Friday 4 August 2017

Yanga sasa kujipima kwa Singida United Jumamosi

Kocha mkuu wa timu ya Singida United, Felix Minziro (aliyesimama) akifuatilia mchezo wa kirafiki wa timu yake dhidi ya Ashanti United uliochezwa kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam hivi karibuni. Ashanti ilishinda kwa mabao 2-1.
Na Mwandishi Wetu
MCHEZO wa kirafiki kati ya Yanga na Singida United uliopangwa kufanyika Agosti 6, mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam umerudishwa nyuma kwa siku moja kupisha shughuli maalum ya Kiserikali siku hiyo na sasa utafanyika Jumamosi ya Agosti 5.

Yanga inatarajiwa kumenyana na Singida United inayofundishwa na kocha wake wa zamani, Mholanzi Hans van der Pluijm katika mchezo maalum wa kila timu kujaribu kikosi chake kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Na kwa sasa kikosi cha kocha Mzambia, George Lwandamina kipo mjini Morogoro kimeweka kambi ya kujiandaa na msimu mpya, wakianza na mchezo wa Ngao ya Jamii, dhidi ya mahasimu, Simba, Agosti 23, mwaka huu Uwanja wa Taifa.

Singida United imerejea Ligi Kuu msimu huu tangu iliposhuka mwaka 2002, lakini baada ya kupanda imefanya usajili wa gharama kubwa, ikichukua wachezaji wenye uzoefu mkubwa kutoka timu mbalimbali za ndani na nje ya nchi.

Timu hiyo si tu itatoa upinzani kwa Yanga Agosri 5, bali pia wanatarajiwa kuwa tishio katika msimu huu wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

No comments:

Post a Comment