Saturday 28 January 2017

Kalusha Bwalya amtabiria ubingwa mwingine wa Afrika kocha Renard wa Morocco



LUSAKA, Zambia
GWIJI wa soka nchini Zambia, Kalusha Bwalya anasema kuwa Herve Renard ana uwezo wa kutwaa tena taji la Mashindano ya Mataifa ya Afrika (Afcon) baada ya kuyaangalia mwenendo mzima wa mashindano hayo hadi sasa.

Endapo kocha Renard atatwaa taji la Afcon itakuwa ni mara yake ya tatu akilibeba huku akiwa na timu tatu tofauti baada ya mwaka 2015 kulitwaa akiwa na Ivory Coast baadaya kulitwaa mwaka 2012 akiwa na timu ya taifaya Zambia ya Chipolopolo.

Nahodha huyo wazamani wa Zambia na Rais wazamani wa Chama cha Soka cha Zambia pia aliiambia BBC kuwa, anafikiri mashindano yanayoendelea Gabon yana timu zenye uwezo, ambazo zinakaribiana kwa uwezo, wakati akiangalia mechi za robo fainali zitakazoanza leo Jumamosi.

Timu ya Morocco inayofundishwa na Renard itakwaana na mabingwa mara saba wa Afrika Misri katika mchezo utakaofanyika kesho Jumapili.

Timu zingine zitakazocheza robo fainali ni:- Burkina Faso v Tunisia na Senegal v Cameroon,ambazo mechi zao zote zitapigwa leo Jumamosi, wakati DR Congo v Ghana zitachezwa kesho Jumapili.

No comments:

Post a Comment