Saturday 11 August 2018

Mamia Wamzika King Majuto Kwao Tanga


Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAELFU ya wakazi wa mkoa wa Tanga leo walijitokeza kumsindikiza katika nyumba yake ya milele msanii mkongwe wa maigizo nchini,  Amri Athumani au King Majuto (70) aliyefariki dunia Jumatano usiku katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili alikokuwa akipatiwa matibabu.

Majuto alifikishwa Muhimbili June 12 akitokea nchini India katika hospitali ya Apollo alipokuwa akipatiwa matibabu ya tezi dume, ambapo alikuwa chini ya uangalizi wa afya yake kabla ya umauti kumkuta.

Majuto ambaye alizaliwa mwaka 1948 alizikwa  katika makaburi ya kijijini kwao Kiruku katika Kata ya Mabokweni jijini hapa.

Katika msiba huo wa kihistoria, Mkuu wa mkoa wa Tanga Martine Shigella pamoja na mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Henry Shekifu, waliongoza mamia ya waombolezaji wakiwemo viongozi wa Serikali na Chama cha Mapinduzi.

Viongozi wengine ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Mkuu wa wilaya ya Tanga, Thobias Mwilapwa, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nicholaus William.

Wengine ni pamoja na viongozi wa dini mbalimbali nchini.

Katika salamu zake za mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigella aliwataka wasanii kutokuwa na ubaguzi, wawe na umoja na kuweka utaratibu wa kumbukumbu za kazi za wasanii waliotangulia mbele za haki.

"Mzee Majuto hakuwa na ubaguzi na kwa upande wangu alikuwa rafiki yangu mkubwa, wasanii nawaomba muwe na utaratibu wa kuweka kumbukumbu kwa wasanii waliotangulia mbele za haki," alisema.

Aliongeza: "Tutaendeleza sanaa ya mzee Majuto iwe kumbukumbu katika maisha yetu na nataka niwahakikishie kuwa mimi binafsi Martine Shigella na Mkuu wa Mkoa wa Tanga nitatoa ushirikiano katika familia ya Mzee Majuto watakapohitaji," alisema.

Mbali na viongozi hao pia wasanii mbalimbali wa Bongo Movies walikuwepo akiwemo, Steve Nyerere, Claud, Mpoki, Wema Sepetu, JB na wengineo wengi.

Katika kuonesha kuwa jamii ya Watanzania imeguswa na msiba huo wa msanii huyo nguli na kuonesha mapenzi kila mtu alikuwa akigombea kubeba jeneza lililobeba mwili wa marehemu wakati linapelekwa msikitini wa Donge, ambapo ibada ya mazishi iliongozwa na shekh mkuu wa mkoa wa Tanga, Juma Luwuchu kwa ajili ya kuswaliwa.

HALI ILIVYOKUWA
Katika msiba huo licha ya wakazi wengi kuhudhuria pia ilionekana kama baadhi yao walifika kuwashangaa wasanii nyota wa filamu, ambao wamekuwa wakiwaona katika runinga wakifanya vitu vyao, ambapo walikuwa wakisukumana ili kuwaona mubashara.

SIKU YA JUMATANO
Mkoani Tanga wakati mwili wa marehemu Mzee Majuto unapita katika barabara kuu ya Chalinze-Segera-Tanga ulionekana msafara kuwa ni mkubwa kutokana na watu wengine kuusimamisha na kutaka kupewa fursa ya kuona jeneza lake na kusababisha msongamano mkubwa.

Hali hiyo ilisababisha kuchelewesha msafara huo na kuingia Tanga majira ya saa saba usiku.

Pia nyumba za kulala wageni zilijaa mapema baada ya watu kutoka mikoa mbalimbali nchini na hata nje ya nchini kufurika Tanga kwa ajili ya kushiriki msiba wa nguli huyo wa uchekeshaji nchini.

No comments:

Post a Comment