Sunday 23 August 2015

CCM wazindua kampeni zao, Magufuli ahadi maendeleo ya ukweli



Na Waandishi Wetu

DK. John Pombe Magufuli (pichani), mgombea wa Urais wa Chama cha Mapinduzi (CCM), amezindua kampeni zake za kuwania nafasi hiyo ya uongozi katika viwanja vya Jangwani jijiniDar es Salaam.

Maguuli aliuambia umati mkubwa wa watu uliojitokeza kumsikiliza, ambapo alisema kuwa ameomba kibarua hicho cha kuiongoza Tanzania kwa ajili ya kuleta mabadiliko ya kweli kwa umma.
 
Kwa hali hiyo  amewaomba Watanzania waichague CCM na waache jazba ya kukiua chama hicho kwani yeye pamoja na mgombea wake mwenza wamedhamiria kuleta mabadiliko ya kweli kwani wanatambua kuwa wananchi wanataka mabadiliko yenye kuwaleta maisha mazuri.

"Natambua kuwa Watanzania mnataka maisha mazuri, naahidi kukomesha wizi na rushwa haraka kwa sababu palipo na rushwa hakuna maendeleo," alisema Dk John Magufuli.

Aliahidi kushughulikia kero za wakulima ambao alisema wanataka wapate pembejeo na mbegu bora kwa bei nzuri pamoja na uhakika wa soko la mazao yao. Alisema akichaguliwa itakuwa mwisho wa mkulima kuikopesha Serikali. Mgombea huyo alihoji inakuwaje mkulima anaikopeshe serikali badala ya Serikali kumkopesha mkulima.

Aliahidi kujenga umoja wa kitaifa kwani taifa mabalo halina umoja haliwezi kujiletea maendeleo, kwa hali hiyo akasema ataendelea kupiga vita ukabila, ukanda na udini kwani ndio utanzania mbao amepanga kuujenga akiwa Rais.

Aliahidi kulinda muungano na kurekebisha dosari ndogondogo, lakini zaidi alisema serikali yake itaendeshwa kwa kuheshimu mipaka ya mihimili ya dola. Alisema angependa awe na Bunge ambalo litaisimamia vizuri Serikali na akatoa mwito kwa wananchi kuchagua Wabunge wengi wa CCM ili wawe wakali kwa serikali yake.

Aliahidi kuunda mahakama itakayoshughulikia kesi za rushwa na ufisadi. "Nitabanana nao polepole ili wananchi waweze kupata haki zao kwani vitendo vya ufisadi ndivyo vilivyoifikisha hapa nchi ilipo.

Mgombea huyo wa CCM aliahidi kuheshimu utawala bora, pia alisema serikali yake itaheshimu  mawazo mazuri yatakayotolewa na vyama vingine vya siasa ambayo mwelekeo wake ni kulijenga taifa.

"Nasema hivyo maana mimi naamini kwamba maendeleo hayana vyama, ninachotaka mimi ni kazi tu ili maendeleo yaweza kusonga mbele," alisema.

Pia aliahidi kuimarisha vyombo vya ulinzi na usalama hasa jeshi la polisi kwa kulipatia vifaa vya kisasa. Alisema ni aibu kwa askari polisi kuvamiwa na majambazi akapigwa hadi akanyang'anywa silaha hivyo akasema serikali yake itataka kuona askari hao wanakuwa na vifaa vya kisasa lakini pia wanaishi kwenye nyumba bora zaidi.

AJIRA:
Kuhusu ajira Dk  Magufuli alisema serikali yake itaongeza ajira kwa vijana ana akasema njia pekee ya kufikia malengo hayo ni kujenga viwanda vingi ambavyo vitasaidia kulimaliza tatizo hilo. Alisema miongoni mwa viwanda atakavyojenga kwa kushirikiana na sekta binafsi ni viwanda vya kuchakata samaki.

"Samaki ambao kwa sasa tunaibiwa huko baharini na wanapelekwa nje, sasa watatengenezewa hapa hapa na hilo linawezekana maana tutalifanya kwa kuleta wawekezaji kutoka nje bila kuwepo urasimu. Maafisa serikalini ambao wamezoea urasimu wa njoo kesho ambayo inakwamisha uwekezaji, nawaambia watafute sehemu nyingine ya kuishi."

Katika eneo hilo la viwanda, Dk Magufuli alisisitiza kuwa hakuna haja ya kuuza marobota ya pamba nje ya nchi; badala yake dawa ni kujenga viwanda vya kutengeneza khanga na vitenge. "Badala ya kuuza nanasi zima kutoka Msoga kwa mheshimiwa Rais Kikwete (Jakaya) sasa tutauza juisi hapa hapa nchini."

Alisema iwapo Serikali itajenga viwanda vingi, ajira itaongezeka kwa asilimia 40. Alisema viwanda vingine ambavyo vitajengwa viwanda vya nyama na maziwa kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji ambao kwa sasa wahamahama na mifugo yao.

"Haya ndio maendeleo ninayoyataka," alisema Dk Magufuli ambaye alitumia saa moja jana kujinadi wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama hicho ambao ulihudhuriwa na maelfu ya watu katika viwanja vya Jangwani, Dar es Salaam.

MADINI:
Alisema licha ya juhudi zinazofanywa na Serikali za kuwasaidia wachimbaji wadogo, lakini yeye akiingia madarakani anatahakikisha kundi hilo linaboreshewa mahitaji yake zaidi ili waweze kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi.

