, na kutoa nafasi zaidi kwa Yanga kujiamini ambapo Gadiel alipiga shuti kali nje ya 18 na kuifungia Yanga bao la pili.

Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika Azam ilikuwa ikiongoza kwa mashambulizi lakini Yanga ilikuwa mbele kwa mabao 2-1.

Kipindi cha pili Azam iliendeleza kasi ya mashabulizi bila mafanikio kwani  tayari Yanga iliweka ukuta na kupata wakati mgumu wa kufunga. Hadi mpira unakwisha matokeo hayo
Kocha wa Azam alijaribu kufanya mabadiliko kadhaa lakini hayakuzaa matunda. Dakika 36 alimtoa Bernard Arthur na kumuingiza Salmin Hoza, pia, kipindi cha pili dakika 55 na 65 alimtoa Stephen Kingue na Shaban Chilunda na kuingia Mbaraka Yusufu na Paul Peter.

Kwa upande wa Yanga dakika ya 66 iliwatoa Emmanuel Martin na kuingia Geofrey Mwashiuya, pia, dakika 68 alimtoa Ibrahim Ajibu na kuingia Juma Mahadhi.

Azam FC.Razack Abalora, Himid Mao, Bruce Kangwa, Agrey Morris, Yakubu Mohamed, Stephan Kingue, Salum Abubakari, Joseph Mahundi, Bernard Arthur, Shaban Chilunda na Enock Atta.

Kikosi cha Yanga. Youthe Rostand, Kelvin Yondani, Gadiel Michael, Hassan Kessy, Raphael Daud, Andrew Vicent, Said Juma, Papy Kabamba Tshishimbi, Obrey Chirwa, Ibrahim Ajibu na Emmanuel Martin.


Mechi nyingine zilizochezwa ni Mwadui dhidi ya Njombe waliopata sare ya mabao 2-2 na Mbeya City dhidi ya Mtibwa sare ya bila kufungana 0-0. Na Kagera Sugar na Lipuli pia zikitoka sare ya 0-0.

No comments:

Post a Comment