Sunday 30 October 2016

TP mazembe yakaribia taji la Shirikisho la Afrika baada ya kuilazimisha sare Mo Bejaia


Mchezaji wa Bejaia, Issama Mpeko (kushoto) akigombea mpira na mchezaji wa TP Mazembe, Mohamed Yacine Atmani wakati wa mchezo wa kwanza wa fainali wa mashindano ya Kombe la Shirikisho kwenye Uwanja wa Stade Mustapfa Tchacher, Blida, Algeria. Timu hizo zilifungana 1-1.

ALGIERS, Algeria
TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imejiweka katika nafasi nzuri ya kutwaa taji la Shirikisho la Afrika baada ya kutoka sare dhidi ya Mouloundia Olympique de Bejaia katika mchezo wa kwanza wa fainali uliofanyika mjini hapa.

Mabingwa hao wazamani wa Ligi ya Mabingwa wa Afrika wamejiweka katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa huo wa Shirikisho kufuatia sare hiyo katika mchezo uliofanyika kwenye Uwanja wa Stade Mustapha Tchaker El Bouleïda mjini Blida juzi usiku.

Mabao hayo yalifungwa katika kila kipindi kupitia kwa Jonathan Bolingi na Faouzi Yaya yaliviwezesha vigogo hivyo kila mmoja kuondoka na pointi moja.

Kwa sare hiyo, TP Mazembe inahitaji suluhu au ushindi wa aina yoyote ili kutangaza ubingwa wa mashindano hayo ya Afrika.

Yacine Athmani nusura afunge bao mwanzoni mwa mchezo huo baada ya kupiga shuti la mbali, lakini lilikwenda moja kwa moja mikononi mwa kipa Sylvain Gbohouo katika dakika tatu tangu kuanza kwa mchezo huo.

Ingawa timu zote zilijaribu kuzifumania nyavu ndani ya dakika 30, lakini walikuwa wageni Mazembe ndio waliweka presha kwa wenyeji wao Mo Bejaia.

Zikiwa zimebaki dakika mbili kabla ya mchezo kuwa mapumziko, wageni walifanikiwa kufunga bao lao la kwanza kupitia kwa Bolingi kwa penalti. Hadi kipindi cha kwanza kinamalizka, ubao ulionesha 1-0 kikosi cha Hubert Velud kikiongoza.

Hatahivyo, baada ya kurejea uwanjani, nahodha wa Bejaia, Yaya aliwafungia bao wenyeji la kusawazisha katika dakika ya 66.

Mchezo wa Marudiano umepangwa kupigwa Jumapili Novemba 6 kwenye Uwanja wa Stade du TP Mazembe jijini Lubumbashi ili kumpata bingwa.

Mazembe iliwahi kuifunga Bejaia mara moja nyumbani mwaka huu, 1-0 katika hatua ya makundi, huku mchezo uliopita uliofanyika Algeria ulimalika kwa suluhu.

Mazembe imeshinda mara tisa taji la Ligi ya Mabingwa wa Afrika lakini haijawahi kushinda taji la Shirikisho, ambapo mshindi ataondokana kitita cha dola za Marekani 660,000 (sawa na sh bil 1.4) huku mshindi wa pili ataondoka na dola 462,000 (sh bil 1).

Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini ambao ni mabingwa wapya wa Ligi ya Mabingwa wa Afrika wenyewe mbali na fedha taslimu pia watawakilisha bara la Afrika katika mashindano ya Klabu Bingwa ya Dunia.

No comments:

Post a Comment