Sunday 19 April 2015

300 wakamatwa Afrika Kusini kwa vurugu za kiubaguzi




Baadhi ya raia wa kigeni wanaoishi Afrika Kusini wakijiandaa kuondoka kwa mabasi baada ya vurugu za kiubaguzi nchini, ambazo zinawalenga wageni.


Raia wa Msumbiji ambaye ni mmiliki wa duka moja nchini Afrika Kusini akiwa hoi baada ya kupigwa vibaya na wenyeji. Raia huyo alifariki dunia siku mbili baadae hospitalini kutokana na kipigo hicho.

Raia huyo wa Afrika Kusini ambaye alikuwa akimiliki duka kubwa.


JOHANNESBURG, Afrika Kusini
ZAIDI ya watu 300 wamekamatwa nchini hapa kuhusiana na vurugu za kiugabuguzi dhidi ya wahamiaji kutoka sehemu mbalimbali za Afrika, amesema waziri wa mambo ya ndani ya nchi.

Malusi Gigaba alitoa onyo kwa wote wanahusika kuwafanyia vurugu hizo raia hao wa kigeni wataadhibiwa kwa kufuata sheria za Afrika Kusini.

Angalau watu sita wameuawa katika wiki mbili zilizopita kutokana na vurugu hizo.

Wakati waziri huyo akiyasema hayo, Rais Jacob Zuma amekatisha ziara yake ya Indonesia na kurejea haraka ili kulishughulikia tatizo hilo ambalo linaonekana kuwa kubwa kila kukicha.

Zuma aliapa kuwa mashambulizi dhidi ya raia hao wa nchi zingine za Afrika zinakoma mara moja.

Maelfu ya wageni waliacha nyumba zao na kwenda katika makambi maalum, na wengine kukimbilia nchi za jirani za Zimbabwe, Malawi na Msumbiji ili kukwepa mashambulizi hao kutoka kwa wenyeji.

Akizungumza na waandishi wa habari, Gigaba alisema watu 307 wamekamatwa kuhusiana na vurugu hizo.

"Kila kitu kinafanywa kurejesha amani, alisema. "Serikali itatekeleza sheria dhidi ya watu hao ambao aliwaita wasio waungwana.

Kwa upande wa Zuma, yeye aliapa kuhakikisha kuwa, mashambulizi dhidi ya raia hao, yanakwisha huku akiwasisitiza na kuwaomba raia hao wasiikimbie nchi hiyo.
 
Kipindi cha wiki tatu cha vurugu na mashambulizi dhidi ya raia wageni nchini humo, kimesababisha vifo vya watu sita hadi sasa na wengine zaidi ya 5,000 kukimbia makazi yao.

Vurugu hizo, zilizoanzia katika jiji la Durban, baadaye zilisambaa hadi katika maeneo mengine nchini humo na kusababisha historia ya Waafrika Kusini kubagua raia wa kigeni kujirudia, ambapo mwaka 2008 vurugu kama hizo ziliibuka na kusababisha vifo vya takribani watu 62.

No comments:

Post a Comment