Monday 14 May 2018

Simba Watua Bungeni, Wabunge Wapagawa


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jana lilipuka kwa shangwe baada ya mabingwa wapya wa soka kutinga katika chombo hicho cha kutunga sheria nchini.

Shangwe hizo zililipuka baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Najma Giga kutangaza kwamba timu hiyo imekuja bungeni  kutembelea, hali iliyofanya wabunge kushindwa kujizuia na kuinuka kwenye viti huku wakishangilia, wengi wao wakionesha vitabu vya bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ambavyo vilikuwa vya rangi nyekundu.

Hali hiyo ilitokea baada ya kipindi cha maswali na majibu na iliwachukua wabunge takriban dakika tatu kushindwa kuficha hisia zako na kushangilia na wengi wao wakisema ‘This is Simba’, msemo ambao umekuw ukisemwa na msemaji wa klabu hiyo, 

Haji Manara na sasa umekuwa maarufu zaidi kwa mashabiki wa timu hiyo.

Miongoni mwa wabunge walionogesha bunge ni Mbunge wa Lushoto, Shaaban Shekilindi (CCM) ambaye alionesha fulana jezi ya Simba iliyoandikwa ‘Simba Bingwa  2018-2019, huku akiizungusha na kuzidisha shangwe, huku Mbunge wa Mbozi, Pascal Haonga(Chadema) alionesha juu tai nyekundu.

Awali, akikaribisha timu hiyo, Giga alisema timu hiyo imekuja na viongozi 10 na wachezaji 48 na kuwataja viongozi hao kwa majina wakiwemo Salim Abdallah, Aden Rage, Mohamed Dewji, Idi Kajuna, Haji Manara, Richard, Kocha Pierre, Masoud Juma na mwisho akamtambilisha Emmanuel Okwi na kuufanya ukumbi wa bunge kulipuka ingawa wapo waliomkosoa kwa kutosimama kama wenzake walivyokuwa wakitambulishwa.
Okwi ndiye mfungaji bora hadi sasa wakati ligi hiyo ikielekea ukingoni.

Mara baada ya wachezaji hao kusimama Wabunge walianza kushangilia huku baadhi wakipiga makofi na viti kuonesha kufurahishwa na ujio wa timu hiyo ambapo Giga aliingilia “Waheshimiwa,Waheshimiwa Wabunge naomba tusikilizane naamini kabisa vifijo hivi vimesaidiwa na Wabunge ,mashabiki wa Yanga kwa vile ni waungwana”.

Kabla ya timu hiyo kutambulishwa, wabunge wakati wakiuliza maswali na mawaziri kujibu wengi walikuwa wakieleza furaha yao kwa timu hiyo kunyakua ubingwa.

No comments:

Post a Comment