Sunday 6 August 2017

Marwa, Angel vinara Bagamoyo Marathon 2017

Wakimbiaji, Dickson Marwa (kulia) na Augustine Sulle wakichuana katika mbio za Bagamoyo Historical Marathon 2017 leo mjini Bagamoyo. Marwa alishinda mbio hizo za kilometa 21.
Na Mswandishi Wetu
DICKSON Marwa na Angel John leo wameibuka nyota wa Bagamoyo Historical Marathon 2017 baada ya kumaliza wa kwanza katika mbio za kilometa 21 kwa upande wa wanaume na wanawake na kila mmoja kujizolewa sh 500,000 fedha taslimu pamoja na medali ya dhahabu.

Marwa alimshinda mpinzani wake wa karibu katika mbio hizo, Augustine Sulle kwa kutumia saa 1:05:07.08 wakati Angel alimzidi makali nguli wa riadha nchini Zakia Mrisho na kutwaa medali ya dhahabu kwa kutumia saa 1:20:56.56.

Mshindi huo kwa wanaume katika mbio za mwaka jana alimaliza katika nafasi ya ili akiwa nyuma ya Alphonce Simbu aliyemaliza wa kwanza. Agustine Sulle alimaliza wa pili kwa saa 1:05:12.93 wakati mshindi watatu alikuwa Wilbert Peter aliyemaliza mbio hizo za kilometa 21 kwa saa 1:07:36.37.
Bakari Jumanne alimaliza mbio hizo katika nafasi ya nne kwa kutumia saa 1:07:44.27, huku Hamisi Athumani aliibuka watano kwa kutumia saa 1:08:15.15.

Kwa upande wa wanawake, Angel alimaliza wa kwanza katika mbio hizo za kilometa 21 kwa kutumia saa 1:20:56.56 na kumshinda Zakia aliyemaliza wa pili kwa kutumia saa 1:21:26.43 huku Neema Msuadi akimaliza katika nafasi ya tatu kwa saa 1:26:22.77.

Mshindi wa kwanza wa mbio hizo za nusu marathoni kwa wanaume na wanawake kila mmoja aliondoka na sh 500,000 wakati wale walioshika nafasi za pili waliondoka na sh 300,000 na watatu sh 200,000 kila mmoja. Washiriki wote waliomaliza walipata medali.

Marwa akizungumza baada ya mbio hizo alisema kuwa zilikuwa ngumu kutokana na mpinzani wake, Sulle kuwa fiti na kuchuana naye vikali katika karibu kilometa 20 kabla ya kumuachia ikiwa imebaki kilometa moja kumalizika kwa mbio hizo.

“Kwa kweli mbio ilikuwa ngumu sana, hasa kutokana na mpinzani wangu kuwa na nguvu sana hadi pale nilipotumia uzoefu ilipobaki kilometa moja kabla ya kumalizika mbia nilipochomoka na kumuacha, “alisema Marwa ambaye ameshiriki mbio nyingi ndani nan je ya nchi.
Washindi wa Bagamoyo Historical Marathon kwa upande wa wanawake, Angel John (katikati), Zakia Mrisho (kushoto) na Neema Msuadi wakiozi kwa picha baada ya kukabidhiwa medali zao.
Angel alisema kuwa mbio haikuwa ngumu sana, lakini tatizo kubwa lilikuwa wingi wa magari na bodaboda.


Kwa upande wa kilometa 10, mshindi wa kwanza kwa wanaume alikuwa Jackson Makombe aliyetumia dakika 31:28:28 huku ushindi wa pili na tatu ulikwenda kwa Emmanuel Mpali na Athumani Rajabu waliotumia dakika 32:47:18 na  33:42:13 wakati mshindi wa kwanza kwa wanawake alikuwa Rosemary Boniface aliyetumia dakika 40:31:19 na Faraja Emmanuel alimaliza wa pili kwa dakika 40:41:28.
Mshindi wa pili wa kilometa 21 kwa wanawake, Zakia Mrisho akiokea zawadi yake leo.








No comments:

Post a Comment