Saturday 15 July 2017

Vijana wa Madola waondoka na matumaini kibao

Wachezaji wa timu ya taifa ya Tanzania itakayoshiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 pamoja na viongozi wa Kamati ya Olimpiki (TOC) kabla timu hiyo haijapanda ndege kwenda Bahamas leo jioni.
Na Mwandishi Wetu
TIMU ya Tanzania itakayoshiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 imeondoka leo nchini kwenda Nassau, Bahamas ikitamba kuwa itafanya vizuri katika michezo hiyo itakayoanza kutimua `vumbi' Jumatano Julai 19.

Tanzania katika michezo hiyo ya sita ya Jumuiya ya Madola kwa wachezaji wa umri chini ya miaka hiyo imepeleka wachezaji wanne tu, wawili wawili wa mchezo wa riadha, Mwinga Mwanjala  na kuogelea, Amir Twalib Abdullah, ambao walitamba timu zao kufanya vizuri katika michezo hiyo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), makocha hao walisema kuwa timu zao zitafanya vizuri kwani wamejiandaa kwenda kushindana na sio kushiriki.

Mwanjala ambaye wachezaji wake ni Regina Mpigachai na Francis Damiano watakaoshiriki mbio za meta  800 na 3,000.wakati waogeleaji ni  Celina Itatiro na Colin Saiboki, ambao watashiriki katika michezo ya aina tofauti tofauti.

Wachezaji hai nao walisema watafanya vizuri katika michezo hiyo kwani wamefanya mazoezi kwa muda mrefu.

Timu hiyo imeondoka leo kwa ndege ya Emirates kupitia Dubai na wanatarajia kurudi nchini Julai 24 siku moja baada ya michezo hiyo kufungwa rasmi Julai 23.
Timu hiyo iliagwa rasmi juzi katika ofisi za Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) na Rais wa TOC Giulam Rashid, ambapo walitakiwa kwenda kupambana ili kuliletea sifa taifa kwa kufanya vizuri mkatika michezo hiyo.

Makamu wa Rais wa TOC Henry Tandau aliwataka wachezaji hao kuondoa uoga na kwenda kushindana katika mashindano hayo na sio kuogopa chochote kwani wanatakiwa kujiamini.
Nahodha wa timu hiyo, Mpigachai alisema kuwa wamejiandaa vizuri na wanajiamini watafanya vizuri katika mashindano hayo, ambapo amewataka Watanzania kuwaombea.
Nahodha wa timu ya Tanzania, Regina Mpigachai akizungumza baada ya kukabidhiwa bendera katika ofisi za TOC jijini Dar es Salaam juzi.
Kwenye Uwanja wa Ndege, timu hiyo ilisindikizwa na Makamu wa Rais wa TOC, Henry Tandau, Katibu Mkuu Filbert Bayi, mjumbe wa Kamati ya Ufundi ya TOC, Peter Mwita na Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday na mjumbe wa RT, Tullo Chambo na waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali.
Kocha wa timu ya taifa ya riadha na Mkuu wa Msafara wa timu ya Jumuiya ya Madola ya Vijana, Mwinga Mwanjala akizungumza baada ya timu hiyo kukabidhiwa bendera.


No comments:

Post a Comment