Monday 25 December 2017

Mkombozi arudi SHIMIWI kwa kishindo

Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja (kulia) akimpongeza Alex Temba mara baada ya uchaguzi wa Shirikisho la Michezo la Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI), uliofanyika hivi karibuni kwenye hoteli ya Mount Uluguru mkoani Morogoro.
 Na Mwandishi Wetu

MWEKA Hazina, William Mkombozi ‘Mgosi’ amerudi kwa kishindo katika nafasi hiyo baada ya kushinda kwenye uchaguzi wa Shirikisho la Michezo kwa Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI), uliofanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa hoteli ya Mount Uluguru mkoani Morogoro.

Mkombozi aliyewahi kuongoza katika miaka ya mwanzoni ya 2000 akiwa na aliyewahi kuwa mjumbe na baadaye Katibu Mkuu, Bw. Ramadhani Sululu, lakini baadaye alikaa pembeni sasa amechaguliwa tena kwa kura 23.

Naye Alex Temba aliyeongoza kwa muda mrefu katika Klabu yenye wachezaji mahiri ya Uchukuzi, alichaguliwa kuwa Katibu Msaidizi baada ya kushinda kwa kura 28 na kumbwaga Margreth Mtaki aliyepata kura 15.

Hatahivyo, nafasi ya Mwenyekiti ilirudi tena kwa Daniel Mwalusamba aliyekuwa hana mpinzani kwa kupata kura 42;  huku Ally Katembo akichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti kwa kura 41; wakati Moshi Makuka ametetea nafasi yake ya Ukatibu kwa kura 38 dhidi ya Andrew Sekimweri aliyeondoka na kura sita.

Katika nafasi ya Mweka Hazina Msaidizi, ameshinda Frank Kibona kwa kura 21; wakati walioshinda kwenye ujumbe wa kamati ya utendaji na kura zao zikiwa kwenye mabano ni Apolo Kayungi (44), Assumpta Mwilanga (42), Aloyce Ngonyani (40), Damiani Manembe (39)  na Seleman Kifyoga (31).

Kwa upande wa nafasi ya viti maalum wanawake walioshinda ni Mwajuma Kisengo (20) na Mariam Kihange (18) na waliwashindwa ni Costance Momadi (16) na Buya Masunga (12).


Michezo ya SHIMIWI inayoshirikisha wafanyakazi wa mashirika ya umma imepoteza mvuto kwa kutofanyika takribani miaka miwili mfululizo kutokana na sababu mbalimbali zilizokuwa zikielezwa na uongozi wa juu.

Hatahivyo, kutofanyika kwa michezo hiyo kumewanyima haki watumishi wa umma kushindwa kujenga afya zao na kudumisha umoja na urafiki ikiwa ni pamoja na kukutana na watumishi wengine mbalimbali wa Idara na Wizara nyingine wakati wa michezo hiyo.

Mbali na kutofanyika kwa michezo hiyo pia kumekuwa hakuna mabonanza ya kushirikisha idara za serikali na wizara kwa muda mrefu, ambapo tayari Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan ameagiza kufanyika kwa mazoezi ya viungo angalau mara moja kila mwezi ili kujenga afya kwa watumishi wa umma.


 

No comments:

Post a Comment