Saturday 10 February 2018

Aguero Atupia Nne City Ikishinda, Arsenal Hoi


LONDON, England
SERGIO Aguero amefunga mabao manne wakati Manchester City ikiendeleza ubabe wake katika kilele cha msimamo wa Ligi Kuu ya England na kufikisha pointi 16 zaidi, huku Harry Kane akifunga wakati Tottenham Hotspur ikiwachapa wapinzani wao wakubwa Arsenal kwa bao 1-0 jana.

Manchester City iliibuka na ushndi mnono wa mabao 5-1 katika mchezo huo uliotawaliwa na washindi.

Baada ya kuanza taratibu kipindi cha kwanza katika mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Wembley, Kane aliruka juu na kuifungia kwa kichwa timu yake akifunga kwa mara ya saba katika mchezo wa saba wa wapinzani hao huku likiwa goli lake la 23 katika ligi hiyo msimu huu.

Spurs, ambayo katika mchezo huo ungeweza kushinda mabao mengi kama ingekuwa makini, lakini umahiri wa kipa wa Arsenal Petr Cech, ndio ulizuia timu hiyo kupata mabao zaidi.

Kwa ushindi huo, Spurs sasa imepanda hadi katika nafasi ya tatu wakati Arsenal iko pointi sita tofauti na Liverpool katika nmafasi ya nne huku kikosi cha kocha Jurgen Klopp kikiwa na mchezo mkononi.

Kwenye Uwanja wa Etihad, Aguero na mkali Kevin De Bruyne, ambaye alisaidia mara tatu, waling’arawakati Man City ikitoa kipigo kwa mabingwa wazamani wa England Leicester katika kipindi cha pili na kuiwezesha timu hiyo kupata ushindi wa 23 katika ligi kati ya 27 msimu huu.

"Nafikiri tulicheza vizuri leo, vijana wamefanya vizuri sana na hasa Sergio Aguero alikuwa mchezaji tofauti kabisa, “alisema Raheem Sterling, ambaye alifunga bao la kwanza la Man City, alipozungumza baada ya mchezo huo.

AGUERO AISIYEZUILIKA

 Baada ya Sterling na Jamie Vardy walipofunga mabao katika kipindi cha kwanza kwa kila upande, Aguero alitawala ufungaji baada ya kutupia mabao mawili ndani ya kipindi cha dakika nane  baada ya mapumziko.

Mshambuliaji huyo alikamilisha hat-trick yake kabla ya kufunga la nne, baada ya kupiga mpira uliogonga mwamba na kutinga wavuni.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 tayari ameshafikisha mabao 21 ya ligi msimu huu na kuwa mchezaji wanne kufunga zaidi ya mabao 20 katika misimu minne ya ligi mfululizo.

No comments:

Post a Comment