Tuesday 11 August 2015

Mkuu wa mkoa wa pwani alivyofungua mafunzo ya ufundishaji mchezo wa mieleka


Washiriki wa mafunzo ya ufundishaji mchezo wa mieleka wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo (wa tatu kutoka kushoto waliokaa), baada ya kufungua mafunzo hayo yanayoendelea katika shule za Filbert Bayi Mkuza Kibaha mkoani Pwani.

 
  RISALA FUPI YA KAMATI YA OLIMPIKI TANZANIA WAKATI WA UFUNGUZI



Mhe. Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Pwani.

Mtaalamu wa Mafunzo-Ndugu Tuma.

Waratibu wa Mafunzo, TOC na AWATA,

Washiriki wa Mafunzo,

Waandishi wa Vyombo vya Habari-Michezo

Mabibi na Mabwana.

Kwa niaba ya Kamati ya Olimpiki Tanzania na kwa niaba yangu napenda kuupongeza uongozi wa Chama cha Mieleka Tanzania (AWATA) kwa kufanikisha mafunzo haya kuanza kwa muda uliopangwa hali kadhalika  kufanikisha kwa ushirikiano na Shirikisho la Mieleka la Dunia (UWW) kuwateua Wakufunzi wawili (2) Ndugu Pino Massidda (Ufaransa) na Eric Ciacke (Cameroon)  ambaye atafika hapa tarehe 12/08/2015.

Mtaalamu Pino Massidda siyo mgeni sana katika Bara la Afrika, amewahi kufundisha mafunzo kama haya katika nchi za Afrika ya Magharibi  hasa zinazozungumza lugha ya Kifaransa kama Togo, Senegal, Ivory Coast n.k.

Chama cha Mieleka Tanzania (AWATA) wakati huo ikishirikiana na Chama cha Mieleka cha Zanzibar (AWAZA) kwa mara ya mwisho nakumbuka walipata mafunzo kama haya mwaka 2005 ambayo yalifanyika mjini Morogoro  kwa kushirikisha walimu 30 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar. 

Ni matumaini ya Kamati ya Olimpiki Tanzania na Shirikisho la Mieleka la Kimataifa (UWW)  walimu hao baada ya kufuzu mwaka 2005 bado wanaendelea na fani ya ufundishaji katika Mikoa yao.

Siku za karibuni mchezo wa mieleka umekuwa hausikiki sana. Taarifa nilizozipata ni kwamba viongozi waliotangulia kabla ya huuambao uko madarakani waliutelekeza mcezo wa mieleka mpaka ukakosa mwelekeo.  Kamati ya Olimpiki Tanzania kwa kuthamini mwelekeo mzuri wa viongozi walio madarakani  imeona haina budi kuwapatia mafunzo haya ya daraja la 1 ili wapatikane walimu wengi watakafundisha mieleka na kufikia hatua ya kutuwakilisha Kimataifa.
Ndugu Mgeni Rasmi, mafunzo yanayogharimiwa na Olimpiki Solidariti kupitia Kamati ya Olimpiki Tanzania ni ya gharama sana, nashauri washiriki watakapomaliza mafunzo haya yanayoanza muda mfupi ujao wawe na chachu ya kuuendeleza mchezo wa Mieleka katika vilabu na mikoa yao wanayotoka.

Sina shaka AWATA tayari ina mipango mahsusi kwa vijana hasa kwenye ngazi za shule. Ni wakati muafaka sasa AWATA ikawa na wanamichezo wadogo katika ngazi mbalimbali kwa kufuata umri (chini ya miaka 15, 17, 20). Wanamichezo hao wakiandaliwa vizuri nina uhakika watafanya vizuri katika siku za usoni.

