Monday 15 January 2018

Refa aliyempiga teke mchezaji matatani Ufaransa

PARIS, Ufaransa
MWAMUZI wa kati Tony Chapron ambaye anadaiwa kumpiga teke mchezaji wa Nantes nchini Ufaransa kabla ya kumtoa nje kwa kadi nyekundu wakati timu hiyo ilipocheza dhidi ya Paris St-Germain (PSG),  amesimamishwa kazi.

Chama cha Soka cha Ufaransa kimetangaza kwamba mwamuzi huyo amesimamishwa kazi kwa muda usiojulikana "hadi uamuzi mwingine utakapotolewa."

Beki Diego Carlos alimgonga mwamuzi Tony Chapron kwa bahati mbaya katika kisigino wakati wakikimbilia ulipo mpira dakika za mwisho mwisho kabla mchezo huo wa Ligue 1 ya Ufaransa haujamalizika.

Chapron alimpiga teke mchezaji huyo na kisha akampa kadi ya pili ya njano kwa sababu ya kulalamika.

Katika mchezo huo, PSG walishinda mechi hiyo kwa bao 1-0.

Nantes wanataka kadi hiyo ibatilishwe kwani isipobatilishwa atakosa mechi moja.
 
Chama cha Soka cha Ufaransa kimesema kuwa chama cha waamuzi kimeamua "kumuondoa Tony Chapron ambaye alikuwa ameteuliwa kusimamia mechi ya Ligue 1 Jumatano kati ya Angers na Troyes, hadi wakati mwingine".

Wameongeza: "Chapron karibuni ataitwa katika Kamati ya Nidhamu ya LFP [Ambao ni Wasimamizi wa Ligi Ufaransa].

"Mwamuzi huyo baada ya kuangalia kwa kina video ya tukio hilo, alikiri kuwa aliangushwa kwa bahati mbaya na halikuwa kusudio la mchezaji huyo.”

Mwenyekiti wa Nantes Waldemar Kita alisema Chapron anafaa kupigwa marufuku kwa miezi sita kwa sababu ya uamuzi huo wenye utata.


Ameongeza kuwa: "Sitaki kukubali kuwa mwamuzi huyo alikusudia kufanya hivyo."

No comments:

Post a Comment