Thursday 22 June 2017

Mamlaka Viwanja vya Ndege yahitimisha wiki ya Utumishi wa Umma kwa maonesho ya shughuli zao


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Salim Msangi (wa pili kushoto) na mwanasheria Ramadhani Maleta wakiwa pamoja na wafanyakazi wa Shirika la Ndege la Precision Air jijini Dar es Salaam leo.
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) inakamilisha Wiki ya Utumishi wa Umma kwa kufanya maonesho ya kuonesha shughuli mbalimbali za kila siku wanazozifanya.

TAA ilianza wiki hiyo ya Utumisi wa Umma kwa Makao Makuu kutembelea idara zao mbalimbali ikiwemo ile ya Utawala, eneo la kuwasili na kuondokea abiria mashuhuri au VIP la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Idara ya Usalama, Uhasibu katika eneo hilo.

Wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) wakiwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu, salim Msangi (wa kwanza kushoto waliokaa) na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Joseph Nyahende.

Pia Kaimu Mkurugenzi Mkuu alitembelea eneo la Usalama katika JNIA Terminal Two, Idara ya Manunuzi, Usalama na kwingineko, ambako alizungumza na wafanyakazi wa idara hizo, ambao walieleza utendaji wao wa kazi na changamoto wanazokumbana nazo katika majukumu yao ya kila siku.

Siku inayofuata, uongozi wa TAA ulikutana na wafanyakazi wa idara zote katika ukumbi wa Kiwanja cha Ndege cha Terminal One, ambako walidajili matatizo mbalimbali yanayowakabili na uongozi ulitoa suluhisho la matatizo hayo.
Katika kutimiza agizo la Serikali la taasisi zake kuadhimisha wiki hiyo kwa kutembelea idara na kusikiliza changamoto zinazowakabili wafanyakazi katika kutekeleza majukumu yao ya siku hadi siku.

Katika kukamilisha wiki hiyo, TAA jana na kesho ina banda lake nje ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), ambako mbali na vipeperushi, majarida na mabango yanayoelezea shughuli zao katika idara tofauti tofauti, pia wapo wafanyakazi wanaotoa maelezo kwa abiria na watu wengine wenye matatizo au kutaka kujua zaidi utendaji wa taasisi hiyo.
Katika banda hilo kuna picha kubwa zinazoonesha viwanja mbalimbali vilivyoboreshwa , ambavyo baadhi yao vilikuwa havina rami lakini sasa vimewekewa rami pamoja na mambo mengine yanayofanywa na TAA.


Wiki ya Utumishi wa Umma inamalizika rasmi kesho nchini kote, huku TAA chini ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Salim Msangi ikijitahidi kuwaelimisha wasafiri na wananchi kwa ujumla juu ya taasisi hiyo na idara zake na jinsi zinavyofanya kazi kwa ujumla.



No comments:

Post a Comment