Sunday 23 July 2017

Wanariadha waahidi medali mashindano ya dunia

Mkuu wa Uhusiano wa Multichoice Tanzania, Johnson Mshana (Kushoto) akimkabidhi Balozi maalum wa DStv Alphonce Simbu (Kulia) wakati wa ziara ya ofisa huyo katika kambi ya mazoezi ya timu ya taif ya riadha inayojiandaa kushiriki mashindano ya dunia London mwezi ujao.
Na Mwandishi Wetu, Arusha
Balozi Maalum wa DStv na moja ya wanariadha wanaounda timu ya taifa itakayoshiriki mashindano ya riadha ya Dunia mwaka huu yatakayofanyika mwezi ujao jijini London, Uingereza, Alphonce Simbu, amesema watanzania watarajie medali kutoka kwa timu hiyo kwani wamejiandaa vizuri.

Akizunngumza wakati wa ziara maalum ya Ofisa Mwandamizi wa DStv, Johnson Mshana katika kambi hiyo iliyopo Ilboru Arusha ambapo pia alishuhudia mazoezi ya timu hiyo, Simbu alisema kuwa yeye na wenzake wamejiandaa kikamilifu kuhakikisha kuwa wanaleta medali nyumbani katika mashindano hayo makubwa yanayofanyika mapema mwezi ujao.

 “Tumejiandaa vizuri na tuna matumaini makubwa ya kushinda. Tumekuwa tukifanya mazoezi mazito na tuko sawasawa kupambana katika mashindano hayo, ” alisema Simbu.
Naye Meneja Uhusiano wa Multichoice Tanzania, Mshana ambayo alitembelea kambi hiyo na kisha kushuhudia mazoezi alisema kampuni yao imefurahishwa sana na mwenendo wa kambi hiyo pamoja na timu nzima.

 “Wakati wote tunapoamua kusaidia katika maandalizi ya timu tunafahamu fika kuwa timu yoyote bila ya maandalizi ya kutosha haiwezi kufanya vizuri kwenye mashindano yoyote yale. Hii ndiyo sababu iliyotusukuma DStv kusaidia katika juhudi hizi za kuiandaa timu yetu ya Taifa itakayokwenda kuwakilisha nchi katika mashindano ya dunia. Tunataka Watanzania tushuhudie medali zikija nyumbani.”

Alisema baada ya DStv kuanza kumdhamini Simbu takriban mwaka mmoja uliopita, wameshuhudia mafanikio makubwa sana, ambayo yamewatia moyo sana kuongeza nguvu ili kuiimarisha zaidi timu ili hatimaye iweze kufanya vizuri zaidi na kulikwakilisha vyema taifa kwenye michuano ya kimataifa.
“Tulianza na Simbu, amefanya vizuri, ameshinda, sasa tunaongeza wigo wa ushindi kwa timu yetu ya Tanzania na tunaamini tutashinda, mbali na hayo DStv ilionesha mubashara Mumbai Marathon tukamuona Simbu akishinda, Tukaonesha Mubashara London Marathon, tukaona Simbu akivunja rekodi yake, na tutaonesha mubashara Mashindano ya Dunia Mwezi Agosti, ambapo bila shaka kwa nguvu hii, tutashuhudia tukikwapua medali kedekede na kuliletea taifa letu sifa kubwa, ” alisema Mshana kwa kujiamini.

Naye Kocha wa timu hiyo Francis John, alisema kuwa kazi kubwa imefanywa na makocho wanaoinoa timu hiyo hapo kambini na kutokana na ushirikiano mkubwa kati ya makocha na wachezaji umefanya mazoezi yao kwenda vizuri.
Alisema wanatarajia kuwa wanariadha hao watafanya vizuri,  kwani hata mmoja wao aliyekuwa na matatizo ya magoti sasa anaendelea vizuri na bila shaka atashiriki vizuri kwenye mashindano hayo.

Alisema  jumla ya wachezaji saba  wakiwemo wanawake watatu na wanaume wanne watashiriki, ambao ni Failuna Abdi  atashiriki mbio za meta  10,000, Gabriel Gerald (meta 5,000), huku Magdalena Krispin, Sarah Ramadhani, Said Makula, Ezekiel Jafar Ng’imba na Alphonce Felix Simbu wenyewe watashiriki mbio za marathon.

Huku Emmanuel Giniki akiongeza idadi ya washiriki kwa timu ya Tanzania baada nay eye juzi kufuzu katika mbio za meta 5,000 baada ya kufanya vizuri katika mbio za kimataifa nchini Ubelgiji.
Giniki alimaliza katika nafasi ya saba kwa kutumia dakika 13:13:24 na kuongeza idadi ya washiriki wa Tanzania kufikia wanariadha nane.
Aidha, timu hiyo ya taifa ya Tanzania inatarajia kukabidhiwa bendera Julai 31 katika Hoteli ya Kilimanjaro jijini Dar es Salaam tayari kushiriki mashindano hayo ya dunia yatakayoanza Agosti 3 hadi 15.

Mashindano hayo sio mchezo kwani kwa mara ya mwisho Tanzania iliata medali mwaka 2005 yaliofanyikia Helisinki, Finland wakati Christoher Isegwe alipotwaa medali ya fedha baada ya kumaliza katika nafasi ya pili katika mbio za marathon.

No comments:

Post a Comment