Monday 23 January 2017

Serikali yaridhia kutoa bandarini vifaa vya ujenzi wa jengo la tatu la abiria Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (TB III)

Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, akionesha kitu kwa mbele (hakionekani pichani) kwa Mkurugenzi wa mradi huo, Mhandisi Mohammed Millanga, wakati alipofanya ziara kukagua ujenzi wa jengo la tatu la abiria (TBIII). Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Salim Msangi.
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa amesema serikali italipia haraka vifaa vya ujenzi wa jengo la tatu la abiria la Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBIII) vilivyokwama bandarini.

Prof. Mbarawa alisema hayo hivi karibuni mara baada ya kufanya ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, ambapo alijibu moja ya changamoto zilizosomwa na Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzania (TAA), Salim Msangi kuwa vifaa vya ujenzi vimekwama bandarini.

Mkurugenzi wa Mradi wa Jengo la Tatu la abiria (TBIII), Mhandisi Mohammed Millanga akiendelea kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya ujenzi kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Prof. Makame Mbarawa (aliyeshika miwani), wakati alipokagua ujenzi wa jengo hilo.
“Hivi vifaa vitalipiwa haraka ili mradi uendelee na kumalizika kwa wakati kama ilivyosemwa utakamilika mwishoni mwa mwezi Desemba mwaka huu,” alisema  Prof. Mbarawa.

Alisema anaamini kukamika kwa jengo hili litakuwa bora kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, kwa kuwa  litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni sita kwa mwaka, na litapunguza msongamano uliokuwepo katika jengo la pili la abiria (JNIA-TBII), ambalo lilijengwa kwa ajili ya kuhudumia abiria 1.5 milioni kwa mwaka, lakini sasa linahudumia abiria 2.5 milioni kwa mwaka.

Mkurugenzi wa Mradi wa Jengo la Tatu la abiria (TBIII), Mhandisi Mohammed Millanga akiendelea kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya ujenzi kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Prof. Makame Mbarawa (aliyeshika miwani), wakati alipokagua ujenzi wa jengo hilo.
Awali, Prof. Mbarawa alisema hii ni mara ya tatu kutembelea jengo hili, na amefanya hivyo ili kumsimamia mkandarasi kwa karibu aweze kutoa mradi mzuri usiokuwa na tatizo kwa siku za usoni.

Pia alisema serikali imejipanga kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege ili ndege yake ya Shirika la ndege (ATCL), ambayo imezindua safari zake katika baadhi ya mikoa iweze kutoa na kupaa bila tatizo.

Mkurugenzi wa Mradi wa Jengo la tatu la abiria (TBIII), Mhandisi Mohammed  Millanga akitoa maelezo ya kina kwa  Waziri, Prof. Makame Mbarawa (wa kwanza kushoto), alipotemebelea na kukagua jengo hilo. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Salim Msangi.“Huu mradi wa TBIII sio pekee, vipo viwanja 13 vitaboreshwa kwa kufanyiwa ukarabati na upanuzi, na baadhi yake ni Mwanza, JNIA TBII, KIA, Songwe, Sumbawanga, Tabora, Shinyanga na Kigoma,” alisema Mhe. Prof. Makame Mbarawa.

Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, akitoa tathmini ya ujenzi wa jengo la tatu la abiria (TBIII), mara baada ya kulitembelea. Katikati ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya TAA (MAB), Prof. Ninatubu Lema bna kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa TAA, Bw. Salim Msangi
Awali akisoma taarifa fupi ya mradi wa TB III, Kaimu Mkurugenzi,  Msangi alisema mradi huo umekumbwa na changamoto ya upatikanaji wa fedha kiasi cha Euro 121,634,888.30, ambazo serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango iliahidi kukamilisha taratibu upatikanaji wa fedha mapema ili kutoathiri utekelezaji wa mradi.

Pia  Msangi alisema changamoto nyingine ni uchelewaji wa malipo ya kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), kwa vifaa vilivyopo bandarini hadi sasa inadaiwa Tsh. Bil. 1,362,801,347.00, kati ya fedha hizo Tsh. Mil. 960,153,258.00 ni za kulipia vifaa maalumu vya usalama vya ukaguzi wa abiria (X-ray machine), ambavyo vinatakiwa visiathiriwe na joto.

“Hali hii ya vifaa kuchelewa kutoka inasababisha kuongeza gharama za mradi pamoja na kuchelewesha kazi zilizopangwa kufanyika, na pia hali hii itasababisha uharibifu wa vifaa ambapo serikali itabidi kuvilipia pindi itakapotokea uharibifu,” alisema Bw. Msangi.

Hatahivyo, Msangi alisema ujenzi wa jengo hilo utakaotumia gharama ya Tsh. Bilioni 560, sasa umekamilika kwa asilimia 66.



IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA MAHUSIANO CHA TAA

No comments:

Post a Comment