Tuesday 13 March 2018

Zawadi Ngorongoro Marathon 2018 Zatangazwa

Na Mwandishi Wetu
WAANDAAJI wa Ngorongoro Marathon 2018 wametangaza zawadi, ambapo mshindi wa kwanza ataondoka na kitita cha Sh milioni 1, ambazo zitafanyika Aprili 21.

Mkurugenzi wa mbio hizo, Meta Petro (pichani chini), akizungumza kwa njia ya simu kutoka Karatu, Arusha jana alisema kuwa, mshindi wa kwanza kwa wanaume na wanawake, kila mmoja ataondoka na Sh milioni 1.

Alisema kuwa mshindi wa pili atapewa Sh 500,000, huku mshindi wa tatu kwa kila upande ataondoka na Sh 250,000.

Alisema kuwa pia kutakuwa na mbio za kujifurahisha za kilometa tano pamoja na zile za watoto wadogo za kilometa 2.5, ambazo hazina viingilio ili kuwawezesha watoto kujitokeza kwa wingi.

Alisema lengo la mbio za mwaka huu ni Kukimbiza Jangili, ambapo wanapiga vita mauaji ya wanyama kama vile tembo, simba, chui, twiga na wengine, ambao wamekuwa wakiuawa kwa sababu ya pembe, meno, kucha na ngozi zao.

Alisema wanyama kama tembo na faru wamekuwa wakiuawa kwa ajili ya biashara haramu ya pembe zao huku twiga na pundamilia wakiuawa kwa ajili ya nyama, na simba na chui wamekuwa wakiuawa kwa ajili ya ngozi zao.
Akielezea ada ya ushiriki, Petro alisema kuwa kwa Watanzania watakaokimbia kilometa 21 watalipa Sh 10,000 kwa fomu huku wageni watalipa dola za Marekani 50.

Alisema kwa wale watakaoshiriki kilometa tano kama timu, kuanzia mtu mmoja hadi watano, watalipia dola za Marekani 500, wakati mtu mmoja mmoja Mtanzania atalipia Sh 10,000 na asiye Mtanzania atalipa dola 10.

Wakati huohuo, Petro amesema kuwa bado wanasaka wadhamini kwa ajili ya mbio hizo, ambazo mbali na kupiga vita vya ujangili, pia zinatangaza vivutio vya utalii nchini.

No comments:

Post a Comment