Monday 14 August 2017

Simbu na wenzake kupokewa kishujaa kesho JNIA

Na Mwandishi Wetu
MSHINDI wa medali ya shaba wa mashindano ya 16 ya dunia yaliyomalizika jijini London, Uingereza jana, Alphonce Simbu pamoja na wenzake wanatarajia kuwasili kesho mchana na kupokewa kifalme.

Tanzania katika mashindano hayo yaliyoanza Agosti 4 na kumalizika jana, ilipeleka wanariadha wanane lakini Simbu peke yake ndiye aliyetwaa medali katika mbio za marathoni kwa kutumia saa mbili na dakika tisa  katika nafasi ya tatu.

Hiyo ni medali ya kwanza kwa Tanzania kupata baada ya miaka 12 baada ya Christopher Isegwe kumaliza wa pili na kupata medali ya fedha katika mbio za marathoni na kuondoka na medali ya fedha katika mashindano yaliyofanyika Helsinki, Finland mwaka 2005.

Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Wihlehm Gidabuday amesema leo Jumatatu kuwa Simbu na wenzake wataata mapokezi makubwa watakaowasili kwenye Kiwanja cha Kimataifa cha Ndege cha Julius Nyerere (JNIA) kesho mchana kwa ndege ya Emirates wakitokea London kupitia Dubai.

Mara baada ya kuwasili, timu hiyo itapokewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe na kufanya mkutani na waandishi wa habari katika kiwanja hicho kuelezea yaliyojiri London.

Kwa mujibu wa Gidabuday, nje ya kiwanja hicho kunatarajia kuwepo burudani kadhaa vikiemo vikundi vya JKT vitakavyoburudisha wanariadha hao pamoja na wadau mbalimbali wa michezo na hasa riadha watakaofika kuwaokea akina Simbu.

Inaelezwa kjuwa Simbu anayedhaminiwa na DStv na wachezaji wengine watakuwa ndani ya gari la wazi, ambalo litawazungusha katika kitaa mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam wakipitia Ilala, Kariakoo na kwingineko kabla ya kutua katika hoteli ya Protea iliyopo Oysterbay jirani na kanisa la Mtakatifu Petro (St Peter’s), ambako Simbu atapumzika kabla ya keshokutwa kwenda kwao Arusha.

Mbali na Simbu, wanariadha wengine waliokuwemo katika timu hiyo ni pamoja na Stephano Huche, Ezekiel Ngimba, Sarah Ramadhani na Magdalena Shauri (Marathoni), Failuna Abdi (Meta 10,000), Gabriel Geay na Emmanuel Giniki (Meta 5,000).

Geay hakukimbia katika mbio zake kutokana na kuwa majeruhi huku Shauri akishindwa kumaliza baada ya kukimbia kwa zaidi ya kilometa 25 kutokana na kuwa na maumivu aliyokuwa nayo hata kabla ya kuondoka nchini.

Nyota ya Simbu ilianza kung’ara katika Michezo ya Olimpiki iliyofanyika Rio, Brazil 2016 wakati alipomaliza wa tano kwa kutumia saa 2;11:15 kabla ya kumaliza wa kwanza katika Mumbai Marathoni mwanzoni mwa mwaka huu alipotumia saa 2:09:32,  kabla ya kuboresha zaidi muda wake bora binafsi pale aliomaliza wa tano kwa kutumia saa 2:09:10 katika London Marathoni licha ya kuibuka watano.

No comments:

Post a Comment