Nawapongeza walimu washiriki katika mafunzo haya. Ni matumaini yangu wote mliofanikiwa kuja hapa mmechaguliwa kwa chama kuwathamini na watawategemea sana baada ya kumaliza mafunzo. Ninawaomba muitendee haki nafasi hiI mliyopewa ya kuja hapa kuongeza ufahamu zaidi katika masuala ya kufundisha  mieleka pamoja na kwamba wengi wenu bado mnacheza. Baada ya kuhitimu hapa na kila mmoja wenu akawa na timu yake ya vijana, basi muda si mrefu tutakuwa na wachezi wengi.

Walimu tusitosheke na hapa tutakapofikia, tujiendeleze zaidi kwani mambo mengi kuhusu ufundishaji mieleka yanabadilika siku hadi hadi. Nina matumaini makubwa kwamba kuna siku mieleka itatuwakilisha katika mashindano ya Kimataifa.
Chama cha Mieleka Tanzania irudi kwenye njia yake baada ya kukosa mwelekeo kwa kuanza  na kuandaa mashindano ya Vilabu na Taifa. Ni muda mrefu mashabiki wenu wamekosa uhondo wa kuona mchezo wa mieleka.
 
Ninawaomba viongozi wa AWATA kwa kushirikiana na baadhi ya wachezaji wa zamani wa AWAZA kufufua mchezo huu huko Zanzibar na Pemba kwani ulishakufa na kutolewa katika orodha ya vyama wanachama wa Kaamati ya Olimpiki Tanzania baada ya kutokuwa hai kwa muda mrefu.

 Mwisho, ninaomba AWATA kuwawekea mazingira mazuri walimu hawa kwa kuwatumia  katika mipango ya kuendeleza mchezo wa mieleka  katika
 ngazi mbalimbali nchini mwetu.

Ninaomba sasa nimkaribishe mgeni rasmi aseme machache na atufungulie mafunzo haya, Karibu Mgeni Rasmi.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.


RISALA YA MGENI RASMI WAKATI WA UFUNGUZI WA MAFUNZO YA WALIMU WA MA MCHEZO WA MIELEKA, MKUZA,  KIBAHA
10 AGUSTI, 2015.

Ndugu Filbert Bayi, Meja Mstaafu na Katibu Mkuu, Kamati ya Olimpiki Tanzania,

Rais Chama cha Mieleka Tanzania,

Katibu Mkuu, Chama cha Mieleka Tanzania

Waratibu wa Utawala (TOC) na Ufundi AWATA)

Wakufunzi wa Mafunzo Pino Massidda (France) na Eric Ciake, (Camerou)

Viongozi wa Mpira wa Wavu Mkoa wa Tanga,

Walimu Washiriki wa Mafunzo,

Wageni Waalikwa,

Mabibi na Mabwana.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo.
 Awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Kamati ya Olimpiki Tanzania kwa kunialika kuja kufungua  mafunzo haya ya aina yake kufanyika kwa mara ya kwanza hapa Kibaha, Mkoa wa Pwani. Nimefahamishwa haya ni mafunzo ya pili kufanyika kwa ufadhili wa Olimpiki Solidariti na kuandaliwa kwa pamoja TOC na AWATA.

Nami kama Kiongozi wa Serikali katika Mkoa huu  nawakaribisha katika manispaa yetu. Ni matumaini yangu kwa wanaotoka nje ya Mkoa wa Pwani, wenyeji wenu wamewakaribisha katika Mkoa wetu.

 Aidha pia niwapongeze TOC  kuitikia ushauri wa Viongozi mbalimbali wa Serikali ya Muungano la kutaka viongozi wa vyama na mashirikisho ya michezo kuendeleza michezo katika Taifa letu ili kufikia viwango vya Kimataifa. Nami kama Kiongozi wa Serikali katika Mkoa huu wa Pwani nawaunga mkono hao viongozi na wapenzi wenye kiu ya maendeleo ya michezo. Tuwape elimu walimu ambao watakuwa na uwezo wa kuwaandaa wachezaji katika ngazi ya Kimataifa.
 
Lengo hili halitafanikiwa kama hatutakuwa na walimu wenye taaluma ya kuwandaa wanamichezo kufikia azma hiyo.

