Monday 8 January 2018

Maelfu ya Wanafunzi Kuchuana Tuzo za Kimataifa za DStv Eutelsat Star

 
*
  Tanzania yajipanga kutetea ushindi ilioupata msimu uliopita

*  Wanafunzi wakereketwa  wa Sayansi na Teknolojia kuoneshana umwamba

Na Mwandishi Wetu

MSIMU wa saba wa tuzo maarufu barani Afrika kwa wanafunzi wapenzi wa masomo ya Sayansi na Teknolojia, DStv Eutelsat Star Awards, umezinduliwa rasmi, ambapo Tanzania ambayo ilishika nafasi ya pili katika tuzo za mwaka jana kupitia mwanafunzi Davids Bwana, inatarajia kuongeza nguvu na hatimaye kuibuka kidekea.

Kama ilivyokuwa siku za nyuma, tuzo hizo zinahusisha uandishi wa insha maalum au kuandaa bango lenye ujumbe kuhusiana na elimu ya anga hususan Setelait. Wanafunzi wa shule za sekondari wenye umri kati ya miaka 14 – 19 wanaruhusiwa kushiriki kinyang’anyiro hicho kitakachoendelea hadi mwishoni mwa mwezi ujao.

Kwa miaka sita mfululizo, tuzo hizi zimekuwa chachu kubwa kwa vijana wenye ari ya kuwa wanasayansi huku zikiangazia ni jinsi gani sayansi ya setelait inavyoweza kubadilisha maendelea, uchumi, na maisha kwa ujumla ya watu wote ulimwenguli.

Kwa mwaka huu, washindani watatakiwa kuandika insha au kubuni bango kuhusu manufaa yaliyoletwa na uvumbuzi wa setelaiti katika maisha ya kila siku hapa ulimwenguni na ni jinsi gani setelait imekuwa kama kiungo muhimu kwa shughuli zote zinazofanyika kote duniani.

Kama kawaida, tuzo hizi zina zawadi kabambe, ambapo mshindi wa Insha atapata fursa ya kuzuru kituo cha Eutelsat nchini Ufaransa na pia kwenda Guiana kushuhudia mubashara urushwaji wa setelait angani.

Mshindi wa bango atajishindia safari ya kwenda nchini Afrika Kusini na kutembelea kituo cha anga cha nchi hiyo na pia Makao Makuu ya MultiChoice Africa akiwa kama mgeni maalum.  Shule zitakazotoa washindi hao zitapata zawadi ya kufungia huduma ya DStv bure.

Insha pamoja na mabango hayo hupitiwa na timu ya watahini wenye uzoefu mkubwa katika hatua mbili. Hatua ya kwanza ni katika kila nchi inayoshiriki, ambapo kila nchi huwasilisha mshindi wa Insha na mshindi wa Bango. Hawa wawili huingia kwenye kinyang’anyiro na washindi kutoka mataifa mengine kote barani afrika.

Washiriki wote wanaweza kupata fomu za ushiriki kutoka ofisi zote za Multichoice au mtandaoni kupitia www.dstvstarawards.com. Lugha inayotumika kwa tuzo hizo ni Kiingereza na kazi zote zitakazowasilishwa zitatathminiwa kulingana na vigezo mbalimbali ikiwemo ubunifu, usahihi wa maelezo na uhalisia. Pia kuwa mara ya kwanza washiriki wote wanaweza kutoa maoni na kuwasiliana kupitia ukurasa maalum wa facebook.


Taarifa zote kuhusu vigezo, zawadi na nyinginezo zinapatikana katika tovuti maalum ya tuzo hizo ambayo ni: http://www.dstvstarawards.com/about.html

No comments:

Post a Comment