Wednesday 28 February 2018

Lundenga Abwaga Manyanga Miss Tanzania


Uncle Hashimu Lundenga na Basila Mwalukuzi
Na Mwandishi Wetu
WAANDAAJI wa muda mrefu wa shindano la Miss Tanzania Kampuni ya Lino Agency wametangaza kuachia ngazi kwa kutojihusisha tena na shughuli hizo za urembo.

Tangu mwaka 1994 Lino imekuwa ikiandaa shindano hilo kwa mafanikio lakini kuanzia mwaka juzi ilishindwa na kukumbwa na kashfa kadhaa ikiwemo kumpa taji mrembo asiye na sifa na kushindwa kutoa zawadi kwa washindi hali iliyofanya kufungiwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata).

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Lino, Hashim Lundenga ‘Uncle’ alisema wameamua kuachana na shughuli hizo tangu Februari 13, mwaka huu na kuiachia Kampuni ya Look chini ya Mkurugenzi wake Miss Tanzania mwaka 1998, Basila Mwanukuzi.

“Sababu kubwa ya kuacha shughuli hizi ni pamoja na malengo yetu mapya ya kuachia damu changa waendeleze na kuleta chachu ili kuifanya Miss Tanzania iwe juu… ili tusije kupata balaa zaidi tumeamua kumpa mwingine jukumu hili,” alisema.

Lundenga alisema wamejitathmini na kuona kuwa kwa siku za karibuni walishindwa kuandaa shindano hilo kutokana na changamoto mbalimbali ingawa pia, wanajivunia baadhi ya mafanikio ikiwemo kuwahi kumtoa mrembo wa dunia aliyeingia sita bora na kuitangaza nchi kimataifa.

Kwa upande wake, Mwanukuzi alisema anawashukuru Lino lakini pia, waandaaji wa Miss Dunia kwa kumpa kibali kuwa ndiye muandaaji na kuahidi kurudisha heshima ya shindano hilo.

“Tunatambua kumekuwepo na changamoto nyingi hivi karibuni katika uandaaji chini ya Lino, sisi kama Look tumeziona, tumejiandaa kikamilifu na tunaahidi kuboresha na kukuza yarudi katika hadhi yake kwa kuzingatia kanuni zilizowekwa,” alisema.

Alisema watazindua rasmi shindano hilo mwishoni mwa mwezi huu na kuanza mchakato, wakitarajia kupeleka mrembo katika mashindano ya dunia baadaye mwaka huu.

Alisema kupitia mashindano ya mwaka huu wanataka kufanya uchunguzi kujua ni kitu gani wanatakiwa wafanye kufikia vigezo vya kimataifa au kama kuna figisu au siasa zinatumika wajue nini cha kufanya kwa lengo la kuboresha.

 Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Basata, Godfrey Mngereza alisema kama serikali hawana budi kuishukuru Lino kwa kusaidia vijana wengi wa kike kupata ajira kupitia fani hiyo ya urembo.

“Ni imani yetu shindano lipo mikononi mwa mtu ambaye alipitia kwenye urembo, ni kweli kuna changamoto lakini anaweza kuzigeuza na kuzifanya fursa ili kurudi katika hadhi yake,” alisema na kuhimiza wazazi kutokuwa na wasiwasi tena juu ya shindano hilo.

No comments:

Post a Comment