Sunday 16 July 2017

Karia Atuma Salamu za Rambirambi Kwa Mwakyembe kwa kifo cha mkewe Linah

Na Mwandishi Wetu
Kaimu Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa msiba wa  Linah George Mwakyembe – mke wa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Linah amefariki usiku wa kuamkia jana Julai 15, mwaka huu kwenye Hospitali ya Aga Khan alikokuwa akipatiwa matibabu. Mipango ya mazishi inafanyika nyumbani kwa Waziri Mwakyembe, Kunduchi jijini Dar es Salaam.

“Hakika nimeshtushwa na taarifa za kifo cha Linah ambaye nimejulishwa kimetokea jana katika Hospitali. Kifo hiki kimeleta huzuni kubwa kwa wanafamilia ya michezo hususani mpira wa miguu.

“Natuma salamu za rambirambi kwako Mheshimiwa Waziri wetu mpendwa. Hakika Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba huu. Ni pigo kubwa katika familia, lakini kwa wakati huu mgumu, Mheshimiwa Mwakyembe, familia yake, ndugu jamaa na marafiki hawana budi kuwa watulivu na wenye subira,” amesema Karia.

“Naungana na familia ya Mwakyembe katika msiba huu ambao pia ni msiba wetu sote wanafamilia ya mpira wa miguu. Naungana nao pia kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke peponi roho ya Marehemu Linah Mwakyembe. Amina.”

No comments:

Post a Comment