Saturday 5 August 2017

Serikali yaipongeza TOC kuandaa kozi ya michezo

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yusuf Singo (wa pili kutoka kushoto), akiwa na washiriki wa mafunzo ya juu ya usimamizi wa uongozi wa Michezo pamoja na viongozi wa TOC kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo.
Na Mwandishi Wetu
KAMATI ya Olimpiki Tanzania (TOC), imepongezwa kwa kuandaa kwa mara ya kwanza Kozi ya Juu ya Usimamizi wa Michezo, kwani itakuwa na manufaa katika medani ya michezo.

Pongezi hizo zimetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo, Dk Yusuf Singo, wakati akizindua kozi hiyo kwenye ukumbi wa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam jana.

Singo aliyemwakilisha Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe, alisema mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka kwa sababu hivi sasa michezo inahitaji kuendeshwa kisasa zaidi.

Alisema kuna vyama ambavyo alitarajia kuona viongozi wake katika kozi hiyo kutokana na hali ilivyonavyo lakini hawapo, hivyo TOC iangalie namna ya kuwafikia.

“Michezo inabadilika kila wakati, viongozi walioongoza zamani ni tofauti na sasa kutokana na mabadiliko. Ndio maana napenda kusisitiza kuwa elimu hii isambae katika vyama vyote, ikiwezekana Kamati nzima za Utendaji,” alisema Singo.

Aidha, aliwataka washiriki wakazanie mafunzo hayo na kuhakikisha wote wanahitimu na kwenda kuonesha mabadiliko katika utendaji wao na kwamba yeye binafsi atayafuatilia kwa karibu.

Awali akitoa taarifa fupi ya kozi hiyo, Mkufunzi Mkuu wa kozi hiyo, Henry Tandau, ambaye atasaidiwa na Mahmoud Suleiman Jabir, alisema kozi hiyo ni ya kwanza kufanyika hapa nchini.
Tandau, alisema kozi hiyo itakayokuwa na awamu saba inashirikisha washiriki 15 badala ya 16 kutoka vyama mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar.
Naye Katibu Mkuu wa TOC, Filbert Bayi akitoa neno la shukrani, alisema watafanyia kazi suala la kutoa semina elekezi kwa viongozi wa vyama vya michezo.

Bayi, alisema mara nyingi wanapoandaa kozi kama hizo, viongozi wakubwa kama Mwenyekiti, Katibu, Muhazina na wengineo hawajitokeza wakati wao ndio wenye matatizo ya migogoro, badala yake wanaohudhuria ni viongozi wa kawaida.

Washiriki wa kozi hiyo na vyama wanavyotokea kwenye mabano ni Nasra Juma Mohamed (Vinyoya Zanzibar), Juma Zaidi Hamisi (Tenisi Zanzibar), na Musa Abdulrab Fadhil (Mikono Zanzibar).
Wengine ni Amina Ahmed (Kikapu), Wilfred Kidau, Danny Msangi (TFF), Suleiman Ame Hamis (Riadha Zanzibar), Sunday Kayuni (Makocha), Asha Muhaji (Taswa), Ruth Kiwia (Mikono), na Ingridy Kimario (Ofisa Michezo Temeke).


Washiriki wengine ni Muharami Mchume (Wavu), Juliana Yasoda (Chama cha Michezo cha Wanawake), Irene Mwasanga (Tenisi), na Mwinga Mwanjala (Riadha).
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yusuf Songo (kushoto) akiteta na Rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Gulam Rashid wakati akifungua semina ya juu ya uongozi wa michezo kwenye Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam leo.

No comments:

Post a Comment