Sunday 9 October 2016

Kifimbo cha Malkia kutua Bongo Aprili 8 maandalizi ya kukipokea kuanza mwezi ujao jijini Dar



Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete na Katibu Mkuu wa TOC, Filbert Bayi wakiwa na Kifimbo cha Malkia wakati kilipotua Ikulu jijini Dar es Salaam mwaka juzi.
Na Mwandishi Wetu
KIFIMBO cha Malkia wa Uingereza kinatarajia kuwasili nchini Aprili 8 mwakani ikiwa ni maandalizi ya Michezo ya 21 ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika Gold Coast, Australia 2018 kuanzia Aprili 4 hadi 15.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Tanzania ni miongoni mwa nchi zitakazopitiwa na mbio hizo za kifimbo cha Malkia, ambacho hupokewa na mkuu wa nchi.

Bayi alisema kuwa maandalizi ya kupokea kifimbo hicho yataanza mwezi ujao wakati TOC itakapokutana na wadau mbalimbali ili kuteua kamati maalum ya itakayoratibu ujio wa kifimbo hicho.

Aliwataja baadhi ya wadau hao kuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Kamanda wa Polisi wa mkoa, ofisi ya Mambo ya Nje na wengine wengi.

Alisema kuwa wanasaka wadhamini ili kufanikisha ujio wa kifimbo hicho, ambapo zinahitajika zaidi ya sh milioni 60 wakati wenyeji Australia wameipatia TOC kiasi cha dola z Marekani 3,000 tu, ambazo ni sawa na sh. Milioni 6.

Bayi alisema kuwa wadhamini hao wanatarajia kuwa ubalozi wa Uingereza, Kampuni ya vinywaji ya Peps Cola ambayo mara ya mwisho kilipokuja kifimbo hicho walisaidia sana, Acacia na ITV, Azam TV na vyombo vingine vya habari.

Alisema kuwa wadhamini wakubwa ni pamoja na British Council, Ubalozi wa Uingereza, Peps na Shirika la Kimataifa la Watoto Duniani, Unicef.

Mwaka 2014 Kifimbo cha Malkia kilitua nchini na kukimbizwa katika barabara mbalimbali za jijini Dar es Salaam kabla ya kutua Ikulu, ambako kilipokewa na Rais wa Awamu ya Nne Jakaya Mrisho Kikwete na baadae kuzungumza na wana michezo.

Kifimbo hicho kilikuwa maalum kwa ajili ya Michezo ya Jumuiya ya Madola iliyofanyika Glasgow, Scoland


Michezo hiyo itafanyikia katika jiji la Gold Coast City, lililopo kusini ya Jimbo la Australia la Queensland, ambapo hii itakuwa ni mara ya tano kwa Australia kuandaa, ambapo pia iliwahi kuandaa mwaka 1938 Sydney, 1962 Perth, 1982 Brisbane na mwaka 2006 Melbourne.





No comments:

Post a Comment