Saturday 25 August 2018

Uchukuzi watakiwa Kulinda Mataji, Kutwaa Zaidi




Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Dk Leonard Chamuriho (kushoto) akipokewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari katika viwanja vya TCAA, ambako bonanza hilo lilifanyikia. 

Na Mwandishi Wetu
KLABU ya Michezo ya Uchukuzi (USC) imetakiwa kubakisha na kuongeza mataji iliyopata katika mashindano yaliyopita ya Mei Mosi na kutwaa ushindi wa jumla baada ya kujikusanyia vikombe 13.

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Dk Leonard Chamuriho wakati akifungua bonanza la kwanza la Sekta ya Uchukuzi lililofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Ukonga Banana Jijini Dar es Salaam.
Chamuriho kwanza aliipongeza USC kwa kutwaa ushindi huo wa jumla wa mashindano ya Mei Mosi yaliyofanyika mjini Iringa mwaka huu, lakini aliwataka kuulinda ushindi huo na kuongeza vikombe vya michezo mingine, ambayo hawakutwaa nafasi ya kwanza.

“Nawapongeza Uchukuzi Sports Club kwa kutwaa ubingwa, lakini kwa kweli kushinda ni jambo rahisi, lakini kuulinda ushindi huo ni jambo gumu sana, hivyo nawataka muulinde ubingwa huo na muongeze mataji mengine, “alisema Chamuriho.
Alisema kuwa lazima Uchukuzi waendelee kubaki namba moja katika michezo, hivyo alisema watafanya kila linalowezekana kuhakikisha wanaendelea kung’ara katika michezo yote watakayoshiriki.

 Mbali na kuzindua bonanza la kwanza la sekta ya Uchukuzi, pia Chamuriho alizindua rasmi mazoezi ya USC kwa ajili ya mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara na Tawala za Mikoa, Shimiwi, ambayo mwaka huu itafanyika mjini Dodoma mwaka huu.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari (kushoto) akiwafanyisha mazoezi wafanyakazi wa Uchukuzi, akiwemo Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Dk Leonard Chamuriho  (mwenye track suit) leo.
Pia aliwasisitizia kuwa atajitahidi kutatua changamoto zinazoikabili USC ili kuhakikisha klabu hiyo inatekeleza majukumu yake vizuri ya kuendeleza michezo na kuwawezesha wafanyakazi wa Uchukuzi kuwa na siha bora.

Katibu Mkuu wa USC, Mbura Tenga wakati akimkaribisha mgeni rasmi alisema kuwa lengo la bonanza hilo ni kuwakutanisha wafanyakazi wa wizara bila kujali kada zao, jinsia, rangi au dini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Dk Leonard Chamuriho (mbele) wakati wa bonanza la michezo la Uchukuzi leo.
Malengo mengine ni kukuza, kusimamia na kuongoza shughuli za michezo kwa wafanyakazi, kushirikiana na Shimiwi kuendeleza michezo kwa mujibu wa taratibu zinazojulikana.

Pia kuanzisha na kukuza uhusiano mwema kati ya viongozi wa wizara, wafanyakazi na wizara zingine huku kubwa zaidi likiwa kuitangaza Wizara-Sekta ya Uchukuzi kupitia shughuli zake kupitia michezo.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari akizungumza wakati wa uzinduzi wa bonanza la michezo la Uchukuzi Sports Club leo. Kulia ni Paul RwegashaMkurugenzi wa Kiwanja cha Kimataifa cha Ndege cha Julius Nyerere (JNIA). 
Hivi karibuni USC ilikabidhi makombe 13 ya ushindi wa Mei Mosi kwa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ambapo Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Grayson Mwaigombe alipokea vikombe hivyo kwa niaba ya Chamuriho.

Mbali na mazoezi pia kulikuwa na michezo ya kuvuta kamba, mpira wa miguu, mpira wa wavu na mingineyo, ambayo ilichezwa na wafanyakazi wa Sekta ya Uchukizi, ambao walijitokeza kwa wingi leo.











No comments:

Post a Comment