Monday 15 January 2018

Wanandoa matatani kwa utesaji familia

NEW YORK, Marekani
Polisi nchini Marekani inawashikilia watu wawili baada ya kugundulika kwa watu 13 wanaodaiwa kufichwa ndani ya nyumba yao, huku baadhi yao wakiwa wamefungwa pingu vitandani zenye minyororo yenye kufuli.

Wanandoa hao, David Allen Turpin mwenye umri wa miaka 57 na Louise Turpin miaka 49 wanashikiliwa kwa makosa ya kuwatesa na kuwaweka `korokoroni’ watoto kadhaa.

Watu 13, wenye miaka kati ya miwili na 29, walikutwa ndani ya nyumba ya wanandoa hao katika kitongoji cha Perris Kusini Mashariki mwa Los Angeles, Marekani na wanaaminika kuwa ni ndugu.

Maafisa wa usalama nchini humo, walipata taarifa kutoka kwa mmoja ya waathirika, ambaye alifanikiwa kutoroka Jumapili na kutoa taarifa kupitia namba ya dharura, kutoka katika simu aliyoikuta ndani ya nyumba hiyo.

Polisi wamesema mtoto huyo wakike aliyekuwa akionekana kama ana miaka 10, na aliyedhoofika sana, amedai kuwa ndugu zake 12 bado wanashikliliwa na wazazi wao.

Baadaye maofisa wa polisi walipofika katika eneo hilo waligundua watoto kadhaa wakiwa na pingu vitandani na wengine kufungwa kufuli katika chumba chenye giza, chenye harufu kali.

Hatahivyo, polisi wamesema mara tu baada ya kukamatwa wazazi wa watoto hao hawakuweza kutoa sababu kwanini walifanya jambo hilo.

Jirani zao wanasema ni nadra sasa walikuwa wakiwaona watoto hao, kwani muda wote walikuwa wamefungiwa ndani.


Waathirika hao wote sasa wanaendelea kupata matibabu hospitalini huku wazazi hao wakishikiliwa na polisi wakihojiwa.

No comments:

Post a Comment