Tuesday 4 August 2015

Mahafali ya Shule ya awali Joyland yalivyofana Kigamboni



 

Na Mwandishi Wetu

WAZAZI wamehimizwa kujenga utamaduni wa kupitia kazi na watoto wao wanaporudi shuleni kwa lengo la kusaidia ufahamu wao na kuwarahisishia kazi walimu katika suala la taaluma.

Pia wamekumbushwa kufuatilia nyendo za watoto wao kujua wanacheza wapi, na akina nani na rafiki gani wanaokuwa nao kwa muda mrefu sambamba na kutowaachia kutumia muda mrefu kwenye runinga kwani ni moja ya sababu ya kuharibika kwao na kuporomoka kimasomo wawapo likizoni.

Wito huo ulitolewa na Mkurugenzi wa Shule ya Kimataifa ya Joyland, Fredrick Otieno wakati wa mahafali ya wanafunzi wa masomo ya awali wa shule hiyo yaliyofanyika mwishoni mwa wiki shuleni hapo, Tua Ngoma, Kigamboni, jijini Dar es Salaam.

Otieno alisema ushirikiano wa wazazi na walimu katika malezi ya watoto ni msaada mkubwa wa wanafunzi, lakini kama wazazi na walezi wataliacha jukumu hilo kwa walimu tu ni mtihani mkubwa na kuchangia kuporomoka kwa kiwango cha elimu nchini. Alisema ni lazima wazazi na walezi wakague madaftari na kazi za watoto wao wawapo majumbani na pia kuwazuia kuingia katika makundi au kuumia muda mrefu kucheza wakati wa likizo ili viwango vyao kitaaluma visiporomoke.

Pia aliwakumbusha wazazi na walezi kujenga tabia ya kuwalipa ada watoto wao ili kurahisisha kazi kwa shule wanazosoma kuwa kile kinachostahiki, alisema kucheleweshwa kwa ada ni tatizo ambalo linapunguza morali wa kazi kwa walimu, ingawa alisema Joyland imekuwa ikijitahidi kuhakikisha wanafunzi wanakipata kile kilichowapeleka wakati wazazi na walezi wakikumbushwa wajibu wao wa kuwalipia ada.

Mkurugenzi huyo alisisitiza kuwa hakuna hazina bora kama mtoto kupewa elimu ambayo huja kumsaidia ukubwani kwa kuzingatia kuwa dunia ya sasa inaendeshwa kisasa na bila elimu bora na ya kutosha ni vigumu kijana kusimama na kukabiliana na changamoto hizo.



Naye Mkaguzi Mkuu wa Elimu Kanda, Shani Kanungira aliwasisitiza wazazi kutumia kujitolea na kutimiza wajibu wao kuwasomesha watoto badala ya kutumia fedha nyingi kwa mambo yasiyo na tija kwa watoto na familia zao kwa ujumla.

Shani alitoa nasaha yake kabla ya kumpisha Mwakilishi wa Ofisa Elimu ya Msingi Manispaa ya Temeke, Frank Makingi aliyesisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kujenga utamaduni wa ushirikiano dhidi ya walimu wa shule wanazosoma watoto wao.

Makingi alisema siyo kila jambo la wanafunzi kuachwa mikononi mwa walimu tu, kadhalika alikumbusha kuwasaidia watoto katika kuwalea katika maadili mema ili kulifanya taifa kuwa na raia wema na viongozi wazuri na waadilifu wa baadaye.

 

No comments:

Post a Comment