Monday 30 January 2017

TFF na TOC yazindua programu za maendeleo kwa timu za vijana chini ya miaka 20


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa kushirikiana na kamati ya Olympic Tanzania TOC, wamezindua kampeni maalumu za kuifanikisha Tanzania kushiriki michuano ijayo ya Olimpiki itakayofanyika mjini Tokyo, nchini Japan mnamo mwaka 2020.

Uzinduzi huo uliofanyika kwenye uwanja wa karume jijini Dar es salaam umehudhuriwa na Mkurugenzi wa Michezo Nchini, Yusuph Omari ambaye alikua mgeni rasmi, Rais wa Shirikisho la mpira wa miguu nchini TFF Jamal Malinzi, Makamu wa Rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Henry Tandau, maafisa wa TFF na wadau wengine wa michezo.

 



kampeni hiyo inayoihusisha timu ya taifa ya soka ya vijana chini ya umri wa miaka 20 (Kilimanjaro Worriers) ambayo itawania kufuzu kucheza michuano ya Olimpiki mwaka 2020, imepewa jina la ‘The Road to Tokyo 2020’.

Rais wa TFF Jamal Malinzi, amesema dhamira kubwa waliyojiweka katika harakati hizo ni kuhakikisha vijana wanaendelezwa kisoka kwa ajili ya kufikia malengo ya kwenda kushiriki michuano ya Olimpiki mwaka 2020.

Rais wa TFF  Jamal Malinzi

Mkurugenzi wa michezo Yusuph Omari “Nimesikia program mbalimbali za TFF, naona zinakuja wakati mwafaka. Niwapongeze kwa mipango yenu mizuri kwa sababu inaleta matumaini. Jambo kubwa ambalo linanisukuma na kuwapongeza ni kuwa na program ya vijana, hatuwezi kufanikiwa kama hatutakuwa na program ya vijana.

“Serikali inatambua haya yote mnayofanya ili kuboresha, Serikali imetenga shule 55 ambazo zitakuwa ni maalumu kwa ajili ya vijana, lengo ni kupata vipaji bora ambavyo vitakuwa vikiendelezwa, huku wakiwa wanapata elimu.

Mkurugenzi wa michezo Yusuph Omari


No comments:

Post a Comment