Pia aliahidi kupunguza tatizo la utoroshaji wa madini nje ya nchi na akaoa mfano kuwa inakuwaje Tanzania ambayo inachimbwa Tanzania pekee leo hii nchi ya kwanza kuuza madini hayo ni India na kufuatiwa na Kenya na Tanzania inashika nafasi ya tatu "Hili nitaliangalia kwa kina."

MAJI, AFYA NA ELIMU:
Alisema Serikal iyake itahakikisha asilimia 87 ya Watanzania walioko vijijini wanapata maji safi na salama na asilimia 95 ya wakazi wa mijini watapata huduma hiyo. Alisema ili kupunguza kero kwa akina mama, watajitahidi huduma hiyo inapatikana karibu na yalipo makazi ya watu.

Alisema pia watajenga zahanati kila kijiji na vituo vya afya kila kata ili kuhakikisha kuwa watanzania wanapata huduma za afya kwa ufanisi.

Kwa upande wa elimu, alisema watahakikisha wanafunzi wanasoma bure kuanzia shule ya msingi hadi kidato na nne. Alisema fedha za kutekeleza mpango huo zitapatikana tu pale atakapobana mianya ya rushwa na ufisaidi serikalini.

Pia aliahidi kujenga nyumba za walimu kwa wingi ili waweze kupata sehemu nzuri ya kukaa pamoja na kuendeleza juhudi za kujenga mabweni katika shule mbalimbali ili kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu katika mazingira mazuri.

 Kwa pande wa wanafunzi wanaosoma vyuo vya elimu ya juu, alisema atakachofanya ni kuhakikisha kuwa wanapatiwa mikopo yao kwa wakati na sio kucheleweshewa.

"Inakuwaje mkopo unacheleweshewa mtu wakati ni mkopo, inakuwaje mwanachuo kupatiwa mkopo hadi agome kwanza? Alihoji mgombea huyo na kusema kuwa atahakikisha mwanafunzi akienda chuo anapatiwa mkopo wake kwa wakati na kazi yake itakuwa ni kusoma peke yake na sio kufuatilia masuala ya fedha.

MIUNDOMBINU:
Dk Magufuli alisema kazi ya kwanza atakayoifanya ni kuhakikisha wanaunganisha makao makuu ya mikoa yawe na barabara ya lami na baadaye wataenda kuunganisha na wilaya zote.

Alisema pia watajenga barabara ya kisasa ya njia sita kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze  ambayo itakuwa na barabara za ghorofa zipatazo saba. Alisema pia kuwa ujenzi wa barabara ya ghorofa katika makutano ya Tazara karibu utaanza kwani kampuni ya kijapani tayari imeshaanza kufanya kazi hiyo

Alisema atajenga reli na kuboresha bandari ili kuhakikisha uchumi wa nchi unaimarika zaidi kwani anaamini kuwa miundombinu hiyo ndio njia pekee ya kuboresha uchumi wa nchi. Alisema katika kukamilisha mambo hayo, serikali yake itakuwa rafiki wa wawekezaji na wafanyabiashara.

WAANDISHI NA WASANII:
Maslahi ya wafanyakazi, vyombo vya habari, wasanii
Maslahi ya Wafanyakazi, Dk Magufuli alisema atapenda kuona walimu wanakuwa na maslahi mazuri pamoja na wafanyakazi wengine. Alisema ataboreha maslahi yao ili wasiwe wanaingia ofisini saa nne na kutoka saa tano asubuhi.

Alisema ataboresha maslahi ya kada hiyo ili wafanye kazi kuanzia asubuhi hadi jioni na watoke na mishahara mizuri.

Pia aliahidi kulienda uhuru wa habari ili waandishi wa habari waendelee kufanya kazi zao katika mazingira mazuri. Alisema angependa kuona waandishi wa habari wanakuwa na chombo chao za kutetea maslahi yao ili atakapochaguliwa tu ahakikishe anakutana na chombo hicho kuangalia namna ya kuboresha maslahi ya wanahabari.

Aliahidi pia kuanzisha mfuko wa wasanii pamoja na wanamichezo ili waweze kunufaika na kazi zao "Nawaahidi kuwa sitawatumia kwenye siasa tu bali pia nitaangalia maslahi yenu."

1 comment:

  1. hodi ni wewe katika haraka haja mkopo kulipia kuanza yako madeni ya kuanzisha biashara au nyumba ??? Kisha inakuja teksi kampuni una imani na relay juu ya 100% uhakika sababu hii ni kampuni ambapo i cashed mkopo wangu kwa mama yangu Stella dawa leo ili kuwasiliana na René Mikopo Firm halisi kupimwa na kuaminiwa na leo mimi nina furaha i got mkopo wangu wa $ 120,000 leo ili kupata kushikamana leo mrsstellareneloanfirm@hotmail.com} {barua pepe hapa chini na kupata jibu la matatizo yako yote kwa sababu Siwezi Kunyamaza ushuhuda huu mkubwa peke yangu binafsi ili i aliamua kuandika kwenye tovuti kwa sababu kula furaha kubwa kwa yangu moyo na leo mimi nina kuishi maisha mapya shukrani kwa wote Stella René


    kolochatechee

    ReplyDelete