Saturday 22 July 2017

Mtanzania atinga fainali Michezo Madola Bahamas

Nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania inayoshiriki Michezo ya Sita ya Vijana ya Jumuiya ya Madola, Regina Mpigachai.

Na Mwandishi Wetu
MWANARIADHA wa Tanzania Regina Mpigachai ametinga fainali ya mbio za meta 800 katika Michezo ya Jumuiya ya Madola kwa vijana inayoendelea Nassau, Bahamas.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari, Mpigachai alipangwa katika kundi la pili la mchujo na alimaliza mbio hizo akiwa katika nafasi ya tano kwa kutumia dakika 2:11.65.

Kundi la mchujo la mwanariadha huyo lilikuwa na wachezaji nane na alifuzu kucheza fainali baada ya kuwa mmoja kati ya wanariadha waliokuwa na muda mzuri zaidi licha ya kutokuwemo katika tatu bora.

Mshindi wa kwanza katika kundi la Mpigachai alikuwa Anna Lilly aliyetumia dakika 2.11.65 wakati mshindi pili ni Carlet Thomas.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi alisema kuwa, Mpigachai kwanza ameboresha muda wake binafsi mpya baada ya ule wa awali wa dakika 2.13.51 aliouweka katika mashindano ya Kanda ya Tano yaliyofanyika Uwanja wa Taifa.

Bayi aliongeza kusema kuwa mwanariadha huyo pia pamoja na kumaliza watano, lakini muda wake ulikuwa bora zaidi akiwazidi wanariadha wote watatu wa kundi la mchujo wa kwanza waliotumia dakika 2.12.21, 2.12.84 na 2.12.86.

Wakati huohuo, mwanariadha mwingine wa Tanzania Francis Damian alitinga moja kwa moja katika fainali baada ya washiriki wa mbio hizo kuwa wachache.

Wanariadha wengine katika mbio hizo ni kutoka Kenya (mmoja), Canada (wawili), New Zealand (mmoja) na Scotland (mmoja).

No comments:

Post a Comment