Monday 22 January 2018

Simba Yaichapa Kagera 2-0 na kurejea kileleni

Na Mwandishi Wetu
MABAO mawili yaliyofungwa na Said Ndemla na John Bocco ‘Adebayor’  dhidi ya Kagera Sugar, leo yameirudisha Simba kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, na kuishusha nafasi ya pili Azam iliyokuwa imekaa nafasi hiyo kwa muda baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Tanzania Prisons jana.

Ushindi huo unaifanya Simba kufikisha pointi 32, katika michezo 14 na wanatarajiwa kumaliza mzunguko wa kwanza wikiendi inayokuja kwa kukabiliana na Majimaji Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

Katika dakika 45 za kipindi cha kwanza, timu zote mbili zilishambuliana kwa zamu na kupoteza nafasi kadhaa walizozipata, huku wachezaji wawili wa Kagera Sugar, Juma Nyosso na Mohamed Fakhi wakioneshwa kadi za njano kutokana na kucheza rafu mbaya kwa wachezaji wa Simba.

Kipindi cha pili Simba waliingia kwa kasi na kufanikiwa kupata bao la kuongoza dakika ya 69, lililofungwa na Ndemla aliyemalizia pasi murua ya Shiza Kichuya na kupiga shuti, ambalo kipa wa Kagera Sugar, Juma Kaseja alibaki akiukodolea macho ukitinga nyavuni kwake.

Kagera Sugar walijitahidi kupambana kutafuta bao la kusawazisha kupitia kwa washambuliaji wake, Atupele Green na Pastory Athanas, lakini safu ya ulinzi ya Simba ilikuwa makini kuondosha hatari zote langoni mwao.

Dakika ya 79 Bocco, aliifungia Simba bao la pili na kuihakikishia timu hiyo ushindi akimalizia krosi nzuri iliyotokana na jitihada kubwa za beki Shomar Kapombe aliyeingia dakika ya 71 kuchukua nafasi ya Nicholaus Gyan.

Hiyo ilikuwa ni mechi ya kwanza kwa Kapombe tangu aliposajiliwa na Simba, akitokea Azam FC, na kabla ya kupiga krosi hiyo alifanya kazi kubwa ya kumtambuka beki wa Kagera Sugar Adeyum Mohamed.

Chirstopher Edward wa Kagera ambaye aliigia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Athanas mara kadhaa alimjaribu kipa Aishi Manula wa Simba, lakini lengo lake lilishindikana kutokana na kipa huyo kuwa imara kwa kudaka mashuti yote ya wapinzani wao.

Mshambuliaji Emmanuel Okwi ambaye katika mchezo uliopita dhidi ya Singida United alifunga mabao mawili akitokea benchi, jana hakuweza kufurukutwa baada ya kuwekwa chini ya ulinzi mkali na Juma Nyosso  ingawa dakika za mwishoni mwa mchezo huo alikaribia kufunga bao, lakini Kaseja alifanya kazi nzuri kwa kuuwahi mpira.


Wakati huo huo; timu ya Singida United nayo ililazimishwa sare kwa kutoka sare ya kufungana 1-1 na Majimaji FC katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Majimaji mjini Songea.

No comments:

Post a Comment