Saturday 27 January 2018

Vinara Simba kibaruani Leo Ikiivaa Majimaji

Na Mwandishi Wetu
SIMBA SC kesho Jumapili ina kibarua kigumu pale itakaposhuka kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kukabiliana na Majimaji FC kwenye mchezo wa kukamilisha raundi ya kwanza ya Ligi Kuu Bara msimu huu.

Mchezo huo utakuwa ndio wa kwanza kwa kocha raia wa Ufaransa, Pierre Lechantre kuiongoza timu hiyo ambaye hivi karibuni aliingia mkataba wa kuwa Kocha Mkuu wa timu hiyo akichukua mikoba iliyoachwa wazi na Mcameroon, Joseph Omog.

Simba inaoongoza kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 32 ikifuatiwa na Azam yenye pointi 30 huku Yanga ina pointi 28, itahitaji ushindi kwa udi na uvumba ili kumaliza mzunguko wa kwanza ikiwa kileleni.

Tangu Simba imtimue kazi Omog mwishoni mwa mwaka jana, timu hiyo ilikuwa chini ya kocha msaidizi Masoud Djuma ambaye aliiongoza kwenye mechi mbili za ligi na kupata ushindi mnono, iliichapa Singida United mabao 4-0 kwenye Uwanja wa Taifa, kisha Kagera Sugar ikiwa nyumbani kwenye Uwanja wa Kaitaba mabao 2-0.

Mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu kwa Simba kutokana na ukweli kuwa Majimaji hawataingia kinyonge, kwani nao pointi tatu zina umuhimu mkubwa baada ya kuwa na pointi 13 kwenye nafasi ya 11 katika msimamo wa ligi.

Akizungumzia mchezo huo kocha Djuma, alisema kuwa si yeye wala kocha wake mkuu, Lechantre wote hakuna anayefahamu timu hiyo vizuri, lakini hilo haliwatishi kwani wameshapata mbinu za kukabiliana nayo.

Alisema kuwa wamekaa na kupanga mikakati yao ambayo moja wapo ni kuingia kwa kushambulia kwa nguvu mwanzo mwisho ili kuwafanya wapinzani wao hao wasitumie mchezo wa kupaki basi.

“Kiukweli mimi pamoja na Kocha Mkuu hakuna anayeijua vizuri Majimaji, lakini hii haiwezi kutufanya tushindwe kupata ushindi kwao, Simba kwa sasa inajitengenezea nafasi ya kuwa bingwa hivyo tunataka mchezo huu tushinde ili tuzidi kuwa kwenye nafasi nzuri,” alisema Djuma.

Kwa upande wao, Majimaji yenye maskani yake Songea mkoani Ruvuma, kupitia kwa mchezaji wao nyota, Jerry Tegete, alisema kuwa mchezo huo kwao wanautizama kwa jicho la tatu kwani wanahitaji kuondoka na pointi tatu ambazo zitawafanya wasogee juu kwenye msimamo wa ligi.

Alisema kuwa wanafahamu wazi kuwa wapinzani wao hao wameonesha kiwango kizuri hivi karibuni pamoja na ujio wa kocha mpya, utawafanya waingie kwenye mchezo huo kwa kujiamini, lakini hayo yote hayawatishi na wanachokitaka ni kurudi Songea na ushindi tu.


“Ukiangalia ligi kwa sasa inaelekea mzunguko wa pili ambao ni wa lala salama,  tunahitaji pointi tatu kwenye mchezio huo ambazo zitatufanya tukae sehemu nzuri wakati ligi ikiwa inaelekea ukingoni,” alisema Tegete.

No comments:

Post a Comment