Friday 29 December 2017

TAA Waomboleza Kifo cha Mwanasheria Delfine

Bi. Delfine Mulogo wakati wa uhai wake.
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), inamlilia kwa masikitiko makubwa Mwanasheria wake Bi. Delfine Mulogo (32) aliyekuwa Kituo cha kazi cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) aliyefariki dunia Desemba 25.

Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi, Bw. Mtengela Hanga akisoma wasifu wa marehemu katika kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Augustine Mbezi Temboni, alisema, atakumbukwa kwa uchapakazi, uhodari na uadilifu wake kazini.

Paroko wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Augustine, Padri Fidelis Mfaranyembo lililopo Mbezi Temboni jijini Dar es Salaam, akinyunyizia maji ya baraka kwenye mwili wa aliyekuwa Mwanasheria wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Kituo cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bi. Delfine Mulogo kabla ya kusafirishwa kwenda Kijiji cha Uru Kishumundu Mkoani Kilimanjaro kwa maziko.

“Tunasikitika kumpoteza mwanasheria huyu kijana, kwa niaba ya Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, tunatoa pole kwa wafiwa kwa kuondokewa na mpendwa wao, lakini sisi kama mamlaka na taifa kwa ujumla tumempoteza mtu muhimu sana aliyekuwa mchapakazi, tutamkumbuka sana marehemu,” alisema Bw. Hanga.

Marehemu ambaye ameacha mume Bw. Alex Temba na watoto wawili, Faith (9) na Harieth (4) alihamishiwa TAA tarehe 01/04/2016 akitokea Halmashauri ya Manispaa ya mji wa Songea alipokuwa akifanya kazi kama mwanasheria kuanzia mwaka 2012.
Bw. Alex Temba (wa pili kushoto), mume wa marehemu aliyekuwa Mwanasheria wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kituo cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bi. Delfine Mulogo akiwa na binti yake Faith Temba (mwenye gauni jeupe) wakitoa heshima za mwisho katika kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Augustine lililopo Mbezi Temboni kabla ya kusafirishwa kwa mazishi katika Kijiji cha Uru Kishumundu mkoani Kilimanjaro. 
Naye Mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS), Bw. Stephen Msechu alisema marehemu alikuwa mwanachama tangu alipoapishwa kuwa Wakili mwaka 2012 na kupewa namba ya uanachama 3361 na amekuwa akishirikiana nao katika shughuli mbalimbali kwa uadilifu mkubwa.

Hata hivyo, Paroko wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Augustine lililopo Mbezi Temboni, Padri Fidelis Mfaranyembo aliwataka waombolezaji waliofika kuuaga mwili wa marehemu  Delfine kujiandaa wakati wote kwa kuwa hawajui siku wala saa watakayotwaliwa.

Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Lawrence Thobias akitoa heshima zake kwa mwili wa aliyekuwa Mwanasheria Kituo cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bi. Delfine Mulogo aliyefariki Desemba 25. Marehemu atazikwa Kijiji cha Uru Kishumundu mkoani Kilimanjaro.
Padri Mfaranyembo alisema pia waombolezaji wahakikishe wanakuwa watu wa sala wakati wote ili kumuombea marehemu aweze kupokelewa na aingie katika ufalme wa mbinguni, kwani ufalme huo upo kwa kuwa kunamaisha baada ya kifo.

“Kuna mwanafalsafa mmoja wa zamani, Plato alitafakari  sana kuwa mwanadamu akifa anakwenda wapi? na akaona kila mwanadamu anabeba roho ya muumbaji  na hivyo unapokufa roho inarudi kwa yule aliyeiumba, "alisema na kuongeza:

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Bi. Agnes Kijazi akimpa pole Bw. Alex Temba kufuatia kifo cha Mkewe Bi. Delfine Mulogo aliyekuwa Mwanasheria kwenye Kituo cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) aliyefariki Desemba 25 na atazikwa Kijiji cha Uru Kishumundu mkoani Kilimanjaro.
" Plato anatufundisha ya kwamba mwisho wa maisha yake hapa duniani Mwanadamu anarudi kwa Mungu wake kulingana na namna alivyokuwa akiishi na wengine hapa duniani,” alisema Padri Mfaranyembo.

Pia amemtaka mume wa marehemu Bw. Temba asifadhaike kwa kuondokewa na mkewe, bali ajikabidhi kwa Mungu kwa kumuomba hakika atamsaidia kwa kumtia nguvu na kumpa uwezo wa kuendelea kuwahudumia watoto wake kwa kadri ya uweza wake Mungu.

Wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) wakijumuika na waombolezaji wengine katika misa ya kumwombea marehemu Bi. Delfine Mulogo aliyekuwa Mwanasheria kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).
Marehemu alipata elimu ya msingi katika shule ya Oysterbay (1991), baadaye sekondari ya St. Mathew (1998), na baadaye elimu ya Kidato cha Tano na Sita katika shule ya Wasichana ya Kibosho (2004), na mwaka 2008 alihitimu Shahada ya Kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu cha Tumaini.     
Mweka Hazina wa Klabu ya Uchukuzi, Bw. Benjamin Bikulamchi (kulia), akimkabidhi rambirambi aliyewahi kuwa Katibu wa Klabu hiyo, Bw. Alex Temba aliyefiwa na mkewe Bi. Delfine Mulogo aliyekuwa Mwanasheria Kituo cha Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).
Viongozi wa Shirikisho la Michezo la Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI), Bi. Itika Mwankenja na Bi. Joyce Benjamin wakitoa rambirambi zao kwa Katibu Msaidizi wa shirikisho hilo Bw. Alex Temba (kushoto) aliyefiwa na Mkewe Bi. Delfine Mulogo wakati wa misa ya kumwombea marehemu iliyofanyika jana katika Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Augustine lililopo Mbezi Temboni.
Bwana Ametoa na Bwana Ametwaa Jina Lake Lihimidiwe.  Amina.

No comments:

Post a Comment