Sunday 26 August 2018

JNIA Yajidhatiti Kudhibiti Ugonjwa wa Ebola


1.       Mlango wa kuingilia abiria kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), wanaotoka nje ya nchi, ambao baadhi ya ndege zimelengwa kutokana na abiria wake aidha kupita au kuanzia safari kwenye nchi ya Kongo iliyotangazwa kuwepo kwa ugonjwa wa Ebola.

Na Mwandishi Wetu

KITENGO cha Afya katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) kimeweka udhibiti madhubuti wa  kujikinga na usambazaji wa magonjwa ambukizi, ikiwemo Ebola.

Ugonjwa wa Ebola unaosambazwa kwa virusi vya Ebola, husababisha homa kali inayoweza kuambatana na kutokwa damu mdomoni, puani, masikioni, machoni na sehemu nyingine za wazi na unaenea kwa haraka. Hivi karibuni  umetangazwa kutokea nchini Kongo na kusababisha vifo.
Eneo maalum la ukaguzi wa afya kwa abiria mara baada ya kuingia kwenye sehemu ya wanaowasili kutoka nje ya nchi, ambapo kumefungwa mashine maalum zenye kuonesha joto la mwili na likizidi 38 abiria huyo hufanyiwa mahojiano ya afya yake, kwa kuwa moja ya dalili za ugonjwa wa Ebola ni kuwa na joto kali

Akizungumzia kuhusiana na mikakati hiyo ya kupambana na magonjwa ambukizi ukiwemo wa Ebola,  Ofisa Afya Mfawidhi wa JNIA, Dk. George Ndaki alisema wanatoa mafunzo kwa watumishi na wahusika wote wanaotumia kiwanja hicho katika kujikinga na magonjwa hayo.

“Sisi tumejiandaa vizuri na tumeshafanya jitihada zote tumeshatoa maelekezo, mafunzo na kamati mbalimbali za kiwanja zimejipanga kudhibiti magonjwa yote ya kuambukiza, ikiwemo sisi wenyewe kujikinga na kuwakinga na abiria wote wanaotoka katika nchi hatarishi”, alisema Dkt. Ndaki.

Aidha, akizungumzia kuhusiana na utaratibu ambao Kiwanja kimeweka ili kuhakikisha abiria wenye maambukizi wanapokelewa kwa tahadhari, ambapo wanapowasili na ndege zinazotoka nje ya nchi zinazopakia abiria wanaosafiri kutoka katika nchi zinazoshirikiana na Kongo hutakiwa kusafisha mikono kwa dawa maalum mara waingiapo katika eneo la kuwasili.

1.        Mmoja wa abiria aliyewasili na ndege ya Rwanda Air kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), akinawa mikono kwa dawa maalum inayoua vijidudu vya maradhi mbalimbali yanayoambukiza, ukiwemo Ebola uliotangazwa hivi karibuni umeibuka nchini Kongo.

 Pia abiria hao wanapoingia katika lango la kuwasili la abiria kutoka nje ya nchi, kumekuwa na mashine maalum inaangalia joto la mwili na likizidi nyuzi joto 38 wanamtaka kutoa maelezo zaidi ya afya yake.

“Abiria wote wanapowasili hupita katika eneo maalum ambalo wote hutakiwa kuosha mikono, lakini pia kuna mashine ambazo zimewekwa ili kuweza kuwatambua abiria ambao wanawasili wakiwa na hali ya joto isiyokuwa ya kawaida mfano kuwa na joto la juu sana kuanzia 38oC, ukiachana na hilo kuna fomu maalum ambazo abiria wanapowasili hujaza na pia taarifa kutoka kwa rubani wa ndege kama kuna abiria ana maambukizi kwenye ndege. Baada ya kumtambua mgonjwa basi atapitishwa katika njia ya tofauti na abiria wengine na kupakiwa katika gari la wagonjwa na kupelekwa Temeke Hospital,” alisema Dk. Ndaki.

1.       Ofisa Afya Mfawidhi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Dkt. George Ndaki akionesha mashine maalum inayompima abiria (thermo scanners) mara anapopita eneo la ukaguzi wa afya, ambapo linakuwa likisomwa na Afisa Afya kwenye komputa iliyopo (kulia). JNIA wamejidhatiti na makonjwa ya milipuko ukiwemo wa ebola uliotangazwa kuwepo nchini Kongo.

 Naye Mkurugenzi wa JNIA, Bw. Paul Rwegasha akitoa ufafanuzi juu taarifa za uwepo wa ugonjwa wa Ebola, ameeleza kuwa tayari JNIA wanazo taarifa za mlipuko wa ugonjwa huo na taratibu zote zimeshachukuliwa kwa kuwakagua abiria wanaotoka nje ya nchi.

“Kwanza kabisa kwa abiria wote ambao wanatokea katika nchi ambazo zinasadikika kuwa na maambukizi wanapowasili wanakuwa sanitized (wanaosha mikono na dawa maalum) ili wasiweze kuleta maambukizi ndani, lakini pia tuna thermo scanners  (mashine ambazo zinaangalia hali ya joto la mtu) anapowasili ambapo tunapogundua mgonjwa anamatatizo tunapeleka isolation (Chumba cha wagonjwa wa kipekee) na baada ya hapo anapelekwa katika vyumba vya waonjwa waliotengwa katika hospitali ya Temeke” alibainisha Bw. Rwegasha.

1.        Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Paul Rwegasha (kulia) akizungumza na waandishi wa habari juu ya udhibiti wa magonjwa ya mlipuko kwenye kiwanja hicho. Hivi karibuni ugonjwa wa Ebola umetangazwa kutokea nchini Kongo.


Katika hatua nyingine Dk. Ndaki alisema mpaka sasa hakuna mgonjwa yeyote ambaye amebainika kuwa na ugonjwa wa Ebola kupitia JNIA.

Dk Ndaki ametaja namna ya kujikinga na ugonjwa wa Ebola ni pamoja na kuepuka kugusa damu, machozi, jasho, matapishi, kamasi, mkojo au kinyesi cha mtu mwenye dalili za ugonjwa; pia mtu hatakiwi kugusa, kuosha au kuzika maiti ya aliyekufa kwa Ebola; pia usiguse au kula wanyama kama popo, sokwe au swala wa msituni.

Dalili za Ebola ni pamoja na homa kali, maumivu ya kichwa na misuli, mwili kulegea, kutapika, kuharisha, vipele ma kutokwa damu


“Natoa wito tu kwa wananchi kuhakikisha wanafuata taratibu zote tulizoziweka ili kuhakikisha kwamba hatupati mgonjwa yeyote katika nchi yetu. Kama kila mtu atatekeleza wajibu wake kwa abiria kufuata taratibu, wanaosimamia masuala ya afya wakitimiza wajibu wao, na Kiwanja kikitimiza wajibu wake basi hakika magonjwa ya mlipuko hayataweza kufika katika nchi yetu” alieleza Dkt. Ndaki.


No comments:

Post a Comment