Kamati ya Olimpiki Tanzania na Chama cha Mieleka Tanzania hawakufanya kosa kuchagua Mkoa wa Pwani hususani Kibaha kuwa mwenyeji wa Mafunzo haya muhimu. Wananchi wa Pwani ni wakarimu na wapenda michezo ya aina mbalimbali. Nawashukuru wote kwa kutupa heshima hii ya kuwa mwenyeji.

Ni heshima kubwa kukutana na walimu mbalimbali kutoka Mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar, hali kadhalika na Wataalamu wa Shirikisho la Kimataifa la Mieleka (FILA) Nugu Pino Massidda (France) na Eric Ciake (Cameroun).

Nawapongeza walimu washiriki katika mafunzo haya. Ni matumaini yangu wote mliofanikiwa kuja hapa mmechaguliwa kutokana na uwezo wenu katika ufahamu wa mchezo wa Mieleka katika Mikoa yenu, kwa hiyo jitihada za ziada zinahitajika ili muweze kuongeza ufahamu zaidi kutoka kwa wataalamu hawa wa Kimataifa ili baada ya mafunzo haya muwe tofauti na mlivyoanza.
 
Ikiwa nchi yetu itakuwa na walimu wengi wa mchezo wa Mieleka, na wakatawanywa kwenye shule zetu ambapo ndiyo kwenye vipaji, basi miaka 5 ijayo tunaweza kuwa na uwakilishi mzuri katika Michezo ya Kimataifa, lakini ikiwa walimu hawa watabaki kwenye vilabu vya taasisi za Serikali (JWTZ, Polisi, Magereza, Jeshi la Kujenga Taifa, Jeshi la kujenga Uchumi nk.) ambazo nyingi ziko katika miji yetu mikuu basi tutabaki pale pale tukitafuta mchawi  wa maendeleo ya mchezo wa mieleka. AWATA na AWAZA lazima wawe na mipango mahususi ya kuendeleza vijana wa umri mbalimbali kuanzia kwenye shule zetu.

Serikali yetu ni sikifu, mmeona wenyewe jinsi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete alivyo mstari wa mbele kuendeleza michezo hasa kwa kuwalipa walimu wa nje wenye uwezo mkubwa kufundisha timu zetu za Taifa. Mhe. Rais alianza kwenye Mpira wa Miguu, kila moja wetu anafahamu alipomleta Maximo (Brazil) kufundisha timu yetu ya mpira wa miguu (Taifa Stars), Simmons McKinns (Australia) kufundisha timu ya Netiboli (Taifa Queens) na kutoa nafasi kwa Riadha Tanzania kumpata mwalimu kutoka nje, lakini mpaka leo wamekuwa kimya bila kutekeleza ahadi aliyotoa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Tanzania. Yote hayo ikiwa ni mchango wa Rais wetu.

Kwa hiyo AWATA/AWAZA na walimu washiriki mnaohudhuria mafunzo haya kazi kwenu, elimu mtakayopata iwe changamoto ya kunyanyua mchezo wa mieleka ili utupeleke kwenye ushiriki wa Kimataifa na kutupatia heshima ambayo ndiyo kiu wa Watanzania.
 
Mwisho napenda kuwashukuru Olimpiki Solidariti kwa kudhamini mafunzo haya, Shirikisho la Mchezo wa Mieleka la Kimataifa (UWW) kuwaleta Wakufunzi wa Kimataifa, Kamati ya Olimpiki Tanzania kwa ushirikiano na AWATA/AWAZA kuamua na kuandaa mafunzo haya kufanyika katika Mkoa wetu wa Pwani, washiriki kwa kuhudhuria, kwani bila wao tusingekuwa hapa leo.

Kwa haya machache, sasa natamka kwamba Mafunzo ya Walimu wa Mchezo wa Mieleka nimeyafungua rasmi.

  Ahsanteni kwa kunisikiliza.
 


 

No comments:

Post a Comment