Friday 24 April 2015

TYADCO wazindua kongamano la kupiga vita malaria kwa watoto wenye ulemavu

*Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wachangia Sh. Milioni 5


Mwenyekiti wa Tanzania Youth Alliance For Development and Corporation (TYADCO), Aloyce Msana akizungumza wakati wa uzinduzi wa kongamano la kupiga vita malaria kwa watoto wenye ulemavu jijini Dar es Salaam hivi karibni.

Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), hivi karubuni ilitoa hundi yenye thamani ya Sh. 5,200,000 kwa Tanzania Youth Alliance For Development and Corporation (TYADCO), kwa ajili ya kupambana na malaria kwa watoto wenye ulemavu.

Hundi hiyo ilikabidhiwa kwa mwenyekiti wa (TYADCO), Aloyce Masana na Mwanasheria Mkuu wa TAA, Ramadhani Maleta kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Suleiman S. Suleiman.

Akizungumza kwa niaba ya Suleiman, Maleta, ambaye pia ni wakili alisema kuwa, mamlaka yao inatambua kuwa, malaria ni ugonjwa hatari ambao hupoteza maisha ya watoto, vijana na hata wazee kwa wingi hapa nchini.

Mwanafunzi wa shule ya sekondari Jangwani akisoma risala wakati wa uzinduzi wa kongamano hilo.
Alisema kuwa kutokana na hali hiyo ni jukumu letu sote kushirikiana katika kuhakikisha kuwa tunapambana na hatimaye kuutokomeza kabisa ugonjwa huu, ambao ni tishio hasa kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitatu na mama wajawazito.

Suleiman alisema kuwa kamwe Watanzania tusikubali ndoto za  vijana wetu hawa za kuwa Marubani, Waandisi, Wanasheria, Waandishi wa Habari n.k zisipotee kwa kukatishwa na vifo vinavyotokana na ugonjwa wa malaria.

Wanafunzi wakicheza mchezo wa kuigiza wakati wa uzinduzi wa kongamano hilo.
Nadhani wakati umefika sasa kwa kila mmoja wetu kuhakikisha anashiriki kikamilifu katika mapambano haya ya kuutokomeza ugonjwa huu, kwani kila vita hii sio ya watu au taasisi fulani, Hii ni vita ya wote na ndio maan sisi TAA hatukusita kushiriki kongamano hili la kuchangia, alisema.

Uzinduzi huo ulikwenda sambamba na kongamano maaluma la kuzuia malaria kwa watoto wenye ulemavu, ambapo zaidi ya watoto 300 walihudhuria kutoka shule na taasisi mbalimbali zilishiriki katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Pia katika kongamano hilo kulijadiliwa masuala ya haki za wanafunzi na watoto wenye ulemavu, afya kwa vijana, pamoja na elimu ya kujitambua kwa wote.

TAA kama zilivyo taasisi zingine za kiserikali hapa nchini, inatilia mkazo sana umuhimu wa haki za watoto wenye ulemavu, afya na elimu ya ufundi stadi kwa watoto hao.

Mwanasheria Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini, Wakili Ramadhani Maleta (kulia) akimkabidhi hundi mwenyekiti wa TYADCO, Aloyce Msana huku Mbunge wa Viti Maalum Al-Shaymaa Kwegyir akishuhudia.
Suleiman alisema ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha tunawasaidia vijana hao kwa ujumla ili waweze kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii pamoja na kufikia malengo ya Millenia.

Mbali na TAA kuchangia kiasi cha Sh. Milioni 5, Kampuni ya Mabibo Beer Wine & Spirits kupitia kwa Mama Rugemalila, ilitoa kiasi cha Sh. Milioni 3 kwa ajili ya kuwasaidia watoto hao walemavu kupambana na malaria.

Naye Masana alisema kuwa, kongamano hilo lilihusu pia kujadili mapungufu yaliyopo baina ya matumizi ya pombe, madawa ya kulevya na mimba za utotoni, ambavyo huwagusa pia vijana wenye ulemavu.

Kingine ni kutathimini na kutoa mpango mkakati wa kupambana na tatizo la kukata tamaa kwa watoto wenye ulemavu.

Aidha, shule ya sekondari ya Jangwani ilisema kuwa pamoja na ukongwe wao, lakini bado wanafuzi wao walemavu wanapata shida ya usafiri, hivyo waliomba wasaidiwe gari.

Baadhi ya wanafunzi waliohudhuria uzinduzi wa kongamano la kupiga vita malaria kwa watoto wenye ulemavu lililofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
Naye Rugemalira alisema kuwa kampuni yao kama kampuni zingine za kijamii hapa nchini inatilia mkazo sana umuhimu wa elimu na afya kwa watoto wenye ulemavu na hivyo adhma yao ni kuangalia jinsi ya kuwasaidia watoto hao ili waweze kufikia malengo yao.

Pia, aliyaomba mashirika mbalimbali, taasisi za kidini na zingine kuwa bega kwa bega katika kusaidia watoto wenye ulemavu kukabiliana na changamoto zinazowakabili.

 

No comments:

Post a Comment