Tuesday 27 March 2018

Ronaldo Ashindwa Kuiokoa Ureno na Kichapo


GENEVA, Uswisi
MABINGWA wa Ulaya Ureno wakongozwa na mchezaji bora wa dunia wa mwaka, Cristiano Ronaldo, wamepokea kichapo cha aina yake kutoka kwa Uholanzi baada ya kufungwa mabao 3-0 katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki hapa.

Winga wazamani wa Manchester United, Memphis Depay na mshambuliaji wazamani wa Liverpool Ryan Babel waliiwezesha timu ya taifa ya Uholanzi kuwa mbele kwa mabao 2-0.

Beki wa Liverpool Virgil van Dijk, ambaye hivi karibuni alitangazwa kuwa nahodha mpya wa timu ya taifa ya Uholanzi, ndiye aliyefunga bao la tatu huku Ureno ikipata pigo baada ya mchezaji wake Joao Cancelo kutolewa katika kipindi cha pili.

Mchezo huo umemfanya mshambuliaji wa Real Madrid Cristiano Ronaldo kuhitimisha bahati yake ya kufunga mechi tisa mfululizo baada ya kutoka kappa katika mchezo huo.

Nahodha huyo wa Ureno, nafasi yake ilichukuliwa na mchezaji wa Monaco Joao Moutinho katika dakika ya  68, ambapo ameifungia Real Madrid mabao 17 na mawili kwa Ureno, dhidi ya Misri Ijumaa.

Ureno wako katika Kundi B katika fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia pamoja na Hispania, Morocco na Iran, lakini Uholanzi, ambayo ilifungwa 1-0 na England katika mchezo wa kwanza ikifundishwa na Ronald Koeman, ilishindwa kufuzu kwa Kombe la Dunia.

No comments:

Post a Comment