Friday 30 June 2017

JNIA TB III kuanza kutumika Decemba mwakani

Jengo la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Terminal 3 likionekana kwa nje leo.
Na Mwandishi Wetu
UJENZI wa jengo la kuondokea na kuwasili abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Terminal 3 utakamilika Septemba mwakani na kuanza kutumika rasmi miezi mitatu baadae, imeelezwa.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame  Mbarawa aliyasema hayo leo baada ya kukamilisha ziara ya kutembelea jengo la kiwanja hicho, ambalo ujenzi wake unaendelea.

Mbarawa alisema kuwa, ujenzi huo unaendelea vizuri na utakamilika Septemba 2018 na kuanza rasmi kutumika Desemba mwaka huo huo.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa akisalimiana na wafanyakazi kabla ya kutembelea Jengo la Kiwanja cha Ndege cha Julius Nyerere Terminal 3 leo.
Alisema jengo hilo litakakuwa likichukua jumla ya abiria milioni 6 kwa mwaka tofauti na jengo lile la Terminal Two, ambalo lina uwezo wa kuchukua abiria milioni 2 tu kwa mwaka, hivyo majengo hayo mawili yakakuwa yakichukua jumla ya abiria milioni 8 kwa mwaka.

Alisema kuwa hatua ya kuchukua abiria wengi litasaidia kuongeza watalii wanaotembelea vizutio vilivyopo nchini.
Waziri Profesa Mkame Mbarawa akisaini kitabu cha wageni leo.
Aliongeza kuwa eneo la maegesho ya kiwanja hicho yatakuwa yakichukua jumla ya ndege 21 kwa wakati mmoja, hivyo kuwezesha watu wengi wakiwemo watalii kuja nchini kupitia katika kiwanja hicho cha ndege.

Pia Mbarawa alimuhakikishia mkandarasi wa uwanja huo kuwa, atalipwa fedha zake zote kwa wakati kama alivyoahidi Rais John Pombe Magufuli alipotembelea kiwanja hicho mapema mwaka huu.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Makame Mbarawa (katikati) akipata maelezo kutoka kwa Mkandarasi Simba Charles leo. Kulia ni  Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mtengeka Hanga.
Mbarawa alitembelea maeneo mbalimbali ya jengo hilo yakiwemo yale ya kukaa abiria wanaondoka na kuwasili, vyumba vya wageni mashuhuri na sehemu tofauti tofauti, ambazo zinajengwa kwa umahiri mkubwa.
Meneja wa Ujenzi wa Kiwanja cha Kimataifa cha Ndege cha Julius Nyerere (JNIA) wa Kampuni ya BAM International-Africa, Ray Blumrick akimpa maelezo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Makame Mbarawa (watatu kushoto) alipotembelea jengo la kiwanja hicho leo Ijumaa.
Waziri Mbarawa alipata maelezo ya kina ya ujenzi huo kutoka kwa mkandarasi, Simba Charles na Meneja Ujenzi, Ray Blumrick wa Kampuni ya BAM-Unternational-Afrika.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Makame Mbarawa (wa pili kulia) akifurahia jambo na Mkandarasi Simba Charles alipokagua ujenzi wa jengo la Kiwanja kipya cha Ndege cha Kimatafa cha Julius Nyerere (JNIA) Terminal 3 leo.




No comments:

Post a Comment